Ali Juma Suleiman alivamiwa na kikosi kikubwa cha watu usiku wa tarehe 26 Septemba mwaka huu nyumbani kwake Mtoni, Unguja. Mke wake, Bi Rehema Nassor Juma, anasema alishuhudia askari wenye sare za vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) wakiwa na mitutu ya bunduki, marungu na mapanga. Continue reading “Mayatima na wajane wa kisiasa hadi lini Zanzibar?”
Tag: haki za binaadamu
Maisha yasiyotathminiwa hayana maana kuyaishi
Ulimwenguni kote na katika zama zote, jamii inapokuwa chini ya utawala ulioziba masikio na macho na nyoyo, watawala hupenda waachiwe wafanye watakavyo. Huwa wamejirithisha wenyewe nchi na raia wake. Na kwa hili hawataki muhali, masahihisho, wala mabadiliko. Anapotokea mtu kuwasahihisha, badala ya kumchukulia kuwa msaidizi, wao humchukulia adui wao nambari moja, na hivyo hujihalalishia kumuadhibu kwa namna yoyote waionayo inafaa. Continue reading “Maisha yasiyotathminiwa hayana maana kuyaishi”
Magufuli anawauzia Watanzania tamaa ya maendeleo kwa gharama ya demokrasia yao
Kwa hakika, Rais John Magufuli anaonekana kuwalazimisha raia wake kufanya naye biashara ya gizani. Yeye awauzie maendeleo, nao wamlipe kwa gharama ya demokrasia angalau hadi mwaka 2020 wakati wa kampeni za uchaguzi mwengine.
Lakini je, biashara hii inawezekana kwa taifa ambalo lilishaonja ladha ya demokrasia kwa robo karne nzima mtawaliya? Je, ili kupata maendeleo ni lazima kuitia rehani misingi ya kikatiba, mgawanyo wa madaraka, haki za binaadamu na uhuru wa mtu binafsi?
Akizungumzia dhana ya demokrasia, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, anasema: “Demokrasia haihusiani pekee na ile siku moja kila baada ya miaka minne au mitano pale panapoitishwa chaguzi, bali inahusiana na mfumo wa serikali unaohishimu mgawanyo wa madaraka, uhuru wa mawazo, wa kidini, wa kujieleza, wa kujiunga na kujikusanya na pia utawala wa sharia. Utawala wowote unaokanyaga misingi hii, hupoteza uhalali wake wa kidemokrasia, hata kama awali uliingia madarakani kwa kushinda uchaguzi.” (Tafsiri ni yangu).
Dk. Chris Sausman, Mkurugenzi wa Chime Communications Group, anayatafsiri maendeleo kwa umbo la pembe tatu. “Kwanza ni mchakato ambao ndani yake muna mkururo wa hatua zinazopelekea – au zinazotegemewa kupelekea – matokeo ya aina fulani makhsusi, pili ni mkakati ndani ya mipango na sera na, tatu, ni matokeo ya mikondo miwili ya kwanza kupitia kiwango cha mtu binafsi – pale anapokuwa na kuutumia uhuru wake, kiwango cha jamii – pale inapoweza kutoka hatua moja ya kimaisha kwenda nyengine na kiwango cha kiuchumi – pale uchumi wa jumla unapoimarika.” (Tafsiri ni yangu).

Namna dhana hizi mbili za demokrasia na maendeleo zinavyoungana zinatuambia kuwa biashara anayoifanya Rais Magufuli na Watanzania haitakuwa na mwisho mwema, hata kama sasa kunatolewa takwimu za mapambio.
Kama anavyosema Mkuu wa Madhehebu ya Shia Ismaili duniani, Aga Khan, “kimsingi maendeleo na demokrasia vimeungana na kuimarika kwa thamani ya maisha ya binaadamu. Uwezo wa kuifahamu (na kuihishimu) mifumo ya kikatiba, uwepo wa vyombo vya habari huru na vyenye kujumuisha wote, asasi imara za kijamii na dhamira ya kweli katika kuelekea utangamano na majadiliano ya kijamii. Hii ndiyo misingi mikuu ya kufikia lengo la maisha bora. Demokrasia inaweza tu kudumu kama inaonesha, muda wote na mwahala mote, kwamba ni njia bora kabisa ya kufikia lengo hilo.” (Tafsiri ni yangu).
Tanzania inapitia kwenye moja ya vipindi vigumu sana vya historia yake ya hivi karibuni. Baada ya kujaribu kuujenga mfumo wa kidemokrasia kwa miongo miwili na nusu, sasa jitihada hizo zinarudi nyuma kwa kasi ya ajabu.
