ZANZIBAR DAIMA PUBLISHING

Maria, Tanzanian Woman and Plus

Maria Sarungi
Very few activists have managed to stand still against the mounting pressure of Tanzanian regime nowadays. Maria Sarungi is one them. She is a woman and plus.
UCHAMBUZI

Je, Tanzania yaweza kupata maendeleo ya kiuchumi kwa kubaka demokrasia?

Shutuma kwamba utawala wa awamu ya tano wa Rais John Magufuli unaibinya roho demokrasia changa ya taifa hili kubwa kabisa Afrika Mashariki zina mashiko yake kwa kuangalia rikodi ya yale yanayotendwa dhidi ya vyama vya upinzani na viongozi wao, asasi za kijamii na hata vyombo vya habari, viwe vipya ama vikongwe.

Lakini wale wanaokosoa kwamba utawala huu unafanya mambo bila ya kuwa na itikadi au falsafa maalum inayouongoza, nao pia wanakosea. Ukweli ni kuwa kinachofanywa sasa na Rais Magufuli na timu yake kina mashiko yake kwenye mojawapo ya matapo makongwe kabisa kwenye taaluma ya uchumi wa kidola.

Tapo hilo ni lile linaloamini kwamba, kwanza, maendeleo yana tafsiri ya ukuwaji wa uchumi kupitia miundombinu na ubanaji matumizi na, pili, maendeleo hayo yanawezekana pale tu ambapo pana mfumo wa kirasimu na utawala wa mkono wa chuma. Ushahidi wa wanaoamini hayo wanautoa kwenye mifano ya Rwanda na baadhi ya mataifa ya Amerika Kusini na Asia, ambayo ni kigezo cha namna udikteta unavyofanikiwa kuimarisha maendeleo ya kiuchumi.

Wasomi akina Walter Galenson, Karl De Schweinitz na Samuel Huntington wanahoji kwamba demokrasia inajikita zaidi kwenye mahitaji ya muda mfupi ambayo yanagharimu uwekezaji na ukuwaji wa uchumi. Kwa maoni yao, “demokrasia inatishia faida na, hivyo, kupunguza uwekezaji na basi haiendani na maendeleo ya kiuchumi.“ Watetezi hao wanahoji kwamba udikteta una uwezo mkubwa zaidi wa kulazimisha upatikanaji wa akiba na hatimaye kuanzisha ukuwaji mkubwa wa uchumi.

Akitetea mtazamo huo, Vaman Rao aliandika maneno haya mwaka 1984: “Maendeleo ya kiuchumi ni mchakato unaohitaji uwekezaji mkubwa wa rasilimali watu, vitu na fedha. Mipango ya uwekezaji kama huo inahusisha makato kwenye matumizi ambayo yanaweza kuwa machungu sana kwa watu wa chini ambao ndio wengi wao kwenye mataifa yanayoendelea. Serikali zinapaswa kuchukuwa hatua kali kabisa na kulazimisha zitekelezwe kimabavu ili kuweza kuzalisha ziada inayohitajika kwa uwekezaji. Endapo hatua hizo zitapigiwa kura na wananchi, hapana shaka zitashindwa. Hakuna chama chochote cha siasa kinachoweza kutegemea kushinda uchaguzi wa kidemokrasia kwa kutumia hoja ya kuwataka wananchi wajitowe muhanga leo ili wawe na maisha mazuri kesho.” (Tafsiri ni yangu).

Na Mohammed Ghassani

Hadi hapo, kwa wale wanaodhani kuwa chini ya Rais Magufuli, Tanzania inaendeshwa mzobemzobe huku mkuu akiwa hajuwi aendako, wanapaswa kuhakiki upya wanayoyaamini. Inawezekana muda wa kuwepo kwake madarakani usitoshe kumfikisha anakolunga, lakini haina maana kuwa hakujuwi – angalau kwa kuzingatia tapo hili la kitaaluma ya uchumi wa kidola.

