BLOG POSTS

The Politademic Bashiru in Mr. Mandola’s Whisky

The character Mr. Mandola in a 2013 Bollywood’s Matru Ki Bijlee Ka Mandola is very rich, very alcoholic and also very revolutionary. But in this political satire film, the side of a revolutionary Harphool Singh Mandola (played by Pankaj Kapur), is not seen in his character until he is drunk.

Continue reading “The Politademic Bashiru in Mr. Mandola’s Whisky”

UCHAMBUZI

Tanzania hailiwi na rushwa pekee, bali pia na ufisadi wa kisiasa

Majuzi Rais John Magufuli alimuapisha Brigedia Jenerali John Mbungo kuwa Naibu Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana  na Rushwa (TAKUKURU) akiweka msisitizo kwamba anataka kuona wala rushwa wanafungwa jela haraka iwezekanavyo.

Kwa maneno yake mwenyewe Rais Magufuli, “mambo makubwa ambayo taifa linapambana nayo yanatokana na rushwa…” na kwamba kama Tanzania ikifanikiwa kuipunguza rushwa angalau kwa asilimia 80, basi itakuwa imeyatatua matatizo yake mengi sana.

Hakuna anayepinga kwamba Tanzania, ambayo imeongozwa na Chama cha Mapinduzi (CCM) – chama chake yeye Rais Magufuli – muda wote wa kuwa kwake taifa huru, imeoza kwa rushwa. Inanuka, imeoza, kila mahala, kila sekta!

Lakini katikati ya uoza huo, au pengine kwa sababu ya uoza huo, ndipo unapokuta hii tabia yetu mbovu ya kuuzungumzia uchafu kwa maneno yanayochuja kimaana. Mojawapo likiwa ni hili la kuuita ufisadi kuwa ni rushwa. Rushwa tu!

Ukweli ni kuwa rushwa ni kitu kidogo sana panapohusika uoza wenyewe hasa uliopo. Rushwa ni utowaji na au upokeaji wa kitu (mara nyingi huwa pesa) kwa ajili ya kutoa au kupokea huduma, ambayo kimsingi ingelikuwa haki kutolewa bila ya kitu hicho.

Na Mohammed Ghassani

Wengi wetu tunadhani rushwa ni sawa na ule msamiati wa Kiingereza ‘corruption’, ndiyo maana hata hiyo taasisi inayoshughulika na kadhia hiyo inaitwa TAKUKURU kwa kuwa tunasema inafanya kazi ya kupambana na kuzuia rushwa.

Na kwa kuwa tunakosea kwenye kuipa jina lake halisi hali hii tunayokabiliana nayo, ndio  maana tunazunguka mumo humo, tukiamini kwamba kubadilisha sura kwenye chombo chenye mamlaka ya kupambana na hali hii kunatosha kuimaliza.

Ukweli ni kwamba kuiangalia hali kwa jicho lake halisi kuna nafasi kubwa mno kwenye kuzifikia hizo asilimia 80 anazolenga Rais Magufuli kwenye vita hivi vikubwa na, kwa hakika, vyenye maana kwetu sote.

Tanzania inaliwa na ufisadi na sio rushwa pekee, na tena ufisadi mkubwa zaidi ni ule wa kisiasa, ambao umejengewa mihimili kwa miaka 50 ya utawala wa CCM, kiasi cha kuufanya uonekane hali ya kawaida kwenye maisha ya kila siku.

Ufisadi wa kisiasa unakwenda mbali zaidi ya pale rushwa ya kutoa na kupokea fedha inapoishia. Huu ni utumiaji mbaya wa madaraka unaofanywa na maafisa wa serikali na, au, wa taasisi za kisiasa kwa maslahi binafsi. Aina zake ni za viwango tafauti, na hiyo rushwa moja tu miongoni mwao.

Katika upana wake utakuta pia udugunaizesheni, wizi wa kura, milungula, wizi wa mali ya umma na ubadhirifu, kwa kutaja machache.

