UCHAMBUZI

Magufuli anawauzia Watanzania tamaa ya maendeleo kwa gharama ya demokrasia yao

Kwa hakika, Rais John Magufuli anaonekana kuwalazimisha raia wake kufanya naye biashara ya gizani. Yeye awauzie maendeleo, nao wamlipe kwa gharama ya demokrasia angalau hadi mwaka 2020 wakati wa kampeni za uchaguzi mwengine.

Lakini je, biashara hii inawezekana kwa taifa ambalo lilishaonja ladha ya demokrasia kwa robo karne nzima mtawaliya? Je, ili kupata maendeleo ni lazima kuitia rehani misingi ya kikatiba, mgawanyo wa madaraka, haki za binaadamu na uhuru wa mtu binafsi?

Akizungumzia dhana ya demokrasia, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, anasema: “Demokrasia haihusiani pekee na ile siku moja kila baada ya miaka minne au mitano pale panapoitishwa chaguzi, bali inahusiana na mfumo wa serikali unaohishimu mgawanyo wa madaraka, uhuru wa mawazo, wa kidini, wa kujieleza, wa kujiunga na kujikusanya na pia utawala wa sharia. Utawala wowote unaokanyaga misingi hii, hupoteza uhalali wake wa kidemokrasia, hata kama awali uliingia madarakani kwa kushinda uchaguzi.” (Tafsiri ni yangu).

Dk. Chris Sausman, Mkurugenzi wa Chime Communications Group, anayatafsiri maendeleo kwa umbo la pembe tatu. “Kwanza ni mchakato ambao ndani yake muna mkururo wa hatua zinazopelekea – au zinazotegemewa kupelekea – matokeo ya aina fulani makhsusi, pili ni mkakati ndani ya mipango na sera na, tatu, ni matokeo ya mikondo miwili ya kwanza kupitia kiwango cha mtu binafsi – pale anapokuwa na kuutumia uhuru wake, kiwango cha jamii – pale inapoweza kutoka hatua moja ya kimaisha kwenda nyengine na kiwango cha kiuchumi – pale uchumi wa jumla unapoimarika.” (Tafsiri ni yangu).

Na Mohammed Ghassani

Namna dhana hizi mbili za demokrasia na maendeleo zinavyoungana zinatuambia kuwa biashara anayoifanya Rais Magufuli na Watanzania haitakuwa na mwisho mwema, hata kama sasa kunatolewa takwimu za mapambio.

Kama anavyosema Mkuu wa Madhehebu ya Shia Ismaili duniani, Aga Khan, “kimsingi maendeleo na demokrasia vimeungana na kuimarika kwa thamani ya maisha ya binaadamu. Uwezo wa kuifahamu (na kuihishimu) mifumo ya kikatiba, uwepo wa vyombo vya habari huru na vyenye kujumuisha wote, asasi imara za kijamii na dhamira ya kweli katika kuelekea utangamano na majadiliano ya kijamii. Hii ndiyo misingi mikuu ya kufikia lengo la maisha bora. Demokrasia inaweza tu kudumu kama inaonesha, muda wote na mwahala mote, kwamba ni njia bora kabisa ya kufikia lengo hilo.” (Tafsiri ni yangu).

Tanzania inapitia kwenye moja ya vipindi vigumu sana vya historia yake ya hivi karibuni. Baada ya kujaribu kuujenga mfumo wa kidemokrasia kwa miongo miwili na nusu, sasa jitihada hizo zinarudi nyuma kwa kasi ya ajabu.

Misingi mikuu ya demokrasia inashambuliwa kila uchao na serikali ya Rais Magufuli, akiamini kuwa ana uhalali wa kufanya lolote atakalo kwa kuwa tu madaraka ya juu yamo mikononi mwake.

Hata miaka miwili haijatimia vyema tangu ale kiapo cha utiifu kwa Katiba, Rais Magufuli ameshathibitisha kuwa yeye si muumini wa misingi mikuu ya Katiba yenyewe, kama vile mgawanyo wa madaraka na hishima kwa uhuru na haki za binaadamu.