Ubakaji demokrasia hauwezi kuwa dawa ya ukuwaji uchumi

Lakini je, kwa kuungwa kwake mkono na wasomi kama hao niliowataja, kunaufanya mtazamo wa kuyachagua maendeleo kwa gharama ya kuiua demokrasia kuwa sahihi? Jibu langu ni hapana. Mtazamo huu si sawa hata kidogo, kwa sababu sio tu kwa kuwa una fasili finyu sana ya maendeleo (kwa kusisitiza ukuwaji wa uchumi kupitia uwekezaji wa miundombinu pekee), bali pia unapingana na hata ushahidi wa wazi na tafiti kadhaa za kisayansi duniani, zikiwemo zile zilizofanywa kwenye mataifa yetu ya Dunia ya Tatu na yale yaliyojikwamua kiuchumi yaitwayo sasa Dunia ya Kwanza.

Wasomi Douglass C. North na Barry R. Weingast, kwa mfano, waliandika hivi mwaka 1989: “Dola ya kikandamizaji kila siku inakuwa tayari kuigeuza jamii kuwa windo lake kwa kisingizio cha kujenga uchumi. Ni taasisi za kidemokrasia pekee ndizo zinazoweza kuizuwia dola hiyo kwa maslahi ya umma. Udikteta wa aina yoyote ile ni chanzo kikuu cha ukosefu wa ufanisi, maana serikali ambayo jukumu lake la msingi ni kuweka mfumo wa kulinda uwekezaji, uzalishaji na usambazaji inajigeuza kuwa ndio mtendaji wa pekee wa kila kitu.”

Dunia ni shahidi wa kupinduka kwa maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kibinafsi kwenye mataifa yaliyoujaribu udikteta hata katika yale ambayo leo hii utawala wa Rais Magufuli unayachukulia kuwa ni kigezo cha kufuatwa. Kuanguka kwa uchumi wa Nicaragua chini ya dikteta Somoza, wa Jamhuri ya Dominik chini ya Trujillo, Ufilipino chini ya Marcos na Ulaya ya Mashariki chini ya tawala za kikomunisti si mambo ya kuigwa.

Athari za ubakaji wa demokrasia ndani ya ‘Tanzania ya Magufuli’

Ndani ya kipindi hiki kifupi cha utawala wa awamu ya tano unaoikanyaga misingi ya kidemokrasia, Tanzania imo kwenye wakati mgumu sana kimaendeleo. Hali ya maisha imezidi kuwa ngumu, imani ya wananchi kwa mfumo inapotea na imani ya wawekezaji wa kati na wa juu inatikisika, licha ya ripoti za kutunga zitolewazo na taasisi za kidola kuonesha kuwa mambo yako shwari.

Bei za bidhaa muhimu kwa matumizi ya kila siku kama vile unga, mchele, sukari na madawa ni ya juu sana, vituo vya afya havina madawa, mashuleni kuna msongomano na ukosefu wa vifaa.

Hoteli kadhaa zimeripoti anguko la asilimia hadi 60 la mauzo yao ndani ya kipindi hiki cha utawala wa Rais Magufuli, huku kukiwa na wimbi la wafanyabiashara wanaohamishia biashara zao nje ya nchi kwa sasa, si kwa kuwa ni wakwepaji kodi kama inavyotakiwa iaminike, bali kwa kuwa hawana hakika ya mitaji yao nchini kutokana na staili ya matamko ya kuripuka na kutaka sifa ya mkuu wa nchi.

Yote haya ni kwa kuwa utawala usiohishimu misingi ya kidemokrasia hukaribisha ghasia – ghasia kwenye nafsi za watu, ghasia kwenye maisha yao, ghasia kwenye mifumo ya kiuchumi na kisiasa. Hizi ni ghasia za kimyakimya lakini zina mahusiano ya moja kwa moja na ukosefu wa maendeleo. Tanzania ya Magufuli – kama mwenyewe anavyopenda kuiita – sasa inapitia kwenye kipindi hicho cha ghasia.

Dawa ni kuimarisha viwili kwa pamoja

Mwaka 1972, muongo mmoja baada ya uhuru wa Tanganyika, Mwalimu Julius Nyerere aliuvunja mfumo uliotoa mamlaka kwa serikali za mikoa kwa minajili ya kuimarisha madaraka na nguvu za serikali kuu iliyopo Dar es Salaam, lakini wakati akikaribia mwisho wa utawala wake, alinukuliwa akisema kwamba: “Kuna mambo ambayo nisingeliyafanya endapo ningeweza kuanza upya. Mojawapo ni kuvunja mamlaka ya serikali za mikoa.”

