UCHAMBUZI

Tanzania hailiwi na rushwa pekee, bali pia na ufisadi wa kisiasa

Majuzi Rais John Magufuli alimuapisha Brigedia Jenerali John Mbungo kuwa Naibu Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana  na Rushwa (TAKUKURU) akiweka msisitizo kwamba anataka kuona wala rushwa wanafungwa jela haraka iwezekanavyo.

Kwa maneno yake mwenyewe Rais Magufuli, “mambo makubwa ambayo taifa linapambana nayo yanatokana na rushwa…” na kwamba kama Tanzania ikifanikiwa kuipunguza rushwa angalau kwa asilimia 80, basi itakuwa imeyatatua matatizo yake mengi sana.

Hakuna anayepinga kwamba Tanzania, ambayo imeongozwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) – chama chake yeye Rais Magufuli – muda wote wa kuwa kwake taifa huru, imeoza kwa rushwa. Inanuka, imeoza, kila mahala, kila sekta!

Lakini katikati ya uoza huo, au pengine kwa sababu ya uoza huo, ndipo unapokuta hii tabia yetu mbovu ya kuuzungumzia uchafu kwa maneno yanayochuja kimaana. Mojawapo likiwa ni hili la kuuita ufisadi kuwa ni rushwa. Rushwa tu!

Ukweli ni kuwa rushwa ni kitu kidogo sana panapohusika uoza wenyewe hasa uliopo. Rushwa ni utowaji na au upokeaji wa kitu (mara nyingi huwa pesa) kwa ajili ya kutoa au kupokea huduma, ambayo kimsingi ingelikuwa haki kutolewa bila ya kitu hicho.

Na Mohammed Ghassani

Wengi wetu tunadhani rushwa ni sawa na ule msamiati wa Kiingereza ‘corruption’, ndiyo maana hata hiyo taasisi inayoshughulika na kadhia hiyo inaitwa TAKUKURU kwa kuwa tunasema inafanya kazi ya kupambana na kuzuia rushwa.

Na kwa kuwa tunakosea kwenye kuipa jina lake halisi hali hii tunayokabiliana nayo, ndio  maana tunazunguka mumo humo, tukiamini kwamba kubadilisha sura kwenye chombo chenye mamlaka ya kupambana na hali hii kunatosha kuimaliza.

Ukweli ni kwamba kuiangalia hali kwa jicho lake halisi kuna nafasi kubwa mno kwenye kuzifikia hizo asilimia 80 anazolenga Rais Magufuli kwenye vita hivi vikubwa na, kwa hakika, vyenye maana kwetu sote.

Tanzania inaliwa na ufisadi na sio rushwa pekee, na tena ufisadi mkubwa zaidi ni ule wa kisiasa, ambao umejengewa mihimili kwa miaka 50 ya utawala wa CCM, kiasi cha kuufanya uonekane hali ya kawaida kwenye maisha ya kila siku.

Ufisadi wa kisiasa unakwenda mbali zaidi ya pale rushwa ya kutoa na kupokea fedha inapoishia. Huu ni utumiaji mbaya wa madaraka unaofanywa na maafisa wa serikali na, au, wa taasisi za kisiasa kwa maslahi binafsi. Aina zake ni za viwango tafauti, na hiyo rushwa moja tu miongoni mwao.

Katika upana wake utakuta pia udugunaizesheni, wizi wa kura, milungula, wizi wa mali ya umma na ubadhirifu, kwa kutaja machache.

Ufisadi huu wa kisiasa, kwa hakika, ndio mama wa maovu mengine yote katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uovu wa madawa ya kulevya, ujambazi, ukahaba na umasikini wa watu wetu, kwa mfano, ni matokeo ya ufisadi wa kisiasa ambao umekuwa ukiila nchi yetu kwa zaidi ya miongo mitano sasa.

Bahati mbaya ni kuwa ufisadi huu una khulka moja ya hatari sana: kuzoeleka. Kila anayechukua nafasi ya uongozi wa umma katika serikali au taasisi ya kisiasa huona sawa kwake kuwa fisadi, na kwa hakika jamii humtarajia awe hivyo. Kwamba atumie fursa ile kujinufaisha binafsi, awatishe wengine, awakomowe, awaangamize ili yeye awe hapo alipo .