Ufisadi huu wa kisiasa, kwa hakika, ndio mama wa maovu mengine yote katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uovu wa madawa ya kulevya, ujambazi, ukahaba na umasikini wa watu wetu, kwa mfano, ni matokeo ya ufisadi wa kisiasa ambao umekuwa ukiila nchi yetu kwa zaidi ya miongo mitano sasa.

Bahati mbaya ni kuwa ufisadi huu una khulka moja ya hatari sana: kuzoeleka. Kila anayechukua nafasi ya uongozi wa umma katika serikali au taasisi ya kisiasa huona sawa kwake kuwa fisadi, na kwa hakika jamii humtarajia awe hivyo. Kwamba atumie fursa ile kujinufaisha binafsi, awatishe wengine, awakomowe, awaangamize ili yeye awe hapo alipo .

Ndio maana maafisa wa tume za uchaguzi huiba kura kwa ajili ya kuwanufaisha wanasiasa wanaowapa vyeo, wagombea hununua wapiga kura, polisi hula mkono kwa mkono na wahalifu, maprofesa hupasisha au kufelisha wanafunzi vyuoni kwa kuzingatia maslahi yao binafsi. Alimradi ni mchafukoge.

Jamii hii ya mchafukoge ni muakisiko wa ufisadi wa kisiasa uliopea na kuzoeleka. Utamaduni wa chukua chako mapema, wa iba ulindwe na kemea udhibitiwe (kama wanavyoonekana kudhibitiwa wapinzani sasa), ndio unaojenga fikra za Watanzania uwaonao mbele yako leo.

Si hasha, kwa hivyo, kusikia hata miongoni mwa kada za hao waitwao wasomi leo hii wakisema: “Naye Tundu Lissu kazidi kidomodomo.” Kwao wao ufisadi ni ada ya maisha ya kila siku.

Kilele cha utamaduni huu huwa ni kile kinachoitwa kleptocracy (rule by thieves), yaani utawala wa wizi – wizi wa kura, wizi wa mali, wizi wa matumaini, wizi wa kesho ya wanyonge walio wengi.

Ufisadi una hatari kubwa na ya pekee katika maendeleo ya taifa. Katika siasa, hufifisha na wakati mwengine kuua kabisa mfumo wa kidemokrasia na utawala wa sheria, maana ufisadi una kiburi cha kuingilia kati chochote ambacho kinaonekana kiko dhidi yake. Ukweli ni kwamba demokrasia na utawala wa sheria ni adui kwa ufisadi; na kilipo kimoja chengine hakikai.

Kwa hivyo, kwa jamii kama yetu, ambayo imejikita katika uoza wa kupindukia wa ufisadi, mafisadi wenyewe hawataki kabisa kuona mfumo wa demokrasia ukistawi ama utawala wa sheria ukisimama. Si ajabu, kwa hivyo, kuona wakiingilia kati taratibu za kawaida za kidemokrasia na za utawala wa sheria kila pale wanapoona zinachukuwa mkondo wake.

Ya kuharibiwa kila mara kwa chaguzi za Zanzibar, kwa mfano, kwa kupelekwa majeshi yenye silaha nzito nzito ni katika hizo jitihada za ufisadi kupingana na demokrasia na utawala wa sheria.

Ufisadi katika chaguzi hupelekea ofisi za umma kukaliwa na watu wasiotokana na ridhaa ya umma na hivyo nao matokeo yake huzikalia ofisi hizo kwa maslahi yao binafsi na sio kwa maslahi ya umma, maana sio uliowaweka ofisini.

Leo hii Rais Magufuli anapolilia ukosefu wa uzalendo miongoni mwa wenzake serikalini – wanaofikia hadi kusaini mikataba ya kuuza madini kiholela – anapaswa kujiuliza namna hao watiaji saini walivyofika hapo madarakani. Je, ni kwa demorasia au kwa ufisadi wa kisiasa?