Hili linatuzinduwa kuwa daima kwenye utawala, jambo la busara ni kutoa uhuru zaidi wa kidemokrasia kwa wananchi na sio kuubana. Ushiriki wa wananchi kwenye uendeshaji wa mambo yao ni jambo la muhimu sana kama jamii hiyo inataka kweli kuyafikia maendeleo.

Ingawa miaka 25 ya siasa za vyama vingi haikuwa na ukamilifu, ikizongwa na matatizo mengi na wakati mwengine ya kuvunja moyo, lakini Tanzania ilikuwa inapiga hatua kidogo kidogo. Hatua hizo zilipaswa kuendelezwa na sio kurejeshwa nyuma kama ambavyo inaonekana wazi hivi sasa.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ina serikali isiyohishimu mgawanyo wa madaraka, isiyohishimu uhuru wa kimsingi kama vile uhuru wa mawazo, uhuru wa kujieleza, na uhuru wa kujiunga na kujikusanya na pia utawala wa sharia, ni taifa lenye utawala uliopoteza uhalali wake wa kidemokrasia, hata kama awali uliingia madarakani kwa kushinda uchaguzi.

Kama kweli tunataka kuwa na maendeleo, tunapaswa kuziunganisha dhana hizi mbili pamoja, kwani kimsingi maendeleo na demokrasia duniani yameungana na uimarishaji wa thamani ya maisha ya binaadamu.

Serikali ya Rais Magufuli inapaswa kuifahamu na kuihishimu mifumo ya kikatiba, vyombo huru vya habari na vyenye kujumuisha wote, asasi imara za kijamii na dhamira ya kweli ya kuelekea utangamano na majadiliano ya kijamii.

Hii ndiyo misingi mikuu ya kufikia lengo la maisha bora. Demokrasia inaweza tu kudumu kama inaonesha, muda wote na mwahala mote, kwamba ni njia bora kabisa ya kufikia lengo hilo.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kabisa na gazeti la Mwelekeo la tarehe 18 Julai 2017.

UCHAMBUZI

Ndiyo kwa ‘uchumagu’, hapana kwa ‘umagukrasia’

Kitu kimojawapo ambacho Rais John Magufuli anajipambanuwa nacho kwa haraka na watangulizi wake, ni tabia yake ya kutokuwa na ajizi na vile kutozingatia kwake mipaka kwenye huko kutokuwa na ajizi. Hayo ni kwa kila alisemalo na kila alitendalo. Kutokuwa na ajizi ni jambo jema kwa kiongozi, lakini kutokuzingatia mipaka si jambo la kusifiwa hata kidogo.

Hapa ndipo ambapo, kwa mwenye akili, anapoweza kirahisi kuchora mstari wa namna ya kumchambua, kumtafakari na kuchaguwa lipi ni lipi kwenye shakhsia ya Rais Magufuli, na kwayo isimuwiye vigumu kujuwa pa kuungana naye na pa kupingana naye.

Kinyume na wanavyochukulia wale wanaojiaminisha kuwa uzalendo hasa ni kumuunga mkono kiongozi wa nchi kwa lolote aliwazalo, alinenalo na alitendalo, utendaji kazi wa Rais Magufuli unawasuta sio tu kwa kutokujuwa kwao maana halisi ya uzalendo, bali pia kwa kuwaonesha kuwa hawana msaada wowote wa maana si kwa Rais Magufuli mwenyewe, wala kwa serikali yake na hata kwa chama chake kinachotawala, CCM.

Ufanyaji wake maamuzi, utoaji wa kauli zake na utendaji kazi wake unatufanya wengine kuona kuwa hata kama hatuna ulazima wa kumuunga mkono kwa kila jambo lake, bado pia hatuna ulazima wa kumpinga kwa kila kitu. Kwamba muna mwahala, kwa mtazamo wetu, anafanya vyema na anahitaji kupewa heko na kusaidiwa na muna mwengine ambamo anafanya vibaya na anapaswa kukosolewa na kuzuiwa.

Uchumagu na Tanzania inayotakiwa

Na Mohammed Ghassani

Binafsi, namuunga mkono Rais Magufuli kwenye hili ninaloliita hapa ‘uchumagu’ – uchumi wa Magufuli, dhana inayowakilisha jitihada zake binafsi kama kiongozi wa nchi kuhakikisha kuwa uchumi wa nchi unakuwa na kuwagusa wananchi wa kawaida, ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakitengwa kando.

