BLOG POSTS

TA’AZIA: Khatib Said, Askari Aliyefia Vitani

Nilibahatika kumjua Marehemu Khatib Said Haji katika Bunge la 2015-2020 yeye akiwa wa Konde na mimi wa Malindi kwa tiketi ya Civic United Front. Sikuwa namjua uso kwa uso kabla.

Continue reading “TA’AZIA: Khatib Said, Askari Aliyefia Vitani”
UCHAMBUZI

Uhai wa CUF unategemea uadilifu wa mahakama

Kuna wanaohoji kwamba mgogoro uliopandikizwa kwenye Chama cha Wananchi (CUF) unaweza tu kumalizika kwa katibu mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad, kukaa kitako na aliyekuwa mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, kuyazungumzia wanayotafautiana.

Mtazamo wa mazungumzo ndio unaonekana, kijuujuu, kutajwa pia na Profesa Lipumba mwenyewe, ambaye katika siku za hivi karibuni alinukuliwa akisema kuwa mgogoro uliopo kwenye chama chake hicho cha zamani umalizwe kwa mazungumzo nje ya mahakama, lakini kwa sharti kubwa la, kwanza, Katibu Mkuu Maalim Seif kumtambua yeye, Lipumba, kuwa mwenyekiti wake na, pili, kwenda Ofisi Kuu za CUF zilizopo Buguruni, Dar es Salaam, ili aende akapangiwe kazi na mwenyekiti wake huyo.

Kauli ya mazungumzo kama njia ya kutatua migogoro inavutia. Inawashawishi wengi waiangalie kama suluhu pekee. Inawaweka wengi hao kwenye bawa la Profesa Lipumba, kumuona kuwa mtu wa suluhu, mtu wa mazungumzo, mtu wa muafaka.

Na Mohammed Ghassani

Wanaoshinikiza kuwa Maalim Seif azungumze na Profesa Lipumba wana hoja tatu mkononi mwao. Kwanza, ukweli kuwa njia ya mazungumzo ndio njia bora kabisa ya kumaliza tafauti baina ya wenye uhasama. Msemo wa kifalsafa hutuambia kuwa: “kinachoshindwa kutatuliwa kwa majadiliano, hakiwezi kutatuliwa kwa mapigano.”

Maana yake ni kuwa mapambano, kama haya yanayoendelea sasa kwenye CUF, hayatafanikisha chochote kwa upande wowote, bali mazungumzo – endapo yatafanyika kati ya pande hizo – ndiyo yanayoweza kuumaliza mkwamo uliopo.

Hoja ya pili waliyonayo ni kuwa, hata kama pametokea hitilafu kubwa baina ya Maalim Seif na Profesa Lipumba huko nyuma, basi uhasama wao hauwezi kuwa mkubwa kuliko uliokuwapo baina ya CUF kwa ujumla wake na CHADEMA, kwa upande mmoja, na au CUF na CCM, kwa upande mwengine, ambamo mote humo muwili, Maalim Seif na Lipumba walisimamia na kuongoza juhudi zilizopelekea makubaliano yaliyokuwa na faida kwa pande zote.

Kwa upande wa CUF na CHADEMA, Profesa Lipumba, ambaye chama chake kilishawahi kuitwa CCM B na cha wapenzi wa jinsia moja na CHADEMA, alikuja baadaye mwaka 2014 kushirikiana na CHADEMA, NCCR-Mageuzi na NLD kuasisi Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ambao umesalia hadi leo kuwa muungano pekee madhubuti wa vyama vya upinzani dhidi ya chama tawala – CCM.

Kwa upande wa CCM, Maalim Seif alikuja kushirikiana na aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho na Rais wa Zanzibar mwaka 2009, Amani Karume, kuasisi Maridhiano ya Wazanzibari ambayo nayo yalikuja kuzaa Mabadiliko Muhimu ya Katiba, Kura ya Maoni na hatimaye Serikali ya Umoja wa Kitaifa, ambayo ilihudumu baina ya 2010 na 2015 visiwani Zanzibar.

Hoja yao ya tatu ni kwamba, hata kama Profesa Lipumba na genge lake ni wasaliti kama unavyodai upande unaomuunga mkono Maalim Seif, bado ni upande huo wa wasaliti ambao wanapewa nguvu na kila nyenzo na vyombo vyote vya dola – polisi, ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, ofisi ya usajili na ufilisi, tume za uchaguzi, na kila aliye chini ya dola inayoongozwa na CCM.