Ndio maana maafisa wa tume za uchaguzi huiba kura kwa ajili ya kuwanufaisha wanasiasa wanaowapa vyeo, wagombea hununua wapiga kura, polisi hula mkono kwa mkono na wahalifu, maprofesa hupasisha au kufelisha wanafunzi vyuoni kwa kuzingatia maslahi yao binafsi. Alimradi ni mchafukoge.

Jamii hii ya mchafukoge ni muakisiko wa ufisadi wa kisiasa uliopea na kuzoeleka. Utamaduni wa chukua chako mapema, wa iba ulindwe na kemea udhibitiwe (kama wanavyoonekana kudhibitiwa wapinzani sasa), ndio unaojenga fikra za Watanzania uwaonao mbele yako leo.

Si hasha, kwa hivyo, kusikia hata miongoni mwa kada za hao waitwao wasomi leo hii wakisema: “Naye Tundu Lissu kazidi kidomodomo.” Kwao wao ufisadi ni ada ya maisha ya kila siku.

Kilele cha utamaduni huu huwa ni kile kinachoitwa kleptocracy (rule by thieves), yaani utawala wa wizi – wizi wa kura, wizi wa mali, wizi wa matumaini, wizi wa kesho ya wanyonge walio wengi.

Ufisadi una hatari kubwa na ya pekee katika maendeleo ya taifa. Katika siasa, hufifisha na wakati mwengine kuua kabisa mfumo wa kidemokrasia na utawala wa sheria, maana ufisadi una kiburi cha kuingilia kati chochote ambacho kinaonekana kiko dhidi yake. Ukweli ni kwamba demokrasia na utawala wa sheria ni adui kwa ufisadi; na kilipo kimoja chengine hakikai.

Kwa hivyo, kwa jamii kama yetu, ambayo imejikita katika uoza wa kupindukia wa ufisadi, mafisadi wenyewe hawataki kabisa kuona mfumo wa demokrasia ukistawi ama utawala wa sheria ukisimama. Si ajabu, kwa hivyo, kuona wakiingilia kati taratibu za kawaida za kidemokrasia na za utawala wa sheria kila pale wanapoona zinachukuwa mkondo wake.

Ya kuharibiwa kila mara kwa chaguzi za Zanzibar, kwa mfano, kwa kupelekwa majeshi yenye silaha nzito nzito ni katika hizo jitihada za ufisadi kupingana na demokrasia na utawala wa sheria.

Ufisadi katika chaguzi hupelekea ofisi za umma kukaliwa na watu wasiotokana na ridhaa ya umma na hivyo nao matokeo yake huzikalia ofisi hizo kwa maslahi yao binafsi na sio kwa maslahi ya umma, maana sio uliowaweka ofisini.

Leo hii Rais Magufuli anapolilia ukosefu wa uzalendo miongoni mwa wenzake serikalini – wanaofikia hadi kusaini mikataba ya kuuza madini kiholela – anapaswa kujiuliza namna hao watiaji saini walivyofika hapo madarakani. Je, ni kwa demorasia au kwa ufisadi wa kisiasa?

Ufisadi katika vyombo vya kutunga sheria hupunguza au huondosha kabisa uwajibikaji na uwakilishi wa kweli katika vyombo hivyo; ufisadi kwenye mahakama huiweka rehani haki ya wananchi; na ufisadi kwenye utawala husababisha ukosefu wa uadilifu katika utowaji wa huduma za kijamii.

Kwa jumla, ufisadi hukokozoa kabisa uwezo wa kitaasisi wa serikali, kwani husababisha taratibu kupuuzwa, rasilimali kuporwa, na ofisi za umma kuuzwa na kununuliwa kama bidhaa nyengine yoyote.

Ufisadi wa kisiasa ukipevuka huufanya hata uhalali wa serikali iliyopo madarakani uhojike na vivyo misingi ya demokrasia na kuaminiana itoweke. Ni mapema, pengine, sasa kwa wananchi wa Tanzania kuhoji uhalali wa serikali yao, lakini kwa mwenendo huu tunaokwenda nao, si muda mrefu tena ujao, hilo la kuhoji litakuwa wajibu wetu wa mwanzo!

Lakini wakati tukisubiri wakati huo ufike, sote ni mashahidi wa namna ambavyo ufisadi wa kisiasa unadumaza maendeleo ya kiuchumi kwa kuchochea ubadhirifu na ukosefu wa ufanisi.