Ndani ya jitihada hizi, muna kampeni kubwa ya kupambana na ufisadi, wizi wa mali ya umma, ukosefu wa uwajibikaji na kiwango kikubwa cha uholela kwenye sekta ya umma. Muna pia jitihada zinazoonekana za kuimarisha miundo mbinu na kuwafikia watu kule waliko. Hapana shaka, mafanikio ya kampeni hii ni faida kwa umma na yana athari za moja kwa moja kwa mwananchi wa kawaida.

Hakuna mwenye mapenzi ya kweli kwa nchi, ambaye hataweza kuunga mkono pale, mathalani, watuhumiwa wa ufisadi wanapofikishwa mahakamani kujibu mashitaka dhidi yao. Hakuna pia atakayepinga pale siku maafisa wa serikali waliokuwa wamepewa dhamana kubwa kuwahudumia wananchi na wakazifanyia khiyana dhamana hizo ‘wanayotumbuliwa’.

Ingawa hata watu wanaweza kukosoa njia zinazotumika kwa kuhofia zisije zikawa za zimamoto na kulifanya lengo halisi kutofikiwa, lakini wanajuwa kuwa vita dhidi ya ufisadi ni jambo linalohitajika.

Baada ya zaidi ya nusu karne ya kutawaliwa na chama cha Rais Magufuli, CCM, serikali za pande zote mbili za Muungano zilishageuka kuwa jalala la uchafu wote wa kiuongozi:  kuanzia wizi wa mali ya umma, udugunaizesheni (upendeleo wa kifamilia na kieneo), ubadhirifu, uzembe na ukosefu wa uwajibikaji.

Kwa ujumla, ufisadi umekuwa ni wa kimfumo ndani ya serikali hizi, kuanzia juu kabisa hadi chini kabisa kwa kipindi kirefu sasa. Hata hizo enzi za Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid Karume, ambazo wengine hutaka kutuaminisha kuwa zilikuwa zama za usafi wa kimaadili, ushahidi unaonesha kuwa zilikuwa na makandokando yake mengi na ndiyo hayo yaliyoasisi uovu uliokuja kudhihirika baadaye.

Mwenyewe Mwalimu Nyerere alikuwa akikiri kuwa hata katika uongozi wake kulikuwa na rushwa, lakini alitaka tukubali kuwa yeye na wenzake wachache waliokuwa juu walikuwa hasa wakiichukia rushwa kwa vitendo, na kwamba kila walipopata mashaka na mteule yeyote aliye chini yao kuhusika na rushwa, basi walimchukulia hatua hapo hapo bila kuchelewa na bila kuchelea.

Kwa hivyo, kwamba leo Rais Magufuli anaongoza vita vya kuukomboa uchumi kutoka mikononi mwa ufisadi wa ndani na wa kimataifa na dhidi ya uporaji wa rasilimali unaofanyika kupitia mikataba ambayo serikali zilizoongozwa na chama chake ziliingia huko nyuma, ni wazi kuwa anapigana vita ambavyo anastahiki sifa na kuungwa mkono, hata kama ni vita vinavyotokana na uchafu uliotendwa na chama chake mwenyewe huko tutokako.

Kwa kutumia maneno yake ya tarehe 1 Julai 2017, wakati akifungua Maonesho ya Sabasaba: “Tanzania tumechezewa sana kwa sababu tulitaka kuchezewa. Lakini sasa kuchezewa basi!” Nami nafanya hivyo: namsifu na namuunga mkono. Tanzania kama taifa lilichezewa sana kwenye uchumi wake kwa kuwa wao kama watawala walitaka taifa hili lichezewe. Kufanikiwa kwa Rais Magufuli kwenye vita hivi, ni kufanikiwa kwa taifa zima.

Tanzania haiuhitaji umagukrasia

Lakini kando ya vita vyake hivi, Rais Magufuli anapigana pia vita vyengine, ambavyo mpigaji hasa ni peke yake kwa kuwa ana nyenzo za kumuwezesha kupiga pasi yeye kushambuliwa, na anaowapiga vita hivyo ni mamilioni ya Watanzania ambao hawakubaliani na siasa zake wala dhamira yake. Hapa nitatumia dhana ya ‘umagukrasia’ kuelezea vita vyake hivyo na namna ambavyo mimi siviungi mkono.