Misingi mikuu ya demokrasia inashambuliwa kila uchao na serikali ya Rais Magufuli, akiamini kuwa ana uhalali wa kufanya lolote atakalo kwa kuwa tu madaraka ya juu yamo mikononi mwake.
Hata miaka miwili haijatimia vyema tangu ale kiapo cha utiifu kwa Katiba, Rais Magufuli ameshathibitisha kuwa yeye si muumini wa misingi mikuu ya Katiba yenyewe, kama vile mgawanyo wa madaraka na hishima kwa uhuru na haki za binaadamu.
Kwa mfano, mara kadhaa muhimili wa utawala kupitia kwake na wateule wake, umekuwa ukiingilia muhimili wa bunge kuwafunga midomo wabunge, kuzima mijadala yenye maslahi kwa taifa na hata kuzuwia matangazo ya bunge hilo kuoneshwa moja kwa moja kwenye televisheni ya taifa, ambayo inaendeshwa kwa kodi ya wananchi.
Wakati akizuwia matangazo hayo kwa kisingizio cha gharama na kubana matumizi ya serikali na pia kuwapa muda wananchi kufanya kazi, shughuli za kisiasa zake na za chama chake, CCM, hupewa nafasi ya kurushwa moja kwa moja na vyombo vya habari vya umma, vinavyolipiwa kwa fedha ya umma na katika wakati wa kazi.
Ndani ya kipindi hiki kifupi, wabunge kadhaa wameshakamatwa, kupigwa, kuwekwa vizuizini na hata kufungwa jela, na katika baadhi ya mifano wakiwa ama bungeni au majimboni mwao katika shughuli zinazohusiana na nyadhifa na madaraka yao kama wabunge na au viongozi wa vyama vyao.
Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameshatoa kauli kadhaa zinazoingilia moja kwa moja uhuru wa mahakama na vyombo vyengine vinavyohusiana moja kwa moja na upatikanaji haki kama vile ofisi ya mwendesha mashitaka, polisi na idara za upelelezi, kwa kuwatia hatiani hadharani wale wote anaowashuku.
Matokeo yake, kwa kuwa tuna aina ya Katiba inayompa mkuu wa nchi nafasi ya uungu mtu, walio chini yake kwenye vyombo hivyo wanajipendekeza kuigeuza kila “kauli ya rais” kuwa ukweli, hata kama kwa kufanya hivyo wanazikanyaga sheria, kanuni na taratibu tulizojiwekea wenyewe kama taifa.
Ndani ya kipindi hiki kifupi, Tanzania imejikuta ikirejea kwenye zama za giza – ikitajwa kuwa na matukio ya utekaji nyara, upoteaji watu, ukamatwaji ovyo ovyo unaofanywa na vyombo vya dola, na hata mauaji dhidi ya raia na pia dhidi ya askari wetu, ambao wana jukumu la kuwalinda raia hao.
Ndani ya kipindi hiki kifupi, kesi kadhaa zimefunguliwa na serikali yake dhidi ya wananchi wa kawaida wanaotumia mitandao ya kijamii kuelezea maoni na mawazo yao kuhusiana na mambo mbalimbali yanayoendelea ndani ya nchi. Sambamba na hilo, magazeti kadhaa yamefungiwa na vyombo vya habari vimevamiwa na waandishi wa habari kushambuliwa, kupigwa na hata kuwekwa ndani, wakati wakiwa kwenye majukumu yao ya kukusanya na kusambaza habari.
Ndani ya kipindi hiki kifupi, Rais Magufuli ameirejesha Tanzania kwenye mfumo wa chama kimoja kwa kuzuwia shughuli zozote za kisiasa ikiwemo mikutano ya hadhara na hata ya ndani, sikwambii maandamano na midahalo ya kitaifa hadi mwaka 2020, kwa kile anachodai ni kumpatia muda wa kutekeleza ilani ya chama chake aliyoinadi kwenye kampeni za uchaguzi wa 2015.
Mara kadhaa, polisi yake imewatia nguvuni viongozi wa upinzani wakiwa kwenye shughuli zao za kisiasa, ingawa haifanyi hivyo kwa viongozi wa CCM wakiwa kwenye shughuli kama hizo.