Kwa mfano, mara kadhaa muhimili wa utawala kupitia kwake na wateule wake, umekuwa ukiingilia muhimili wa bunge kuwafunga midomo wabunge, kuzima mijadala yenye maslahi kwa taifa na hata kuzuwia matangazo ya bunge hilo kuoneshwa moja kwa moja kwenye televisheni ya taifa, ambayo inaendeshwa kwa kodi ya wananchi.

Wakati akizuwia matangazo hayo kwa kisingizio cha gharama na kubana matumizi ya serikali na pia kuwapa muda wananchi kufanya kazi, shughuli za kisiasa zake na za chama chake, CCM, hupewa nafasi ya kurushwa moja kwa moja na vyombo vya habari vya umma, vinavyolipiwa kwa fedha ya umma na katika wakati wa kazi.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, wabunge kadhaa wameshakamatwa, kupigwa, kuwekwa vizuizini na hata kufungwa jela, na katika baadhi ya mifano wakiwa ama bungeni au majimboni mwao katika shughuli zinazohusiana na nyadhifa na madaraka yao kama wabunge na au viongozi wa vyama vyao.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameshatoa kauli kadhaa zinazoingilia moja kwa moja uhuru wa mahakama na vyombo vyengine vinavyohusiana moja kwa moja na upatikanaji haki kama vile ofisi ya mwendesha mashitaka, polisi na idara za upelelezi, kwa kuwatia hatiani hadharani wale wote anaowashuku.

Matokeo yake, kwa kuwa tuna aina ya Katiba inayompa mkuu wa nchi nafasi ya uungu mtu, walio chini yake kwenye vyombo hivyo wanajipendekeza kuigeuza kila “kauli ya rais” kuwa ukweli, hata kama kwa kufanya hivyo wanazikanyaga sheria, kanuni na taratibu tulizojiwekea wenyewe kama taifa.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Tanzania imejikuta ikirejea kwenye zama za giza – ikitajwa kuwa na matukio ya utekaji nyara, upoteaji watu, ukamatwaji ovyo ovyo unaofanywa na vyombo vya dola, na hata mauaji dhidi ya raia na pia dhidi ya askari wetu, ambao wana jukumu la kuwalinda raia hao.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, kesi kadhaa zimefunguliwa na serikali yake dhidi ya wananchi wa kawaida wanaotumia mitandao ya kijamii kuelezea maoni na mawazo yao kuhusiana na mambo mbalimbali yanayoendelea ndani ya nchi. Sambamba na hilo, magazeti kadhaa yamefungiwa na vyombo vya habari vimevamiwa na waandishi wa habari kushambuliwa, kupigwa na hata kuwekwa ndani, wakati wakiwa kwenye majukumu yao ya kukusanya na kusambaza habari.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameirejesha Tanzania kwenye mfumo wa chama kimoja kwa kuzuwia shughuli zozote za kisiasa ikiwemo mikutano ya hadhara na hata ya ndani, sikwambii maandamano na midahalo ya kitaifa hadi mwaka 2020, kwa kile anachodai ni kumpatia muda wa kutekeleza ilani ya chama chake aliyoinadi kwenye kampeni za uchaguzi wa 2015.

Mara kadhaa, polisi yake imewatia nguvuni viongozi wa upinzani wakiwa kwenye shughuli zao za kisiasa, ingawa haifanyi hivyo kwa viongozi wa CCM wakiwa kwenye shughuli kama hizo.

Tumeshuhudia kiwango kikubwa kabisa cha kukosewa hishima taratibu za kinchi kwenye teuzi, utenguwaji, utendaji na hivyo uwajibikaji wa watumishi wa sekta ya umma. Kila mmoja, kutoka raia wa chini kabisa hadi afisa wa juu serikalini, anaishi kwenye khofu ya kulengwa na kuandamwa si kwa sababu ya makosa anayoyatenda, lakini kwa sababu ya ‘hisia’ za mtawala mkuu wa nchi, ambazo nazo hutokana na taarifa zisizo sahihi anazofikishiwa na wale alioamua pekee kuwaamini na kuwakubali ‘ukweli’ wao.