Umagukrasia ni aina ya utawala wa kisiasa ambao Rais Magufuli anaujenga, ambao unalenga kumtukuza yeye na chama chake juu ya kila kitu kwa gharama ya kuwadhalilisha wengine wote wasiokuwa wa chama chake au wasiomuunga mkono yeye. Kwa imani kwamba yeye – kama kiongozi mkuu wa dola na chama tawala – anamiliki pekee maarifa yote ya mwelekeo wa taifa na anaongozwa na nia safi isiyo doa kwenye kila anenalo na atendalo, Rais Magufuli hana uvumilivu hata chembe kwa wale wanaomuona tafauti.

Ukosefu wa uvumilivu wake unadhihirika kwa ayasemayo na ayatendayo dhidi ya sauti za ukosowaji ndani ya nchi, akitumia mikono yake aliyonayo kama mkuu wa dola, serikali, chama, na hivyo mwenye kauli ya juu kwenye mihimili mingine yote ya nchi.

Alianza na bunge, chombo kinachopaswa kuwa muhimili huru wa kuisimamia serikali. Kwa namna kilivyotekeleza wajibu wake wa kuikosoa na kuisimamia serikali kwenye awamu iliyopita, inaonekana Rais Magufuli anaamini kuwa ndiko kulikopelekea kwa mara ya kwanza kabisa, chama chake cha CCM kushindwa kuvuuka asilimia 60 ya kura za urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.

Kwa hivyo, kitu cha mwanzo kabisa alichofanya, ni kuliminya bunge kwa kulitenganisha na wananchi wa kawaida, ambao wanaonekana kuathirika na kinachoendelea Dodoma.

Kisha akaenda kwenye vyama vya kisiasa ambavyo vinaonekana kumpinga. Tunashuhudia sio tu kupigwa marufuku kwa mikusanyiko ya vyama hivyo, bali pia kuandamwa kwa viongozi wake wa ngazi mbalimbali, wakikamatwa, kuadhirishwa, kuadhibiwa, kufunguliwa kesi na hata kufungwa jela.

Kisha akaja kwenye vyombo vya habari vya kawaida (televisheni, redio na magazeti) na vya kisasa (hasa mitandao ya Facebook, WhatsApp na blogu), ambako sauti mbadala ya wananchi wa kawaida huwa inasikikana bila kupitia taratibu za kawaida za uchujaji.

Ndani ya kipindi hiki kifupi cha kuwapo kwake madarakani, redio na magazeti kadhaa yameshafungiwa na watumiaji kadhaa wa mitandao hiyo ya kijamii wameshakamatwa, huku wengine wakiripoti kuteswa, wengine wakifunguliwa mashitaka na wengine wakiwa wametoweka bila kujuilikana walipo hadi leo.

Inavyoonekana ni kuwa sasa mkono wa Rais Magufuli unazielekea asasi za kijamii ambazo zinajihusisha na masuala ya haki za binaadamu kwa ujumla wake ama haki za makundi maalum, kama vile vijana, wasichana na wanafunzi.

Haya na mengine ambayo yanafanywa na utawala wa Rais Magufuli katika jitihada zake za kupunguza duara la ukosowaji dhidi yake na kutanuwa duara la ama uungaji mkono wa kulazimisha au ukimya wa khofu, ndicho hicho ninachokiita ‘umagukrasia’.

Mwelekeo unaostahiki

Umagukrasia si jambo la kusifiwa wala kuungwa mkono na yeyote mwenye mapenzi ya kweli na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Taifa hili ilikuwepo kabla ya Rais Magufuli hajakuwa rais na misingi yake ya kitaifa, ikiwemo demokrasia, haki za binaadamu, kijamii na kisiasa na hishima kwa mawazo mbadala – licha ya mapungufu makubwa yaliyokuwa nayo – bado ilianzishwa na kuanza kuengwaengwa kidogo kidogo na waliomtangulia.

Rais Magufuli amekuja madarakani zaidi ya nusu karne tangu Watanzania waanze safari ya kuelekea kwenye utawala wa watu, unaotokana na watu na uliopo kwa ajili ya watu, wakiimarisha hatua kwa hatua taasisi zao za utawala – vyama vya siasa, vyama vya kiraia, vyombo vya habari, bunge, mahakama na serikali yenyewe.

