KISWAHILI KINA WENYEWE

Mvuvi

Ndimi mvuvi halisi, kulla vuvi nalijuwa
Nivuwaye mikambisi, na papa wenye khatuwa
Wala sivui vingisi, mishipi haisumbuwa
Nimekwambiya elewa

Sivuwi bahari ndogo, hatia nanga fuoni
Havisimbika vigogo, vilivyozama majini
Na wala Sivuwi ngogo, vidagaa na mbinini
Siwavui asilani

Jabali hulijilisi, jishipi nikalitupa
Haotea mifulusi, na nguru na mijipapa
Si kasikazi si kusi, khabari yangu nakupa
Wala sivui kwa pupa

Na nivuapo malema, huingia ndani ndani
Maji yangu ni ya pima, thalatha u thalathini
Na ndiyo ninayozama, lema halibwaga tini
Uliza mimi n’nani?

Na nivuapo maziyo, mavuvi ya kizamani
Kwa hino hali niliyo, huvua kwa kutamani
Hatafuta kiteweyo, cha wali mwema kombeni
Haandaa siniani

Ela uvuvi wa juya, kuvua siutamani
Sababuye ‘takwambiya, ufahamiwe mwendani
Ni kwambakwe huingiya, samaki waso thamani
Kama wewe mwafulani

Ni kuu yangu bahari, elewa sana elewa
Huko hakwendi vihori, wala vyenu vimashuwa
Shoti nahodha hodari, kisha ende kwa ngalawa
Na milango kuijuwa

“Malenga wa Mvita: Diwani ya Ustadh Bhalo Ahmad Nassir” ukurasa wa 34

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.