Kila mtu na kila taasisi ambayo ni tishio kwa ‘ukweli wa hisia’ za mtawala, basi haiko salama. Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ambavyo viliisababisha kwa mara ya kwanza CCM kushindwa kupata asilimia 60 ya kura za urais ndani ya miaka 25 vinanyanyaswa kusudi na vyombo vya dola.

Chama cha Wananchi (CUF) ni mmoja wa wahanga wakubwa wa kipindi hiki kifupi cha utawala wa Rais Magufuli, kwa kuwa kinaonekana kukataa kuwa sehemu ya ‘ukweli wake wa hisia’ kwamba rais pekee ndiye anayemiliki maoni, mawazo, na njia sahihi kwa kila kinachojiri, likiwemo suala tete la ‘uhuni’ uliofanywa na CCM na vyombo vya dola dhidi ya maamuzi sahihi ya wananchi wa Zanzibar ya tarehe 25 Oktoba 2015.

Kwa ufupi, ndani ya utawala huu wa awamu ya tano, misingi ya kidemokrasia, kama ilivyotajwa hapo juu na Kofi Annan, inakanyagwa na utawala wa Rais Magufuli. Yote kwa jina la kumpa yeye nafasi ya kuleta maendeleo aliyoyaahidi kwa wananchi.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 24 Julai 2017.

 

UCHAMBUZI

Je, Tanzania yaweza kupata maendeleo ya kiuchumi kwa kubaka demokrasia?

Shutuma kwamba utawala wa awamu ya tano wa Rais John Magufuli unaibinya roho demokrasia changa ya taifa hili kubwa kabisa Afrika Mashariki zina mashiko yake kwa kuangalia rikodi ya yale yanayotendwa dhidi ya vyama vya upinzani na viongozi wao, asasi za kijamii na hata vyombo vya habari, viwe vipya ama vikongwe.

Lakini wale wanaokosoa kwamba utawala huu unafanya mambo bila ya kuwa na itikadi au falsafa maalum inayouongoza, nao pia wanakosea. Ukweli ni kuwa kinachofanywa sasa na Rais Magufuli na timu yake kina mashiko yake kwenye mojawapo ya matapo makongwe kabisa kwenye taaluma ya uchumi wa kidola.

Tapo hilo ni lile linaloamini kwamba, kwanza, maendeleo yana tafsiri ya ukuwaji wa uchumi kupitia miundombinu na ubanaji matumizi na, pili, maendeleo hayo yanawezekana pale tu ambapo pana mfumo wa kirasimu na utawala wa mkono wa chuma. Ushahidi wa wanaoamini hayo wanautoa kwenye mifano ya Rwanda na baadhi ya mataifa ya Amerika Kusini na Asia, ambayo ni kigezo cha namna udikteta unavyofanikiwa kuimarisha maendeleo ya kiuchumi.

Wasomi akina Walter Galenson, Karl De Schweinitz na Samuel Huntington wanahoji kwamba demokrasia inajikita zaidi kwenye mahitaji ya muda mfupi ambayo yanagharimu uwekezaji na ukuwaji wa uchumi. Kwa maoni yao, “demokrasia inatishia faida na, hivyo, kupunguza uwekezaji na basi haiendani na maendeleo ya kiuchumi.“ Watetezi hao wanahoji kwamba udikteta una uwezo mkubwa zaidi wa kulazimisha upatikanaji wa akiba na hatimaye kuanzisha ukuwaji mkubwa wa uchumi.