Kama kiongozi mkuu wa dola, serikali na taifa, ana muda wake maalum wa kuwapo hapo. Ukifika atapaswa kuondoka kama walivyoondoka wenzake, lakini hataondoka na nchi hii. Jamhuri hii itabakia na itaendelea baada ya yeye.

Kwa hivyo, anatakiwa sio tu kuiwacha salama kisiasa kama alivyoikuta, bali pia ana wajibu wa kuongezea thamani kwenye misingi hiyo ya kitaifa na kikatiba aliyoikuta na sio kuiangamiza kama anavyoonekana sasa akifanya.

Ndio maana, kwa hilo la umagukrasia, mimi simuungi mkono kabisa kabisa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa mara ya kwanza na gazeti la Mwelekeo la tarehe 4 Julai 2017.

 

UCHAMBUZI

Musiloweza kulisema Tanganyika, mwalisema Zanzibar

Mimi sifichi msimamo wangu dhidi ya ‘siasa’ za huu tunaoaminishwa kuwa ni Muungano wa Tanzania kuelekea Zanzibar, ingawa naweka mpaka baina ya kusimama dhidi ya Muungano wenyewe na kusimama dhidi ya hizo niziitazo siasa za Muungano, maana kwangu hivyo ni vitu viwili tafauti.

Tangu mwaka 2001 nilipoanza kuandika mawazo yangu kwenye vyombo vya habari, mtazamo wangu ni kuwa siasa hiyo inaelezeka kwa sentesi moja tu: Muungano imara kwa Zanzibar dhaifu. Naamini hiyo ndiyo falsafa inayouongoza Muungano wenyewe miongoni mwa viongozi wakuu wa Muungano huo na wafuasi wao.

Kwao wao, ili kuwa na Muungano imara, basi ni lazima uwe na Zanzibar iliyo dhaifu. Ni ipi Zanzibar dhaifu na ni upi Muungano imara? Muungano imara ni ule ambao unahodhi na kumiliki kila kitu cha Zanzibar kwenye kapu lake na kuitawalisha Tanganyika kwenye udhibiti wa kapu hilo. Huo ndio Muungano hasa unaotakiwa na watawala na siasa yao inaakisi ukweli huo.

Na Zanzibar dhaifu ni ile Zanzibar isiyo na mamlaka ya kisiasa kujiamulia mambo yake yenyewe, isiyo na madaraka ya kifedha kusimamia uchumi wake yenyewe, na isiyokuwa na uthubutu wa kuiongoza jamii yake yenyewe. Hiyo ndiyo Zanzibar hasa inayotakiwa na siasa ya Muungano huu na siasa yao inaakisi pia ukweli huo.

Kwa hivyo, kuidhoofisha Zanzibar kwa kauli na vitendo ni sehemu muhimu sana ya kuufanya Muungano uwe na nguvu, uwe madhubuti na udumu milele.

Na Mohammed Ghassani

Kwao wao, ukiwa na Zanzibar yenye nguvu na iliyo imara kwenye uchumi wake, siasa yake na jamii yake, una Muungano ulio dhalili. Ni kama vile wamechora mstari mwekundu baina ya viwili hivi na kisha wanakuradulisha upande mmojawapo wa mstari huo. Ama usimame upande wa Muungano na hivyo uwe sehemu ya udhalilishaji wa siasa, uchumi na jamii ya Zanzibar, au uchaguwe kusimama upande wa Zanzibar na hivyo uwe sehemu ya kuubomoa na kuuvuruga Muungano huo!

Hivyo ndivyo akili zao zinavyofanya kazi na ndivyo inavyodhihirika, kama nilivyosema, kwenye kauli na amali zao. Mifano ni mingi. Nimeiandika mingi huko nyuma tangu wakati wa Rais Benjamin Mkapa, nikafanya hivyo wakati wa Rais Jakaya Kikwete na sasa nafanya hivyo wakati wa Rais John Magufuli.

Ni kama vile ambavyo Marekani isivyoweza kubadilisha msingi wa siasa zake za nje hata akija rais gani, ndivyo ilivyo kwa siasa ya Muungano kuelekea Zanzibar isivyoweza kubadilika hata aje mtawala gani. Wanaweza kubadili kila kitu kuhusu siasa za ndani ya Tanganyika (wenyewe hawataki hata kulisikia hili jina), lakini hawatathubutu kubadili siasa ya Muungano kuelekea Zanzibar.