Kwa mujibu wa hoja hii, Lipumba na kundi lake watashinda tu hatimaye kwenye vita hivi na watajipatia wanachokitaka, kama ambavyo hadi sasa wanaonekana kufanikiwa kwa kila wanalolifanya.

Wanatoa mfano wa karibuni kabisa wa Lipumba kuwafukuza wabunge wanane na madiwani wawili wa viti maalum, na kisha hatua hiyo kubarikiwa kwa uharaka wa ajabu na ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, bunge na tume ya uchaguzi.

Kwa hoja hii, ni kwamba ili Maalim Seif aendelee kubakia salama (ikiwa kweli hadi sasa yupo salama ndani ya CUF), basi ni kumridhia Profesa Lipumba kwa kila analolitaka. Ingawa wenye hoja hii hawahakikishi ikiwa endapo Profesa Lipumba akipatiwa hilo, atasimamia hapo au atataka mengine zaidi.

Nimesema kuwa hoja ya mazungumzo baina ya kambi mbili zilizopo mahakamani hivi sasa ndani ya CUF inashawishi sana. Kama unaiingia kichwa kichwa, unaweza kudhani kuwa upande wa Maalim Seif kwenye mzozo huu ni wapumbavu sana kutokuupokea haraka mkono wa maridhiano unaonyooshwa na Profesa Lipumba.

Lakini ukweli ni kuwa hoja hii imeanza kupotea njia tangu awali kabisa, na hivyo kuamua kuijibu kuangalia mwisho wake hakuna mantiki yoyote.

Kwanza, mgogoro huu uliopandikizwa kwa jina la Profesa Lipumba hauna tafauti hata kidogo na kile kitendo cha Jecha Salum Jecha wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kuufuta uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015. Mawili haya yana uhusiano mkubwa kwa asili, njia, lengo na hata muendelezo wake.

Kwa hivyo, kama vile ambavyo huwezi kuyajadili yaliyofuata baada ya tarehe 28 Oktoba 2015, pale Jecha alipochukuwa hatua hiyo, bila kulirejea kwanza hilo tukio lenyewe na kulipima uhalali na uharamu wake, kufaa na kutofaa kwake, ndivyo ambavyo mtu hawezi kulijadili hili la Lipumba bila kwanza kurejelea kwenye chimbuko lake.

Huwezi kuenda popote kabla yakwanya kulijadili na kulimaliza la kujiuzulu kwa Profesa Lipumba kwa hiyari yake, licha ya kuombwa sana na wenziwe akiwemo Maalim Seif kwamba asichukuwe hatua hiyo, na kisha kuja kujirejesha kwenye nafasi hiyo mwaka mmoja baadaye licha ya upinzani mkubwa wa hao hao waliomtaka mwanzo abakie.

Sharti kwanza mwenye kusaka suluhu baina ya kambi hizi mbili, amalizane na hili na uhalali na uharamu wa kitendo hicho, kufaa na kutofaa kwake. Akishamaliza hilo, ndipo sasa aje kwenye meza ya mazungumzo kusaka njia ya kwenda mbele baada ya hapo.

Pili, hoja hii ya mazungumzo baina ya Maalim Seif na Profesa Lipumba imejengwa juu ya upotoshaji kwamba mgogoro uliopandikizwa na ujio huo wa Profesa Lipumba mwaka mmoja baada ya kujiuzulu, ni mgogoro baina ya Maalim Seif na yeye, Profesa Lipumba.

Licha ya wote wawili kurejelea mara kwa mara kwamba wao kama wao wana historia ya miongo kadhaa kama marafiki wa karibu, wajengaji wa hoja hii wanakataa uhalisia huo.

Bahati mbaya ni kwamba baada ya kwishajirejesha madarakani, hata Profesa Lipumba ameazima maneno hayo hayo ya kueleza uhasama baina yake na Maalim Seif, akiwacha kabisa hoja ya msingi inayozozaniwa hapa, ambayo ni matakwa ya katiba, kwa upande mmoja, na ya kimaadili, kwa upande mwengine.

Kuliweka hili kwenye nafasi yake, ni vyema ikafahamika kuwa chimbuko la mzozo huu halimo kwenye ugomvi wa wawili hao, bali limo kwenye katiba na maadili ya kiuongozi. Profesa Lipumba aliondoka kwenye uwenyekiti wa CUF kwa hoja madhubuti ya kimaadili.