Watanzania wameshuhudia mali za nchi zikiibiwa mbele ya macho yao: mchanga wa dhahabu unasafirishwa makontena kwa makontena, meli za kigeni zinavua tani kwa tani za samaki kwenye bahari yao, na wenye vyeo wanajikopesha na kujikatia juu kwa juu kutoka hazina ya taifa.

Na hayo hayajasimama kwa kuwa Rais Magufuli kasema anataka kuwaona wala rushwa wakifungwa jela. Yatasimama kwa kuuita ufisadi kwa jina lake halisi na kuutendea kama ututendeavyo – kuuwa maana nao unatuuwa.

Haitoshi kila siku kulia majukwaani na kwenye vichwa vya habari magazetini. Kuuzungumzia ufisadi kwa jina la rushwa hakutoshi. Kueleza ushahidi wa rushwa hiyo ilivyolimaliza taifa pia hakutoshi.

Hakutoshi, maana baada ya kuwa mashahidi na walalamikaji miaka yote 50 ya taifa huru, kumetusaidia nini? Kwa karibuni miongo mitano yote, hiyo imekuwa hali ambayo taifa hili limeishi nayo.

Leo hii tunajikokota kwenye mstari wa mwisho wa umasikini duniani, watoto wetu wakifa kwa maradhi na njaa, na bado tumeendelea kuwa mashahidi na walalamikaji ambao tunalizunguka tatizo lenyewe, badala ya kutua katikati yake – penye ufisadi wa kisiasa.

Kwa hivyo, si mwanajeshi  John Mbungo anayepaswa kuvaa magwanda yake kupambana na ufisadi huu wa kisiasa, maana si ajabu kuwa hata yeye mwenyewe ni matokeo ya mfumo uliousimamisha ufisadi wa aina hiyo, na ndio maana hata amiri jeshi wake anataka tu akahakikishe anawafunga wala rushwa. Wala rushwa tu!

Ni wananchi wanaopaswa, kwanza, kuufahamu  ufisadi wa kisiasa ambao Tanzania imekulia nao. Kisha, pili, kuuchukia kwelikweli, na mwisho, la tatu, kuchukuwa hatua dhidi ya uoza huu kwa njia halali.

Miongo hiyo mitano ya ufisadi wa kisiasa imewashuhudia watawala wale wale wakiwazoesha kuupenda na kuushabikia ufisadi na kuufanya kuwa utamaduni wao. Wamewapotosha vya kutosha. Wamefanywa waone jambo la kawaida kutoa na kupokea rushwa. Wamewafanya wautarajie ufisadi na wautegemee kama njia ya kupita kufika waendako.

Wanapaswa sasa kukataa na kusema hapana. Hapana kwa ufisadi wa kisiasa. Hapana kwa mafisadi wa kisiasa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 28 Agosti 2017.

 

UCHAMBUZI

Serikali inapojibu mabomu ya Lissu kwa risasi za maji

Inaonekana mtazamo wa serikali ya Rais John Magufuli kumuelekea mwanasheria wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Tundu Lissu, unaanza kubadilika.

Kutoka kumkamatakamata kila akitoa kauli na kumweka ndani kisha kumfungulia mashitaka yasiyo kichwa wala miguu, sasa serikali imeamua kujibizana naye neno kwa neno, ‘bandika-bandua’ wasemavyo vijana wa mjini.

Sasa leo Lissu akisema jambo kuhusu serikali, ngojea kauli ya msemaji wa serikali hiyo kesho yake. Hii ni hatua nzuri sana, mara nyingi zaidi kuliko ule anaouita mwanamuziki Ibrahim Musa (Roma Mkatoliki) kama ‘uhuni wa kishamba.’

Uhuni wa kishamba ni pamoja na huu wa kukamatamata wanasiasa wa upinzani ovyo, kuwapiga, kuwatesa na kisha kuwafungulia mashitaka yasiyo mashiko alimradi tu kuwasumbua, kuwavunjia heshima na haki zao za kibinaadamu na kuwapotezea muda wao.

Kwa hivyo, ni jambo la kusifiwa kuwa serikali inaamua kuachana na tabia isiyo sahihi, angalau kwa kuanza na huyu mwanasheria anayetambuliwa kwa misimamo ya kimapinduzi, Lissu.