Ufisadi katika vyombo vya kutunga sheria hupunguza au huondosha kabisa uwajibikaji na uwakilishi wa kweli katika vyombo hivyo; ufisadi kwenye mahakama huiweka rehani haki ya wananchi; na ufisadi kwenye utawala husababisha ukosefu wa uadilifu katika utowaji wa huduma za kijamii.

Kwa jumla, ufisadi hukokozoa kabisa uwezo wa kitaasisi wa serikali, kwani husababisha taratibu kupuuzwa, rasilimali kuporwa, na ofisi za umma kuuzwa na kununuliwa kama bidhaa nyengine yoyote.

Ufisadi wa kisiasa ukipevuka huufanya hata uhalali wa serikali iliyopo madarakani uhojike na vivyo misingi ya demokrasia na kuaminiana itoweke. Ni mapema, pengine, sasa kwa wananchi wa Tanzania kuhoji uhalali wa serikali yao, lakini kwa mwenendo huu tunaokwenda nao, si muda mrefu tena ujao, hilo la kuhoji litakuwa wajibu wetu wa mwanzo!

Lakini wakati tukisubiri wakati huo ufike, sote ni mashahidi wa namna ambavyo ufisadi wa kisiasa unadumaza maendeleo ya kiuchumi kwa kuchochea ubadhirifu na ukosefu wa ufanisi.

Watanzania wameshuhudia mali za nchi zikiibiwa mbele ya macho yao: mchanga wa dhahabu unasafirishwa makontena kwa makontena, meli za kigeni zinavua tani kwa tani za samaki kwenye bahari yao, na wenye vyeo wanajikopesha na kujikatia juu kwa juu kutoka hazina ya taifa.

Na hayo hayajasimama kwa kuwa Rais Magufuli kasema anataka kuwaona wala rushwa wakifungwa jela. Yatasimama kwa kuuita ufisadi kwa jina lake halisi na kuutendea kama ututendeavyo – kuuwa maana nao unatuuwa.

Haitoshi kila siku kulia majukwaani na kwenye vichwa vya habari magazetini. Kuuzungumzia ufisadi kwa jina la rushwa hakutoshi. Kueleza ushahidi wa rushwa hiyo ilivyolimaliza taifa pia hakutoshi.

Hakutoshi, maana baada ya kuwa mashahidi na walalamikaji miaka yote 50 ya taifa huru, kumetusaidia nini? Kwa karibuni miongo mitano yote, hiyo imekuwa hali ambayo taifa hili limeishi nayo.

Leo hii tunajikokota kwenye mstari wa mwisho wa umasikini duniani, watoto wetu wakifa kwa maradhi na njaa, na bado tumeendelea kuwa mashahidi na walalamikaji ambao tunalizunguka tatizo lenyewe, badala ya kutua katikati yake – penye ufisadi wa kisiasa.

Kwa hivyo, si mwanajeshi  John Mbungo anayepaswa kuvaa magwanda yake kupambana na ufisadi huu wa kisiasa, maana si ajabu kuwa hata yeye mwenyewe ni matokeo ya mfumo uliousimamisha ufisadi wa aina hiyo, na ndio maana hata amiri jeshi wake anataka tu akahakikishe anawafunga wala rushwa. Wala rushwa tu!

Ni wananchi wanaopaswa, kwanza, kuufahamu  ufisadi wa kisiasa ambao Tanzania imekulia nao. Kisha, pili, kuuchukia kwelikweli, na mwisho, la tatu, kuchukuwa hatua dhidi ya uoza huu kwa njia halali.

Miongo hiyo mitano ya ufisadi wa kisiasa imewashuhudia watawala wale wale wakiwazoesha kuupenda na kuushabikia ufisadi na kuufanya kuwa utamaduni wao. Wamewapotosha vya kutosha. Wamefanywa waone jambo la kawaida kutoa na kupokea rushwa. Wamewafanya wautarajie ufisadi na wautegemee kama njia ya kupita kufika waendako.