Leo nazungumzia mfano wa karibuni kabisa ambao umedhihirishwa na Rais Magufuli, wakati akihutubia baada ya kumuapisha Bi Anna Elisha Mghwira wa Chama cha ACT-Wazalendo kuwa mkuu mpya wa mkoa wa Kilimanjaro.

Akionekana kuwajibu wale ambao walimuona kuwa ni mtu wa kigeugeu juu ya uamuzi wake wa kuteua wapinzani kuingia kwenye serikali yake baada ya kujiapiza kuwa kamwe asingelimuigiza Dk. Ali Mohamed Shein wa Zanzibar ambaye amefanya, Rais Magufuli alisema wanaomkosoa hivyo wanapaswa kwanza kujuwa mazingira ambayo alitoa kauli hiyo.

Mwaka mmoja na kidogo uliopita, akiwa kwenye mkutano wa hadhara kuwashukuru wapigakura kisiwani Unguja, Rais Mafuguli akiwa mbele ya Dk. Shein na viongozi wengine wa chama chake na vyama vichache vijiitavyo vya upinzani, alimshangaa Dk. Shein kwa kuwaingiza ‘wapinzani’ kwenye serikali yake.

“Rais uchaguliwe upate asilimia 92, bado unawachukuwa watu wa vyama vingine unawaingiza kwenye serikali yako. Mimi nilipata asilimia 58, hakuna wa chama chengine kule ndani yangu. Na wala hataingia.”

Sasa akihalalisha hatua yake ya kumteua ‘mpinzani’ kuingia kwenye serikali yake, Rais Magufuli akataka aeleweke kimuktadha anapotoa maneno yake.

“Ni lazima watu waelewe nilizungumza hilo nikiwa mahali gani. Nilizungumza nikiwa Zanzibar. Lakini pia msimamo wa kutoteuwa mpinzani kwenye nafasi zangu kumi za wabunge, sitafanya hivyo kweli. Nilishateuwa tisa, nimebakiza moja, na hiyo nafasi moja haitakuwa ya wapizani.”

Kama kuna kitu amekisema kweli kwenye hili basi ni hilo la muktadha wa kutoa kauli zake zinazopishana. Kwenye viwanja vya Kibandamaiti kisiwani Unguja katika ardhi ya Zanzibar, kauli ni kuwa umoja wa kitaifa kwenye serikali hauna maana, madhali huyo aambiwaye ni mshindi ana uhalali wa kuzoa na kukokozoa vyote. Kwenye jengo la Ikulu, katika ardhi ya Tanganyika, kauli ni kuwa nchi inapaswa kujengwa na wananchi wote bila kujali vyama vyao, maana nchi kwanza.

Kwa nini kauli mbilimbili? Jibu limo kwenye ufafanuzi wa awali wa namna siasa ya Muungano inavyofanya kazi yake kuelekea Zanzibar. Waswahili husema kuwa: “Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu”, na kwa mantiki yake ni kuwa kama Zanzibar itakuwa na umoja huo, basi itakuwa na nguvu, na ikiwa na nguvu basi Muungano utakuwa dhaifu.

Kwa hivyo, kwa kiongozi wa juu wa Jamhuri ya Muungano kushadidia utengano wa Wazanzibari kwenye muktadha huu wa uendeshaji nchi, anakusudia hasa kutekeleza kwa vitendo siasa hiyo ya Muungano kuelekea Zanzibar – Zanzibar dhaifu kwa Muungano imara!

Kwa kusema kuwa ahukumiwe kauli zake hizi mbili kwa msingi wa mwahala alimozizungumza, Rais Magufuli anatupa ujumbe wa wazi, ambao kwetu wengine unafahamika kitambo, kwamba linapokuja suala la mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar, basi viongozi wakuu wa Jamhuri ya Muungano si sehemu ya suluhisho, bali sehemu ya tatizo.

Nimesema kuwa huu ni mfano mmoja tu kati ya mingi iliyokwishatokezea huko nyuma, na ambayo mingine kati yao nilipata fursa ya kuielezea. Katika miaka ya mwisho mwisho ya utawala wake, Rais Mkapa alialikwa kwenye shughuli mbili muhimu visiwani Zanzibar – moja ni kuadhimisha Mapinduzi na nyengine Muungano, na mote muwili aliakisi siasa hiyo hiyo ya Muungano kuelekea Zanzibar.