Na Mohammed Ghassani

Huenda tabia hii ikachukuliwa pia dhidi ya wengine wasiokuwa wanasheria, lakini ambao wanaamini kuikosoa serikali iliyopo madarakani kwa mijadala na midahalo ni njia bora zaidi kuliko kugeukia uasi wa silaha na matumizi ya nguvu.

Hata hivyo, inapoamua kutenda hivi, serikali bado inapaswa kujipanga. Isiwe inakurupuka kama kule kwenye huo uitwao ‘uhuni wa kishamba.’ Vyenginevyo, itakuwa inapata matokeo yale yale – ya kubwagwa kwa aibu na fadhaa.

Kwa aliyefuatilia mara mbili tatu ambazo ofisi ya msemaji maalum wa serikali imeamua kumjibu Lissu, atagundua kirahisi namna ofisi hiyo inavyotumia staili ile ile ya kukurupuka hadi sasa, na matokeo yake kuja na majibu mepesi kwa maswali mazito ambayo mnadhimu huyo wa kambi ya upinzani bungeni anayaibua.

Mfano wa karibuni kabisa ni huu wa majuzi, ambapo Lissu aliibua suala la kuzuiliwa kwa ndege aina ya Bombardier Q400-Dash 8 iliyonunuliwa na serikali ya Rais Magufuli nchini Canada kutokana na deni la dola milioni 37.8 (shilingi bilioni 87) ambalo serikali ya Tanzania inadaiwa kwa kuvunja kwake mkataba na kampuni moja ya ujenzi, Stirling Civil Engineering Ltd.

Kwa mujibu wa Lissu, kampuni hiyo ina hati ya mahakama inayoipa haki ya kuzuia mali za Tanzania sio tu nchini Canada, bali pia Uholanzi, Ufaransa, Ubelgiji, Uingereza na hata nchi jirani ya Uganda.

Kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, Lissu aligusia pia taarifa ya kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia Mining kuifungulia serikali ya Tanzania kesi kwenye mahakama ya usuluhishi ikidai pia mamilioni ya dola kwa kuzuiwa mchanga wake wa dhahabu, maarufu kama makinikia. Acacia wamefungua kesi hiyo hata kama bado mazungumzo baina ya pande hizo mbili yanaendelea.

Hicho ndicho cha msingi alichokibainisha Lissu kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, ingawa kiliambatana na makandokando mengine kama vile kusema kuwa ukweli huo ulifichwa na serikali kwa kuwa ni matokeo ya tabia ya serikali hiyo kufanya mambo kwa kuripuaripua bila kufuata taratibu.

Sasa sikiliza majibu ya kaimu msemaji rasmi wa serikali, Zamaradi Kawawa, kwenye hili. Kwanza, kwamba ni kweli Bombardier-4000 imezuiliwa, lakini jitihada zinaendelea kuikwamua na kuifikisha Tanzania muda mfupi ujao.

Pili, kwamba kuzuiwa kwa ndege hiyo kunatokana na kampeni inayoendeshwa na wanasiasa wetu wasioitakia mema Tanzania.

Tatu, kwamba serikali ya Rais Magufuli haibaguwi kwenye maendeleo.

Nne, kwamba serikali hiyo inawafuatilia kwa karibu wanasiasa wanaokwamisha maendeleo kwani pia ni hatari kwa usalama wa taifa.

Wengi walioyasikia majibu haya walivunjwa moyo tangu sentensi ya kwanza kabisa kuanza kusomwa na kaimu msemaji huyo wa serikali. Sababu ni kuwa Lissu kwenye uwasilishaji wa ‘bomu’ lake alikuja na ushahidi mzito na wa moja kwa moja dhidi ya serikali.

Kwamba serikali ilikuwa imevunja mkataba wa ujenzi barabara mwaka 2009 na kampuni hiyo. Kwamba ikashitakiwa. Kwamba ikashindwa kesi. Kwamba ikakataa kulipa fidia. Kwamba ikakata rufaa. Kwamba ikashindwa rufaa. Ikaamuriwa kulipa tena. Ikakataa. Sasa ndege yake imekamatwa. Kwamba ni baada ya ndege kukamatwa kwa deni, ndipo Waziri wa Mambo ya Nje, Balozi Augustine Mahiga, akaenda nchini Canada kusaka njia ya kulimaliza hilo kimya kimya.