Akitetea mtazamo huo, Vaman Rao aliandika maneno haya mwaka 1984: “Maendeleo ya kiuchumi ni mchakato unaohitaji uwekezaji mkubwa wa rasilimali watu, vitu na fedha. Mipango ya uwekezaji kama huo inahusisha makato kwenye matumizi ambayo yanaweza kuwa machungu sana kwa watu wa chini ambao ndio wengi wao kwenye mataifa yanayoendelea. Serikali zinapaswa kuchukuwa hatua kali kabisa na kulazimisha zitekelezwe kimabavu ili kuweza kuzalisha ziada inayohitajika kwa uwekezaji. Endapo hatua hizo zitapigiwa kura na wananchi, hapana shaka zitashindwa. Hakuna chama chochote cha siasa kinachoweza kutegemea kushinda uchaguzi wa kidemokrasia kwa kutumia hoja ya kuwataka wananchi wajitowe muhanga leo ili wawe na maisha mazuri kesho.” (Tafsiri ni yangu).

Na Mohammed Ghassani

Hadi hapo, kwa wale wanaodhani kuwa chini ya Rais Magufuli, Tanzania inaendeshwa mzobemzobe huku mkuu akiwa hajuwi aendako, wanapaswa kuhakiki upya wanayoyaamini. Inawezekana muda wa kuwepo kwake madarakani usitoshe kumfikisha anakolunga, lakini haina maana kuwa hakujuwi – angalau kwa kuzingatia tapo hili la kitaaluma ya uchumi wa kidola.

Ubakaji demokrasia hauwezi kuwa dawa ya ukuwaji uchumi

Lakini je, kwa kuungwa kwake mkono na wasomi kama hao niliowataja, kunaufanya mtazamo wa kuyachagua maendeleo kwa gharama ya kuiua demokrasia kuwa sahihi? Jibu langu ni hapana. Mtazamo huu si sawa hata kidogo, kwa sababu sio tu kwa kuwa una fasili finyu sana ya maendeleo (kwa kusisitiza ukuwaji wa uchumi kupitia uwekezaji wa miundombinu pekee), bali pia unapingana na hata ushahidi wa wazi na tafiti kadhaa za kisayansi duniani, zikiwemo zile zilizofanywa kwenye mataifa yetu ya Dunia ya Tatu na yale yaliyojikwamua kiuchumi yaitwayo sasa Dunia ya Kwanza.

Wasomi Douglass C. North na Barry R. Weingast, kwa mfano, waliandika hivi mwaka 1989: “Dola ya kikandamizaji kila siku inakuwa tayari kuigeuza jamii kuwa windo lake kwa kisingizio cha kujenga uchumi. Ni taasisi za kidemokrasia pekee ndizo zinazoweza kuizuwia dola hiyo kwa maslahi ya umma. Udikteta wa aina yoyote ile ni chanzo kikuu cha ukosefu wa ufanisi, maana serikali ambayo jukumu lake la msingi ni kuweka mfumo wa kulinda uwekezaji, uzalishaji na usambazaji inajigeuza kuwa ndio mtendaji wa pekee wa kila kitu.”

Dunia ni shahidi wa kupinduka kwa maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kibinafsi kwenye mataifa yaliyoujaribu udikteta hata katika yale ambayo leo hii utawala wa Rais Magufuli unayachukulia kuwa ni kigezo cha kufuatwa. Kuanguka kwa uchumi wa Nicaragua chini ya dikteta Somoza, wa Jamhuri ya Dominik chini ya Trujillo, Ufilipino chini ya Marcos na Ulaya ya Mashariki chini ya tawala za kikomunisti si mambo ya kuigwa.

Athari za ubakaji wa demokrasia ndani ya ‘Tanzania ya Magufuli’

Ndani ya kipindi hiki kifupi cha utawala wa awamu ya tano unaoikanyaga misingi ya kidemokrasia, Tanzania imo kwenye wakati mgumu sana kimaendeleo. Hali ya maisha imezidi kuwa ngumu, imani ya wananchi kwa mfumo inapotea na imani ya wawekezaji wa kati na wa juu inatikisika, licha ya ripoti za kutunga zitolewazo na taasisi za kidola kuonesha kuwa mambo yako shwari.