Wanapaswa sasa kukataa na kusema hapana. Hapana kwa ufisadi wa kisiasa. Hapana kwa mafisadi wa kisiasa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHALISI la tarehe 28 Agosti 2017.

 

UCHAMBUZI

Ndiyo kwa ‘uchumagu’, hapana kwa ‘umagukrasia’

Kitu kimojawapo ambacho Rais John Magufuli anajipambanuwa nacho kwa haraka na watangulizi wake, ni tabia yake ya kutokuwa na ajizi na vile kutozingatia kwake mipaka kwenye huko kutokuwa na ajizi. Hayo ni kwa kila alisemalo na kila alitendalo. Kutokuwa na ajizi ni jambo jema kwa kiongozi, lakini kutokuzingatia mipaka si jambo la kusifiwa hata kidogo.

Hapa ndipo ambapo, kwa mwenye akili, anapoweza kirahisi kuchora mstari wa namna ya kumchambua, kumtafakari na kuchaguwa lipi ni lipi kwenye shakhsia ya Rais Magufuli, na kwayo isimuwiye vigumu kujuwa pa kuungana naye na pa kupingana naye.

Kinyume na wanavyochukulia wale wanaojiaminisha kuwa uzalendo hasa ni kumuunga mkono kiongozi wa nchi kwa lolote aliwazalo, alinenalo na alitendalo, utendaji kazi wa Rais Magufuli unawasuta sio tu kwa kutokujuwa kwao maana halisi ya uzalendo, bali pia kwa kuwaonesha kuwa hawana msaada wowote wa maana si kwa Rais Magufuli mwenyewe, wala kwa serikali yake na hata kwa chama chake kinachotawala, CCM.

Ufanyaji wake maamuzi, utoaji wa kauli zake na utendaji kazi wake unatufanya wengine kuona kuwa hata kama hatuna ulazima wa kumuunga mkono kwa kila jambo lake, bado pia hatuna ulazima wa kumpinga kwa kila kitu. Kwamba muna mwahala, kwa mtazamo wetu, anafanya vyema na anahitaji kupewa heko na kusaidiwa na muna mwengine ambamo anafanya vibaya na anapaswa kukosolewa na kuzuiwa.

Uchumagu na Tanzania inayotakiwa

Na Mohammed Ghassani

Binafsi, namuunga mkono Rais Magufuli kwenye hili ninaloliita hapa ‘uchumagu’ – uchumi wa Magufuli, dhana inayowakilisha jitihada zake binafsi kama kiongozi wa nchi kuhakikisha kuwa uchumi wa nchi unakuwa na kuwagusa wananchi wa kawaida, ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakitengwa kando.

Ndani ya jitihada hizi, muna kampeni kubwa ya kupambana na ufisadi, wizi wa mali ya umma, ukosefu wa uwajibikaji na kiwango kikubwa cha uholela kwenye sekta ya umma. Muna pia jitihada zinazoonekana za kuimarisha miundo mbinu na kuwafikia watu kule waliko. Hapana shaka, mafanikio ya kampeni hii ni faida kwa umma na yana athari za moja kwa moja kwa mwananchi wa kawaida.

Hakuna mwenye mapenzi ya kweli kwa nchi, ambaye hataweza kuunga mkono pale, mathalani, watuhumiwa wa ufisadi wanapofikishwa mahakamani kujibu mashitaka dhidi yao. Hakuna pia atakayepinga pale siku maafisa wa serikali waliokuwa wamepewa dhamana kubwa kuwahudumia wananchi na wakazifanyia khiyana dhamana hizo ‘wanayotumbuliwa’.