Yote haya hayajibiki kwa kusema kuwa ndege italipiwa na itafika nyumbani na Watanzania waendelee kuiamini serikali yao. Waiamini kwa msingi upi kwenye hili, wakati haikuwahi hata siku moja kusema kuwa ndege iliyotakiwa kufika mwezi mmoja nyuma haikufika kwa sababu gani? Na hata alipokuja mtu kutamka hadharani, sababu za kuchelewa kwake kufika, serikali inamrukia mtu huyo kuwa anakwamisha maendeleo?

Mambo matatu yanazuka sasa hapa, sio kwenye suala lenyewe la Bombardier tu, bali kwenye tabia yenyewe ya serikali kuyaendea maswala muhimu ya nchi. Kwanza, serikali hii inayojipambanua kwa kupambana kwake na ufisadi, wizi na ubadhirifu katika sekta ya umma, imeuficha udhaifu wake nyuma ya ukali wa kiongozi mkuu, Rais Magufuli.

Kwamba pale guo la ukali huo wa Rais Magufuli linapovuliwa, basi kinachodhihirika ni serikali isiyo viunganishi na muunganiko. Waliofuatilia suala hili hili, wanajuwa kuwa huko kwenye mitandao ya kijamii, Waziri wa Mawasiliano na Ujenzi Makame Mbarawa alishakanusha siku moja tu nyuma juu ya kushikiliwa kwa Bombardier. Huyu ni mjumbe wa baraza la mawaziri. Lakini siku moja baadaye, msemaji wa serikali anakiri kuwa ni kweli inashikiliwa. Hii inaonesha kuwa huko ndani, nje ya ukali wa Rais Magufuli, kuna vikuku vya mkufu wa mawasiliano ndani ya utawala vimekatika. Na huo ni udhaifu mkubwa.

Pili, miaka miwili baada ya kuingia madarakani, Rais Magufuli ameshindwa kupanga timu yake ya mkakati vyema. Bado utendaji wake na wa timu yake unakwendana na mapigo ya kinachoendelea mitandaoni na kwenye majukwaa ya kisiasa.

Mawasiliano baina ya serikali na umma yanajengwa na kipi kimeibuliwa na ‘waropokaji’ huku nje – mitandaoni, majukwaani, mitaani. Ujanja wa kuziwahi taarifa mapema ili kuchomeka wazo ambalo serikali inataka liwe wazo kuu kwa wananchi haumo ndani ya vichwa vya timu ya mkakati ya Rais Magufuli.

Tatu, na la mwisho, serikali inadanganya kwa jina la uzalendo. Kuanzia Rais Magufuli mwenyewe hadi wanaomfuata chini yake, kauli yao kubwa ya kukumbizia takataka chini ya zulia ni kwamba taifa letu linahitaji uzalendo wa hali ya juu, ambao kwa maoni yao ulikuwa umekosekana siku nyingi huko nyuma.

Wakati hilo ni sahihi kabisa, kisichokubalika ni kwa serikali hiyo hiyo kuficha ukweli au kudanganya kwa wananchi ili kujenga mapenzi yasiyo ya kweli kwa serikali yao.

Ingelikuwa vyema kabisa kile kinachohubiriwa na Rais Magufuli majukwaani, kwamba yeye ni msema kweli, kikawa ndicho kinachoakisika katika mtiririko mzima wa wanaomfuata chini yake. Na inapobainika kwamba kimakosa serikali ilidanganya au ilificha ukweli uliopaswa kufahamika na umma kwa wakati muafaka, basi iwe tayari kuomba radhi haraka na kwa ufanisi.

Mapenzi na uzalendo hujengwa juu ya ukweli na uwazi.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza kwenye gazeti la Mwelekeo la tarehe 22 Agosti 2017.

UCHAMBUZI

Magufuli anawauzia Watanzania tamaa ya maendeleo kwa gharama ya demokrasia yao

Kwa hakika, Rais John Magufuli anaonekana kuwalazimisha raia wake kufanya naye biashara ya gizani. Yeye awauzie maendeleo, nao wamlipe kwa gharama ya demokrasia angalau hadi mwaka 2020 wakati wa kampeni za uchaguzi mwengine.

Lakini je, biashara hii inawezekana kwa taifa ambalo lilishaonja ladha ya demokrasia kwa robo karne nzima mtawaliya? Je, ili kupata maendeleo ni lazima kuitia rehani misingi ya kikatiba, mgawanyo wa madaraka, haki za binaadamu na uhuru wa mtu binafsi?