Tumeshuhudia kiwango kikubwa kabisa cha kukosewa hishima taratibu za kinchi kwenye teuzi, utenguwaji, utendaji na hivyo uwajibikaji wa watumishi wa sekta ya umma. Kila mmoja, kutoka raia wa chini kabisa hadi afisa wa juu serikalini, anaishi kwenye khofu ya kulengwa na kuandamwa si kwa sababu ya makosa anayoyatenda, lakini kwa sababu ya ‘hisia’ za mtawala mkuu wa nchi, ambazo nazo hutokana na taarifa zisizo sahihi anazofikishiwa na wale alioamua pekee kuwaamini na kuwakubali ‘ukweli’ wao.
Kila mtu na kila taasisi ambayo ni tishio kwa ‘ukweli wa hisia’ za mtawala, basi haiko salama. Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ambavyo viliisababisha kwa mara ya kwanza CCM kushindwa kupata asilimia 60 ya kura za urais ndani ya miaka 25 vinanyanyaswa kusudi na vyombo vya dola.
Chama cha Wananchi (CUF) ni mmoja wa wahanga wakubwa wa kipindi hiki kifupi cha utawala wa Rais Magufuli, kwa kuwa kinaonekana kukataa kuwa sehemu ya ‘ukweli wake wa hisia’ kwamba rais pekee ndiye anayemiliki maoni, mawazo, na njia sahihi kwa kila kinachojiri, likiwemo suala tete la ‘uhuni’ uliofanywa na CCM na vyombo vya dola dhidi ya maamuzi sahihi ya wananchi wa Zanzibar ya tarehe 25 Oktoba 2015.
Kwa ufupi, ndani ya utawala huu wa awamu ya tano, misingi ya kidemokrasia, kama ilivyotajwa hapo juu na Kofi Annan, inakanyagwa na utawala wa Rais Magufuli. Yote kwa jina la kumpa yeye nafasi ya kuleta maendeleo aliyoyaahidi kwa wananchi.
TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 24 Julai 2017.
Ndiyo kwa ‘uchumagu’, hapana kwa ‘umagukrasia’
Kitu kimojawapo ambacho Rais John Magufuli anajipambanuwa nacho kwa haraka na watangulizi wake, ni tabia yake ya kutokuwa na ajizi na vile kutozingatia kwake mipaka kwenye huko kutokuwa na ajizi. Hayo ni kwa kila alisemalo na kila alitendalo. Kutokuwa na ajizi ni jambo jema kwa kiongozi, lakini kutokuzingatia mipaka si jambo la kusifiwa hata kidogo.
Hapa ndipo ambapo, kwa mwenye akili, anapoweza kirahisi kuchora mstari wa namna ya kumchambua, kumtafakari na kuchaguwa lipi ni lipi kwenye shakhsia ya Rais Magufuli, na kwayo isimuwiye vigumu kujuwa pa kuungana naye na pa kupingana naye.
Kinyume na wanavyochukulia wale wanaojiaminisha kuwa uzalendo hasa ni kumuunga mkono kiongozi wa nchi kwa lolote aliwazalo, alinenalo na alitendalo, utendaji kazi wa Rais Magufuli unawasuta sio tu kwa kutokujuwa kwao maana halisi ya uzalendo, bali pia kwa kuwaonesha kuwa hawana msaada wowote wa maana si kwa Rais Magufuli mwenyewe, wala kwa serikali yake na hata kwa chama chake kinachotawala, CCM.
Ufanyaji wake maamuzi, utoaji wa kauli zake na utendaji kazi wake unatufanya wengine kuona kuwa hata kama hatuna ulazima wa kumuunga mkono kwa kila jambo lake, bado pia hatuna ulazima wa kumpinga kwa kila kitu. Kwamba muna mwahala, kwa mtazamo wetu, anafanya vyema na anahitaji kupewa heko na kusaidiwa na muna mwengine ambamo anafanya vibaya na anapaswa kukosolewa na kuzuiwa.
Uchumagu na Tanzania inayotakiwa

Binafsi, namuunga mkono Rais Magufuli kwenye hili ninaloliita hapa ‘uchumagu’ – uchumi wa Magufuli, dhana inayowakilisha jitihada zake binafsi kama kiongozi wa nchi kuhakikisha kuwa uchumi wa nchi unakuwa na kuwagusa wananchi wa kawaida, ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakitengwa kando.
Ndani ya jitihada hizi, muna kampeni kubwa ya kupambana na ufisadi, wizi wa mali ya umma, ukosefu wa uwajibikaji na kiwango kikubwa cha uholela kwenye sekta ya umma. Muna pia jitihada zinazoonekana za kuimarisha miundo mbinu na kuwafikia watu kule waliko. Hapana shaka, mafanikio ya kampeni hii ni faida kwa umma na yana athari za moja kwa moja kwa mwananchi wa kawaida.