Kwamba akiwa kinara wa kupambana na ufisadi, nafsi yake ilikuwa inamsuta kujiona kuwa analazimika sasa kuungana na kumpigia debe mshukiwa mkuu wa ufisadi nchini Tanzania, Edward Lowassa. Akatumia haki yake ya kikatiba, kuiacha nafasi ya kukiongoza chama chake katika wakati ambao, kwa hakika, kilikuwa kikimuhitaji sana.

Maadili na katiba vikafanya kazi yake kwake wakati huo, ikitarajiwa kuwa maadili na katiba hiyo hiyo vingelifanya kazi tena baadaye. Haikuwa hivyo, kwa upande wake. Lakini imekuwa hivyo kwa upande wa waliompinga wakati ule alipoondoka na wanaompinga leo alipojirejesha.

Na ni kwa msingi huo huo wa maadili ya kiuongozi na katiba, ndipo ambapo roho ya dhati ya CUF inasalia hadi leo. Ndipo tamaa ya kuendelea uhai wa roho hiyo ulipo. Na, hapana shaka, hakuna mahala pengine popote ambapo roho ya maadili na katiba inaweza kuhuishwa pasipokuwa kwenye mahakama inayoutambua wajibu wake na inayotenda kazi kiadilifu.

Swali ni kwamba je, idara ya mahakama nchini Tanzania inazo sifa hizo za uhuru, usawa na uadilifu? Mpaka hapo kesi hizi zitakapoamuliwa, majibu ya uhakika hakuna aliyenayo. Hiyo ni kwa sababu, katika mifano kadhaa, muhimili huu wa kugawa haki umeonekana kuchezewa na muhimili wa dola, ingawa ipo pia mifano ambapo ulisimama imara.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 21 Agosti 2017

UCHAMBUZI

Akina Mnyaa, Khalifa na wenzao hawatuwakilishi Wapemba

Hii si mara ya kwanza kwa Chama cha Wananchi (CUF) kujikuta kwenye mgogoro unaokimomonyoa ndani kwa ndani na kisha kikainuka imara kusonga mbele, lakini lazima tuseme wazi kuwa mgogoro wa safari hii si kama mingine ya nyuma na kuna wasiwasi kuwa kinaweza kushindwa kuvuuka salama usalimini.

Katika mengi yaliyoibuka ndani ya mgogoro huu mkubwa, leo nataka nizungumzie kitu kimoja tu – nacho ni hawa waliojiunga na timu ya Profesa Ibrahim Lipumba kutokea visiwani Zanzibar, ambapo ukiziangalia sura zote zilizokwishajitokeza waziwazi hadi hivi sasa, unachoweza kukiona ni kisiwa cha Pemba.

Nassor Seif Amour, Mussa Haji Kombo, Mohamed Habib Mnyaa, Haroub Mohamed Shamis, Khalifa Suleiman Khalifa, Rukiya Kassim Ahmed na Thiney Juma Mohamed, wote wanatoka kisiwani Pemba, ambako kunasalia kuwa ngome madhubuti ya CUF na ambako daima kumekuwa kukikiadhibu Chama cha Mapinduzi (CCM).

Na Mohammed Ghassani

Ukimtoa mwanajeshi Thiney Juma Mohamed, waliobakia wote wamewahi kuwa wabunge na au wawakilishi katika nyakati tafauti, huku wengine kama Khalifa wakikaa bungeni tangu uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995. Kwa hivyo, pamoja na kujitolea kwao kukubwa kukijenga chama, kwa hakika wao ndio hasa waliojengwa na CUF.

Pemba, kisiwa ambacho mimi pia ninatokea, kinatambulika kihistoria kwa upinzani wake dhidi ya watawala kisiowakubali, hata wawe na nguvu kiasi gani. Wenyewe Wapemba tuna fakhari ya kuwa kizazi cha wahenga waliopambana na kuushinda utawala katili wa Mreno baada ya karne nzima, tunajivunia kuupinga utawala wa Busaid, na hata uliofuata baadaye wa Mwingereza na kisha wa CCM.

Kwa sababu zinazofanana, kisiwa hiki kimekuwa sehemu ya mapambano ya Zanzibar dhidi ya wanachoamini Wazanzibari kuwa ni utawala wa Tanganyika kwa hadhi ya nchi yao.