Akizungumzia dhana ya demokrasia, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, anasema: “Demokrasia haihusiani pekee na ile siku moja kila baada ya miaka minne au mitano pale panapoitishwa chaguzi, bali inahusiana na mfumo wa serikali unaohishimu mgawanyo wa madaraka, uhuru wa mawazo, wa kidini, wa kujieleza, wa kujiunga na kujikusanya na pia utawala wa sharia. Utawala wowote unaokanyaga misingi hii, hupoteza uhalali wake wa kidemokrasia, hata kama awali uliingia madarakani kwa kushinda uchaguzi.” (Tafsiri ni yangu).

Dk. Chris Sausman, Mkurugenzi wa Chime Communications Group, anayatafsiri maendeleo kwa umbo la pembe tatu. “Kwanza ni mchakato ambao ndani yake muna mkururo wa hatua zinazopelekea – au zinazotegemewa kupelekea – matokeo ya aina fulani makhsusi, pili ni mkakati ndani ya mipango na sera na, tatu, ni matokeo ya mikondo miwili ya kwanza kupitia kiwango cha mtu binafsi – pale anapokuwa na kuutumia uhuru wake, kiwango cha jamii – pale inapoweza kutoka hatua moja ya kimaisha kwenda nyengine na kiwango cha kiuchumi – pale uchumi wa jumla unapoimarika.” (Tafsiri ni yangu).

Na Mohammed Ghassani

Namna dhana hizi mbili za demokrasia na maendeleo zinavyoungana zinatuambia kuwa biashara anayoifanya Rais Magufuli na Watanzania haitakuwa na mwisho mwema, hata kama sasa kunatolewa takwimu za mapambio.

Kama anavyosema Mkuu wa Madhehebu ya Shia Ismaili duniani, Aga Khan, “kimsingi maendeleo na demokrasia vimeungana na kuimarika kwa thamani ya maisha ya binaadamu. Uwezo wa kuifahamu (na kuihishimu) mifumo ya kikatiba, uwepo wa vyombo vya habari huru na vyenye kujumuisha wote, asasi imara za kijamii na dhamira ya kweli katika kuelekea utangamano na majadiliano ya kijamii. Hii ndiyo misingi mikuu ya kufikia lengo la maisha bora. Demokrasia inaweza tu kudumu kama inaonesha, muda wote na mwahala mote, kwamba ni njia bora kabisa ya kufikia lengo hilo.” (Tafsiri ni yangu).

Tanzania inapitia kwenye moja ya vipindi vigumu sana vya historia yake ya hivi karibuni. Baada ya kujaribu kuujenga mfumo wa kidemokrasia kwa miongo miwili na nusu, sasa jitihada hizo zinarudi nyuma kwa kasi ya ajabu.

Misingi mikuu ya demokrasia inashambuliwa kila uchao na serikali ya Rais Magufuli, akiamini kuwa ana uhalali wa kufanya lolote atakalo kwa kuwa tu madaraka ya juu yamo mikononi mwake.

Hata miaka miwili haijatimia vyema tangu ale kiapo cha utiifu kwa Katiba, Rais Magufuli ameshathibitisha kuwa yeye si muumini wa misingi mikuu ya Katiba yenyewe, kama vile mgawanyo wa madaraka na hishima kwa uhuru na haki za binaadamu.

Kwa mfano, mara kadhaa muhimili wa utawala kupitia kwake na wateule wake, umekuwa ukiingilia muhimili wa bunge kuwafunga midomo wabunge, kuzima mijadala yenye maslahi kwa taifa na hata kuzuwia matangazo ya bunge hilo kuoneshwa moja kwa moja kwenye televisheni ya taifa, ambayo inaendeshwa kwa kodi ya wananchi.

Wakati akizuwia matangazo hayo kwa kisingizio cha gharama na kubana matumizi ya serikali na pia kuwapa muda wananchi kufanya kazi, shughuli za kisiasa zake na za chama chake, CCM, hupewa nafasi ya kurushwa moja kwa moja na vyombo vya habari vya umma, vinavyolipiwa kwa fedha ya umma na katika wakati wa kazi.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, wabunge kadhaa wameshakamatwa, kupigwa, kuwekwa vizuizini na hata kufungwa jela, na katika baadhi ya mifano wakiwa ama bungeni au majimboni mwao katika shughuli zinazohusiana na nyadhifa na madaraka yao kama wabunge na au viongozi wa vyama vyao.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameshatoa kauli kadhaa zinazoingilia moja kwa moja uhuru wa mahakama na vyombo vyengine vinavyohusiana moja kwa moja na upatikanaji haki kama vile ofisi ya mwendesha mashitaka, polisi na idara za upelelezi, kwa kuwatia hatiani hadharani wale wote anaowashuku.