Kwenye sherehe za Mapinduzi, aliwataka waliohudhuria katika viwanja vya Amani, waitikie kwa nguvu “Mapinduzi Daima”, hadi vitukuu na vijukuu vya Waarabu na masultani wa Kiarabu wasikie kuwa kweli Waafrika weusi wa Zanzibar wamechukuwa hatamu za nchi yao. Kwenye jukwaa siku hiyo alikuwepo Rais Amani Karume, mke wake Shadia na watoto wao, ambao kwa hakika ni vijukuu na vitukuu hivyo vya hao Waarabu. Sadfa ni kuwa takribani miaka 10 baadaye, vijana wa Chama chake cha Mapinduzi (CCM), walipita na mabango yanayowataka “Machotara na Mahizbu” kutafuta nchi ya kwenda kutawala, maana Zanzibar si pao.

Wakati akifungua bunge la kwanza kwenye utawala wake mwaka 2005, Rais Kikwete naye akasema kwamba ni ajabu kwamba Wapemba ambao wanafaidika na fursa kadhaa za Muungano huo, wanakuwa wa kwanza kuonesha kujitenga, akirejea matokeo ya chaguzi, ambazo kila mara watu wa kisiwa cha Pemba hupiga kura kuikataa CCM kwa ujumla wake.

Sadfa ikaja ikawa kwamba wakati anaondoka madarakani mwaka 2015, serikali ya umoja wa kitaifa ambayo iliundwa kwa shinikizo la Wazanzibari wenyewe ndani ya kipindi cha mwisho cha muhula wake wa urais, inakufa. Kilichoiuwa ni kuharibiwa kwa uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015 na chama chake, CCM, kupitia vyombo vya dola vilivyokuwa chini yake kama amiri jeshi mkuu.

Kwa hivyo, alichokisema Rais Magufuli kinaakisi kabisa siasa za Muungano kuelekea Zanzibar. Mtazamo wa kuiona Zanzibar iliyozidi kudhoofika, iliyozidi kugawika, na hivyo iliyo rahisi kutawalika na kudhibitika.

Binafsi simuoni kuwa Rais Magufuli, akiwa kama msimamizi mkuu wa siasa hiyo, ana kosa lolote. Kwa hakika hasa, huyu ni kiongozi ‘anayetekeleza’ wajibu wake katika hili, kwa kiwango kile kile ambacho rais wa Marekani anapotekeleza wajibu wake kwenye siasa za nje za taifa lake akiuma na kupuliza kwenye mizozo ya mataifa ya Ghuba na Mashariki ya Kati.

Kosa kubwa litakuwapo pale ambapo yeye na wenzake watataka kutulazimisha sisi kuamini kinyume na hiki wanachokihubiri. Kwa mfano, wakitulazimisha sote tuwaone kuwa wao ni watetezi wa amani, maendeleo na utangamano wa Zanzibar, na kutuadhibu pale tunapowaeleza kuwa hivyo sivyo kabisa walivyo, hapo watakuwa wanatuonea vikubwa!

Kosa jengine kubwa ni kwa hao wanaoelekezewa siasa hii ya Muungano, yaani Wazanzibari wenyewe. Ikiwa zaidi ya nusu karne tangu kubuniwa na kutekelezwa kwa siasa hii, bado hawajang’amua kuwa ipo na inatumika dhidi yao, taifa lao na utambulisho wao, basi hiyo ni dhambi kubwa. Ikiwa wameng’amuwa na wanaipendelea iendelee, basi huo ni uhaini mkubwa dhidi ya taifa lao.

Ama endapo wameng’amuwa na wanaipinga isiwepo, japo kama hadi sasa hawajafanikiwa, hayo ni mapambano ya fakhari. Waendelee nayo hadi pale siasa ya Muungano huu kuelekea nchi yao itakapobadilika, na watawala wafahamu kwamba unaweza kuwa na Zanzibar imara na yenye nguvu, kwa upande mmoja, na wakati huo huo Muungano madhubuti wenyevheshima na adabu kwa pande zote.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kwenye gazeti la Mwelekeo la tarehe 13 Juni 2017