Ukweli kwamba CUF iliungwa mkono na kisiwa kizima cha Pemba mara tu ilipoanzishwa, haukutokana pekee na sababu ya kuwa mmoja wa waanzilishi wake, Maalim Seif Sharif Hamad, ni mzaliwa wa kisiwa hicho, bali pia, na zaidi, ni kwa sababu kisiwa chenyewe kilikuwa kinasaka muda mrefu jukwaa la kuonesha upinzani wake dhidi ya mtawala wasiyemkubali.

Kwa nini sasa wanasiasa hawa kutoka Pemba wamekuwa sehemu ya genge linalosimama dhidi ya chama ambacho kimekuwa daima alama ya mapambano ya Zanzibar dhidi ya mtawala aliyeshiriki, kupanga na kuwahujumu wananchi wa Zanzibar kwa miaka-nenda, miaka-rudi?

Kwa nini akina Mnyaa na Khalifa, ambao walikaa muda mrefu bungeni kwa kura za Wapemba wenzao, wakafaidika kiuchumi wao na familia zao, wamegeuka leo dhidi ya maslahi mapana ya watu waliokanyaga mabega yao kujiinuwa?

Kwa nini akina Nassor Seif na Mussa Haji wawe sehemu ya mchakato wa kuipeleka CUF njia ya NCCR-Mageuzi, chama kilichowahi kuwa na nguvu sana mwanzoni mwa mfumo wa vyama vingi na kutikisa nchi kwenye uchaguzi wa 1995, lakini kikapandikiziwa migogoro ya kiuongozi na hatimaye kusambaratishwa, hadi sasa kimesalia na mbunge mmoja tu bungeni?

Kwa nini akina Thiney na Bi Rukiya wawe sehemu ya mkakati wa kuimaliza CUF, ambayo hadi mwaka 2015 ilikuwa sehemu ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa visiwani Zanzibar na iliyowahi kuwa ya pili kwa ukubwa bungeni na kusaidia kuikaribisha Zanzibar kwenye ndoto yake ya kuwa na mamlaka kamili ndani ya Jamhuri ya Muungano?

Majibu ya maswali haya wanaweza kuwa nayo zaidi wenyewe, na pengine wataandika kujibu kwa wakati wao, lakini hawawezi kuondosha ukweli uliopo; kwamba, kwanza, wanachokifanya kiko dhidi ya Zanzibar yao na hivyo kisiwa chao cha Pemba walikozaliwa na kukulia na, pili, kwamba wao ni wasaliti dhidi ya Pemba na Wapemba.

Kwa yote mawili, hawa si wawakilishi wa Wapemba, mimi nikiwa mmoja wao. Nimezaliwa, kukulia na kufundwa ndani ya kisiwa hicho. Mbali ya kuutangatanga ulimwengu, bado nabakia sehemu ya Wapemba na Wazanzibari wanaojuwa nini tunakisimamia kwenye taswira ndogo ya Zanzibar na Tanzania, na kisha taswira kubwa ya Afrika Mashariki, Afrika na hata dunia kwa ujumla.

Ukihesabu gharama ambazo hata wao wenyewe zimeshawapata kwenye mapambano haya, ikiwemo kufungwa, kupigwa na hata kuuliwa kwa ndugu na jamaa zao wa karibu, akina Mnyaa na Khalifa hawakupaswa kabisa kuwa mahala hapa tupaitapo kwa Kipemba ‘asfala-safilina’ – yaani chini kuliko walio chini, panapohusika dhamira.

Lakini pengine swali kubwa kuliko yote ni kwa nini CUF yenyewe – kama chama – imefikishwa mahala hapa? Wengine wanasema ni kutokana na kosa la uongozi wenyewe wa CUF kuchelewa kuchukuwa hatua muafaka kutokana na masharti ya katiba yao, pale pale na wakati ule ule Lipumba alipoamua kuwaacha mkono wakati wakimuhitaji sana karibu na uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Kwao wao, laiti CUF ingelifuata kikamilifu katiba yake tangu siku Lipumba anajiuzulu mwenyewe na kwenda zake Rwanda, basi kiongozi huyo asingelikuwa tena na nafasi ya kurejea kuivuruga CUF kwa namna ambayo anafanya sasa kwa mafanikio makubwa kupitia mkono wa dola na ushirikiano aupatao kutoka kwa hawa waliaomua kujiunga na usaliti kutokea kisiwani Pemba.