Matokeo yake, kwa kuwa tuna aina ya Katiba inayompa mkuu wa nchi nafasi ya uungu mtu, walio chini yake kwenye vyombo hivyo wanajipendekeza kuigeuza kila “kauli ya rais” kuwa ukweli, hata kama kwa kufanya hivyo wanazikanyaga sheria, kanuni na taratibu tulizojiwekea wenyewe kama taifa.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Tanzania imejikuta ikirejea kwenye zama za giza – ikitajwa kuwa na matukio ya utekaji nyara, upoteaji watu, ukamatwaji ovyo ovyo unaofanywa na vyombo vya dola, na hata mauaji dhidi ya raia na pia dhidi ya askari wetu, ambao wana jukumu la kuwalinda raia hao.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, kesi kadhaa zimefunguliwa na serikali yake dhidi ya wananchi wa kawaida wanaotumia mitandao ya kijamii kuelezea maoni na mawazo yao kuhusiana na mambo mbalimbali yanayoendelea ndani ya nchi. Sambamba na hilo, magazeti kadhaa yamefungiwa na vyombo vya habari vimevamiwa na waandishi wa habari kushambuliwa, kupigwa na hata kuwekwa ndani, wakati wakiwa kwenye majukumu yao ya kukusanya na kusambaza habari.

Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameirejesha Tanzania kwenye mfumo wa chama kimoja kwa kuzuwia shughuli zozote za kisiasa ikiwemo mikutano ya hadhara na hata ya ndani, sikwambii maandamano na midahalo ya kitaifa hadi mwaka 2020, kwa kile anachodai ni kumpatia muda wa kutekeleza ilani ya chama chake aliyoinadi kwenye kampeni za uchaguzi wa 2015.

Mara kadhaa, polisi yake imewatia nguvuni viongozi wa upinzani wakiwa kwenye shughuli zao za kisiasa, ingawa haifanyi hivyo kwa viongozi wa CCM wakiwa kwenye shughuli kama hizo.

Tumeshuhudia kiwango kikubwa kabisa cha kukosewa hishima taratibu za kinchi kwenye teuzi, utenguwaji, utendaji na hivyo uwajibikaji wa watumishi wa sekta ya umma. Kila mmoja, kutoka raia wa chini kabisa hadi afisa wa juu serikalini, anaishi kwenye khofu ya kulengwa na kuandamwa si kwa sababu ya makosa anayoyatenda, lakini kwa sababu ya ‘hisia’ za mtawala mkuu wa nchi, ambazo nazo hutokana na taarifa zisizo sahihi anazofikishiwa na wale alioamua pekee kuwaamini na kuwakubali ‘ukweli’ wao.

Kila mtu na kila taasisi ambayo ni tishio kwa ‘ukweli wa hisia’ za mtawala, basi haiko salama. Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ambavyo viliisababisha kwa mara ya kwanza CCM kushindwa kupata asilimia 60 ya kura za urais ndani ya miaka 25 vinanyanyaswa kusudi na vyombo vya dola.

Chama cha Wananchi (CUF) ni mmoja wa wahanga wakubwa wa kipindi hiki kifupi cha utawala wa Rais Magufuli, kwa kuwa kinaonekana kukataa kuwa sehemu ya ‘ukweli wake wa hisia’ kwamba rais pekee ndiye anayemiliki maoni, mawazo, na njia sahihi kwa kila kinachojiri, likiwemo suala tete la ‘uhuni’ uliofanywa na CCM na vyombo vya dola dhidi ya maamuzi sahihi ya wananchi wa Zanzibar ya tarehe 25 Oktoba 2015.

Kwa ufupi, ndani ya utawala huu wa awamu ya tano, misingi ya kidemokrasia, kama ilivyotajwa hapo juu na Kofi Annan, inakanyagwa na utawala wa Rais Magufuli. Yote kwa jina la kumpa yeye nafasi ya kuleta maendeleo aliyoyaahidi kwa wananchi.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 24 Julai 2017.