Hakuna mwenye mapenzi ya kweli kwa nchi, ambaye hataweza kuunga mkono pale, mathalani, watuhumiwa wa ufisadi wanapofikishwa mahakamani kujibu mashitaka dhidi yao. Hakuna pia atakayepinga pale siku maafisa wa serikali waliokuwa wamepewa dhamana kubwa kuwahudumia wananchi na wakazifanyia khiyana dhamana hizo ‘wanayotumbuliwa’.
Ingawa hata watu wanaweza kukosoa njia zinazotumika kwa kuhofia zisije zikawa za zimamoto na kulifanya lengo halisi kutofikiwa, lakini wanajuwa kuwa vita dhidi ya ufisadi ni jambo linalohitajika.
Baada ya zaidi ya nusu karne ya kutawaliwa na chama cha Rais Magufuli, CCM, serikali za pande zote mbili za Muungano zilishageuka kuwa jalala la uchafu wote wa kiuongozi: kuanzia wizi wa mali ya umma, udugunaizesheni (upendeleo wa kifamilia na kieneo), ubadhirifu, uzembe na ukosefu wa uwajibikaji.
Kwa ujumla, ufisadi umekuwa ni wa kimfumo ndani ya serikali hizi, kuanzia juu kabisa hadi chini kabisa kwa kipindi kirefu sasa. Hata hizo enzi za Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid Karume, ambazo wengine hutaka kutuaminisha kuwa zilikuwa zama za usafi wa kimaadili, ushahidi unaonesha kuwa zilikuwa na makandokando yake mengi na ndiyo hayo yaliyoasisi uovu uliokuja kudhihirika baadaye.
Mwenyewe Mwalimu Nyerere alikuwa akikiri kuwa hata katika uongozi wake kulikuwa na rushwa, lakini alitaka tukubali kuwa yeye na wenzake wachache waliokuwa juu walikuwa hasa wakiichukia rushwa kwa vitendo, na kwamba kila walipopata mashaka na mteule yeyote aliye chini yao kuhusika na rushwa, basi walimchukulia hatua hapo hapo bila kuchelewa na bila kuchelea.
Kwa hivyo, kwamba leo Rais Magufuli anaongoza vita vya kuukomboa uchumi kutoka mikononi mwa ufisadi wa ndani na wa kimataifa na dhidi ya uporaji wa rasilimali unaofanyika kupitia mikataba ambayo serikali zilizoongozwa na chama chake ziliingia huko nyuma, ni wazi kuwa anapigana vita ambavyo anastahiki sifa na kuungwa mkono, hata kama ni vita vinavyotokana na uchafu uliotendwa na chama chake mwenyewe huko tutokako.
Kwa kutumia maneno yake ya tarehe 1 Julai 2017, wakati akifungua Maonesho ya Sabasaba: “Tanzania tumechezewa sana kwa sababu tulitaka kuchezewa. Lakini sasa kuchezewa basi!” Nami nafanya hivyo: namsifu na namuunga mkono. Tanzania kama taifa lilichezewa sana kwenye uchumi wake kwa kuwa wao kama watawala walitaka taifa hili lichezewe. Kufanikiwa kwa Rais Magufuli kwenye vita hivi, ni kufanikiwa kwa taifa zima.
Tanzania haiuhitaji umagukrasia
Lakini kando ya vita vyake hivi, Rais Magufuli anapigana pia vita vyengine, ambavyo mpigaji hasa ni peke yake kwa kuwa ana nyenzo za kumuwezesha kupiga pasi yeye kushambuliwa, na anaowapiga vita hivyo ni mamilioni ya Watanzania ambao hawakubaliani na siasa zake wala dhamira yake. Hapa nitatumia dhana ya ‘umagukrasia’ kuelezea vita vyake hivyo na namna ambavyo mimi siviungi mkono.
Umagukrasia ni aina ya utawala wa kisiasa ambao Rais Magufuli anaujenga, ambao unalenga kumtukuza yeye na chama chake juu ya kila kitu kwa gharama ya kuwadhalilisha wengine wote wasiokuwa wa chama chake au wasiomuunga mkono yeye. Kwa imani kwamba yeye – kama kiongozi mkuu wa dola na chama tawala – anamiliki pekee maarifa yote ya mwelekeo wa taifa na anaongozwa na nia safi isiyo doa kwenye kila anenalo na atendalo, Rais Magufuli hana uvumilivu hata chembe kwa wale wanaomuona tafauti.