Ingawa hata watu wanaweza kukosoa njia zinazotumika kwa kuhofia zisije zikawa za zimamoto na kulifanya lengo halisi kutofikiwa, lakini wanajuwa kuwa vita dhidi ya ufisadi ni jambo linalohitajika.

Baada ya zaidi ya nusu karne ya kutawaliwa na chama cha Rais Magufuli, CCM, serikali za pande zote mbili za Muungano zilishageuka kuwa jalala la uchafu wote wa kiuongozi:  kuanzia wizi wa mali ya umma, udugunaizesheni (upendeleo wa kifamilia na kieneo), ubadhirifu, uzembe na ukosefu wa uwajibikaji.

Kwa ujumla, ufisadi umekuwa ni wa kimfumo ndani ya serikali hizi, kuanzia juu kabisa hadi chini kabisa kwa kipindi kirefu sasa. Hata hizo enzi za Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid Karume, ambazo wengine hutaka kutuaminisha kuwa zilikuwa zama za usafi wa kimaadili, ushahidi unaonesha kuwa zilikuwa na makandokando yake mengi na ndiyo hayo yaliyoasisi uovu uliokuja kudhihirika baadaye.

Mwenyewe Mwalimu Nyerere alikuwa akikiri kuwa hata katika uongozi wake kulikuwa na rushwa, lakini alitaka tukubali kuwa yeye na wenzake wachache waliokuwa juu walikuwa hasa wakiichukia rushwa kwa vitendo, na kwamba kila walipopata mashaka na mteule yeyote aliye chini yao kuhusika na rushwa, basi walimchukulia hatua hapo hapo bila kuchelewa na bila kuchelea.

Kwa hivyo, kwamba leo Rais Magufuli anaongoza vita vya kuukomboa uchumi kutoka mikononi mwa ufisadi wa ndani na wa kimataifa na dhidi ya uporaji wa rasilimali unaofanyika kupitia mikataba ambayo serikali zilizoongozwa na chama chake ziliingia huko nyuma, ni wazi kuwa anapigana vita ambavyo anastahiki sifa na kuungwa mkono, hata kama ni vita vinavyotokana na uchafu uliotendwa na chama chake mwenyewe huko tutokako.

Kwa kutumia maneno yake ya tarehe 1 Julai 2017, wakati akifungua Maonesho ya Sabasaba: “Tanzania tumechezewa sana kwa sababu tulitaka kuchezewa. Lakini sasa kuchezewa basi!” Nami nafanya hivyo: namsifu na namuunga mkono. Tanzania kama taifa lilichezewa sana kwenye uchumi wake kwa kuwa wao kama watawala walitaka taifa hili lichezewe. Kufanikiwa kwa Rais Magufuli kwenye vita hivi, ni kufanikiwa kwa taifa zima.

Tanzania haiuhitaji umagukrasia

Lakini kando ya vita vyake hivi, Rais Magufuli anapigana pia vita vyengine, ambavyo mpigaji hasa ni peke yake kwa kuwa ana nyenzo za kumuwezesha kupiga pasi yeye kushambuliwa, na anaowapiga vita hivyo ni mamilioni ya Watanzania ambao hawakubaliani na siasa zake wala dhamira yake. Hapa nitatumia dhana ya ‘umagukrasia’ kuelezea vita vyake hivyo na namna ambavyo mimi siviungi mkono.

Umagukrasia ni aina ya utawala wa kisiasa ambao Rais Magufuli anaujenga, ambao unalenga kumtukuza yeye na chama chake juu ya kila kitu kwa gharama ya kuwadhalilisha wengine wote wasiokuwa wa chama chake au wasiomuunga mkono yeye. Kwa imani kwamba yeye – kama kiongozi mkuu wa dola na chama tawala – anamiliki pekee maarifa yote ya mwelekeo wa taifa na anaongozwa na nia safi isiyo doa kwenye kila anenalo na atendalo, Rais Magufuli hana uvumilivu hata chembe kwa wale wanaomuona tafauti.