Bei za bidhaa muhimu kwa matumizi ya kila siku kama vile unga, mchele, sukari na madawa ni ya juu sana, vituo vya afya havina madawa, mashuleni kuna msongomano na ukosefu wa vifaa.

Hoteli kadhaa zimeripoti anguko la asilimia hadi 60 la mauzo yao ndani ya kipindi hiki cha utawala wa Rais Magufuli, huku kukiwa na wimbi la wafanyabiashara wanaohamishia biashara zao nje ya nchi kwa sasa, si kwa kuwa ni wakwepaji kodi kama inavyotakiwa iaminike, bali kwa kuwa hawana hakika ya mitaji yao nchini kutokana na staili ya matamko ya kuripuka na kutaka sifa ya mkuu wa nchi.

Yote haya ni kwa kuwa utawala usiohishimu misingi ya kidemokrasia hukaribisha ghasia – ghasia kwenye nafsi za watu, ghasia kwenye maisha yao, ghasia kwenye mifumo ya kiuchumi na kisiasa. Hizi ni ghasia za kimyakimya lakini zina mahusiano ya moja kwa moja na ukosefu wa maendeleo. Tanzania ya Magufuli – kama mwenyewe anavyopenda kuiita – sasa inapitia kwenye kipindi hicho cha ghasia.

Dawa ni kuimarisha viwili kwa pamoja

Mwaka 1972, muongo mmoja baada ya uhuru wa Tanganyika, Mwalimu Julius Nyerere aliuvunja mfumo uliotoa mamlaka kwa serikali za mikoa kwa minajili ya kuimarisha madaraka na nguvu za serikali kuu iliyopo Dar es Salaam, lakini wakati akikaribia mwisho wa utawala wake, alinukuliwa akisema kwamba: “Kuna mambo ambayo nisingeliyafanya endapo ningeweza kuanza upya. Mojawapo ni kuvunja mamlaka ya serikali za mikoa.”

Hili linatuzinduwa kuwa daima kwenye utawala, jambo la busara ni kutoa uhuru zaidi wa kidemokrasia kwa wananchi na sio kuubana. Ushiriki wa wananchi kwenye uendeshaji wa mambo yao ni jambo la muhimu sana kama jamii hiyo inataka kweli kuyafikia maendeleo.

Ingawa miaka 25 ya siasa za vyama vingi haikuwa na ukamilifu, ikizongwa na matatizo mengi na wakati mwengine ya kuvunja moyo, lakini Tanzania ilikuwa inapiga hatua kidogo kidogo. Hatua hizo zilipaswa kuendelezwa na sio kurejeshwa nyuma kama ambavyo inaonekana wazi hivi sasa.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo ina serikali isiyohishimu mgawanyo wa madaraka, isiyohishimu uhuru wa kimsingi kama vile uhuru wa mawazo, uhuru wa kujieleza, na uhuru wa kujiunga na kujikusanya na pia utawala wa sharia, ni taifa lenye utawala uliopoteza uhalali wake wa kidemokrasia, hata kama awali uliingia madarakani kwa kushinda uchaguzi.

Kama kweli tunataka kuwa na maendeleo, tunapaswa kuziunganisha dhana hizi mbili pamoja, kwani kimsingi maendeleo na demokrasia duniani yameungana na uimarishaji wa thamani ya maisha ya binaadamu.

Serikali ya Rais Magufuli inapaswa kuifahamu na kuihishimu mifumo ya kikatiba, vyombo huru vya habari na vyenye kujumuisha wote, asasi imara za kijamii na dhamira ya kweli ya kuelekea utangamano na majadiliano ya kijamii.

Hii ndiyo misingi mikuu ya kufikia lengo la maisha bora. Demokrasia inaweza tu kudumu kama inaonesha, muda wote na mwahala mote, kwamba ni njia bora kabisa ya kufikia lengo hilo.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kabisa na gazeti la Mwelekeo la tarehe 18 Julai 2017.