Lakini kwa wanaoujuwa ukweli wa mambo, majibu si mepesi kiasi hicho. Hao wanajuwa kuwa CUF haidhuriwi kabisa na katiba yake, bali inadhuriwa na mambo matatu makubwa kwenye hili: kwanza ni msimamo wake dhidi ya uhuni uliotendeka Zanzibar tarehe 28 Oktoba 2015, siku uliyofutwa uchaguzi mkuu wa Oktoba 25.

CCM na vyombo vyake vya dola kwenye serikali zote havikuwahi kuisamehe CUF kwa jinsi chama hicho kilivyowaweka uchi katika kadhia hii nzima. Kwa CCM, chama cha CUF kinapaswa kuondoka kwenye uso wa dunia haraka iwezekanavyo kabla ya uchaguzi mwengine wowote ujao, maana aibu ya Oktoba 2015 visiwani Zanzibar hawakuweza kuifidia hadi leo.

Pili, CUF inadhuriwa na msimamo wake wa muda mrefu kuelekea mfumo wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, kwani hiki ni chama pekee cha kisiasa ambacho kimejijenga vizuri mno katika “Siasa za Muungano” katika kiwango ambacho CCM inapoteza kila uchao kutokana na uungwaji mkono unaoongezeka kwa hoja ya CUF juu ya Muungano huo.

Hili halijaanza leo, na daima vyombo vya dola vimekuwa vikisaka njia ya kuimaliza CUF ili kunyamazisha kabisa hoja dhidi ya Muungano wenyewe. Hadi kufikia mgogoro huu mkubwa kabisa wa Lipumba, CUF ilishapandikiziwa mingine mingi huko nyuma kwa mkono wa vyombo vya dola kutokana na msimamo wake huo.

Na, tatu, CUF inadhuriwa na hatua yake ya kujiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ambao uliitikisa sana CCM kwenye uchaguzi mkuu wa 2015, kiasi cha kwamba kwa mara ya kwanza chama hicho tawala kilikosa asilimia 60 ya kura za jumla. Kwenye hili, CUF hailengwi peke yake, bali ni pamoja na mshirika wake mkuu, CHADEMA, ambacho kimekumbwa na ukandamizaji mkubwa dhidi ya viongozi wake tangu kumalizika uchaguzi huo.

Kwa hivyo, Lipumba na wenzake hawapo kwenye nafasi ya kushinda ‘vita’ vinanavyoendelea sasa eti kwa kuwa uongozi wa CUF ulidharau kuitumia katiba yao kwa wakati tu, lakini zaidi ni kwa kuwa CCM na vyombo vya dola vinataka kuona kuwa CUF inasambaratika kabla ya uchaguzi mkuu wa 2020 ili kuyauwa kabisa madai ya chama hicho kwa uchaguzi wa 2015 Zanzibar, kuizika moja kwa moja ajenda ya Zanzibar kuhusu Muungano na ikibidi kuiuwa kabisa UKAWA.

Uongozi wa CUF unalijuwa hili na unasema mara kadhaa kuwa haupambani na Lipumba na genge lake wala haupingani na katiba ya chama chao, bali unapambana na kupingana na dola nzima iliyosimama nyuma ya genge hilo.

Ni jambo la kushangaza sana kwamba, kwa upande wa Zanzibar, genge hilo linaundwa na wanasiasa kutoka kisiwani Pemba pekee, anakotokea Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif, tena baadhi yao, muna ambao kupanda kwao ngazi kuliwezeshwa kwa hishima tu ya wanachama kwa Maalim Seif tu, na si vyenginevyo.

Siku wananchi walipoamua kuchukuwa hatua dhidi ya wanasiasa hawa kwa njia zao wenyewe kwenye kura za mchujo huko mashinani na wakaangushwa, akina Mnyaa, Khalifa, Mussa Haji, Rukia na wenzao, ndipo walipojitokeza kwa sura zao halisi. Maslahi.

Ni bahati mbaya kwamba sasa wanatumia sura zao hizo kuiuwa taasisi pekee ambayo ilitegemewa sio tu na wapigakura wa kisiwa chao, bali pia na Wazanzibari na Watanzania wengine kwa ujumla, kama jukwaa la kuisemea na kuitetea Zanzibar kitaifa na kimataifa.

Hawa ndio wale waitwao wa Kipemba: “Nalitote!” Madhali wao wamekosa ulwa ndani ya CUF, basi CUF nayo naife.