Ukosefu wa uvumilivu wake unadhihirika kwa ayasemayo na ayatendayo dhidi ya sauti za ukosowaji ndani ya nchi, akitumia mikono yake aliyonayo kama mkuu wa dola, serikali, chama, na hivyo mwenye kauli ya juu kwenye mihimili mingine yote ya nchi.
Alianza na bunge, chombo kinachopaswa kuwa muhimili huru wa kuisimamia serikali. Kwa namna kilivyotekeleza wajibu wake wa kuikosoa na kuisimamia serikali kwenye awamu iliyopita, inaonekana Rais Magufuli anaamini kuwa ndiko kulikopelekea kwa mara ya kwanza kabisa, chama chake cha CCM kushindwa kuvuuka asilimia 60 ya kura za urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.
Kwa hivyo, kitu cha mwanzo kabisa alichofanya, ni kuliminya bunge kwa kulitenganisha na wananchi wa kawaida, ambao wanaonekana kuathirika na kinachoendelea Dodoma.
Kisha akaenda kwenye vyama vya kisiasa ambavyo vinaonekana kumpinga. Tunashuhudia sio tu kupigwa marufuku kwa mikusanyiko ya vyama hivyo, bali pia kuandamwa kwa viongozi wake wa ngazi mbalimbali, wakikamatwa, kuadhirishwa, kuadhibiwa, kufunguliwa kesi na hata kufungwa jela.
Kisha akaja kwenye vyombo vya habari vya kawaida (televisheni, redio na magazeti) na vya kisasa (hasa mitandao ya Facebook, WhatsApp na blogu), ambako sauti mbadala ya wananchi wa kawaida huwa inasikikana bila kupitia taratibu za kawaida za uchujaji.
Ndani ya kipindi hiki kifupi cha kuwapo kwake madarakani, redio na magazeti kadhaa yameshafungiwa na watumiaji kadhaa wa mitandao hiyo ya kijamii wameshakamatwa, huku wengine wakiripoti kuteswa, wengine wakifunguliwa mashitaka na wengine wakiwa wametoweka bila kujuilikana walipo hadi leo.
Inavyoonekana ni kuwa sasa mkono wa Rais Magufuli unazielekea asasi za kijamii ambazo zinajihusisha na masuala ya haki za binaadamu kwa ujumla wake ama haki za makundi maalum, kama vile vijana, wasichana na wanafunzi.
Haya na mengine ambayo yanafanywa na utawala wa Rais Magufuli katika jitihada zake za kupunguza duara la ukosowaji dhidi yake na kutanuwa duara la ama uungaji mkono wa kulazimisha au ukimya wa khofu, ndicho hicho ninachokiita ‘umagukrasia’.
Mwelekeo unaostahiki
Umagukrasia si jambo la kusifiwa wala kuungwa mkono na yeyote mwenye mapenzi ya kweli na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Taifa hili ilikuwepo kabla ya Rais Magufuli hajakuwa rais na misingi yake ya kitaifa, ikiwemo demokrasia, haki za binaadamu, kijamii na kisiasa na hishima kwa mawazo mbadala – licha ya mapungufu makubwa yaliyokuwa nayo – bado ilianzishwa na kuanza kuengwaengwa kidogo kidogo na waliomtangulia.
Rais Magufuli amekuja madarakani zaidi ya nusu karne tangu Watanzania waanze safari ya kuelekea kwenye utawala wa watu, unaotokana na watu na uliopo kwa ajili ya watu, wakiimarisha hatua kwa hatua taasisi zao za utawala – vyama vya siasa, vyama vya kiraia, vyombo vya habari, bunge, mahakama na serikali yenyewe.
Kama kiongozi mkuu wa dola, serikali na taifa, ana muda wake maalum wa kuwapo hapo. Ukifika atapaswa kuondoka kama walivyoondoka wenzake, lakini hataondoka na nchi hii. Jamhuri hii itabakia na itaendelea baada ya yeye.
Kwa hivyo, anatakiwa sio tu kuiwacha salama kisiasa kama alivyoikuta, bali pia ana wajibu wa kuongezea thamani kwenye misingi hiyo ya kitaifa na kikatiba aliyoikuta na sio kuiangamiza kama anavyoonekana sasa akifanya.
Ndio maana, kwa hilo la umagukrasia, mimi simuungi mkono kabisa kabisa.
TANBIHI: Makala hii ilichapishwa mara ya kwanza na gazeti la Mwelekeo la tarehe 4 Julai 2017.