Ukosefu wa uvumilivu wake unadhihirika kwa ayasemayo na ayatendayo dhidi ya sauti za ukosowaji ndani ya nchi, akitumia mikono yake aliyonayo kama mkuu wa dola, serikali, chama, na hivyo mwenye kauli ya juu kwenye mihimili mingine yote ya nchi.

Alianza na bunge, chombo kinachopaswa kuwa muhimili huru wa kuisimamia serikali. Kwa namna kilivyotekeleza wajibu wake wa kuikosoa na kuisimamia serikali kwenye awamu iliyopita, inaonekana Rais Magufuli anaamini kuwa ndiko kulikopelekea kwa mara ya kwanza kabisa, chama chake cha CCM kushindwa kuvuuka asilimia 60 ya kura za urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.

Kwa hivyo, kitu cha mwanzo kabisa alichofanya, ni kuliminya bunge kwa kulitenganisha na wananchi wa kawaida, ambao wanaonekana kuathirika na kinachoendelea Dodoma.

Kisha akaenda kwenye vyama vya kisiasa ambavyo vinaonekana kumpinga. Tunashuhudia sio tu kupigwa marufuku kwa mikusanyiko ya vyama hivyo, bali pia kuandamwa kwa viongozi wake wa ngazi mbalimbali, wakikamatwa, kuadhirishwa, kuadhibiwa, kufunguliwa kesi na hata kufungwa jela.

Kisha akaja kwenye vyombo vya habari vya kawaida (televisheni, redio na magazeti) na vya kisasa (hasa mitandao ya Facebook, WhatsApp na blogu), ambako sauti mbadala ya wananchi wa kawaida huwa inasikikana bila kupitia taratibu za kawaida za uchujaji.

Ndani ya kipindi hiki kifupi cha kuwapo kwake madarakani, redio na magazeti kadhaa yameshafungiwa na watumiaji kadhaa wa mitandao hiyo ya kijamii wameshakamatwa, huku wengine wakiripoti kuteswa, wengine wakifunguliwa mashitaka na wengine wakiwa wametoweka bila kujuilikana walipo hadi leo.

Inavyoonekana ni kuwa sasa mkono wa Rais Magufuli unazielekea asasi za kijamii ambazo zinajihusisha na masuala ya haki za binaadamu kwa ujumla wake ama haki za makundi maalum, kama vile vijana, wasichana na wanafunzi.

Haya na mengine ambayo yanafanywa na utawala wa Rais Magufuli katika jitihada zake za kupunguza duara la ukosowaji dhidi yake na kutanuwa duara la ama uungaji mkono wa kulazimisha au ukimya wa khofu, ndicho hicho ninachokiita ‘umagukrasia’.

Mwelekeo unaostahiki

Umagukrasia si jambo la kusifiwa wala kuungwa mkono na yeyote mwenye mapenzi ya kweli na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Taifa hili ilikuwepo kabla ya Rais Magufuli hajakuwa rais na misingi yake ya kitaifa, ikiwemo demokrasia, haki za binaadamu, kijamii na kisiasa na hishima kwa mawazo mbadala – licha ya mapungufu makubwa yaliyokuwa nayo – bado ilianzishwa na kuanza kuengwaengwa kidogo kidogo na waliomtangulia.

Rais Magufuli amekuja madarakani zaidi ya nusu karne tangu Watanzania waanze safari ya kuelekea kwenye utawala wa watu, unaotokana na watu na uliopo kwa ajili ya watu, wakiimarisha hatua kwa hatua taasisi zao za utawala – vyama vya siasa, vyama vya kiraia, vyombo vya habari, bunge, mahakama na serikali yenyewe.

Kama kiongozi mkuu wa dola, serikali na taifa, ana muda wake maalum wa kuwapo hapo. Ukifika atapaswa kuondoka kama walivyoondoka wenzake, lakini hataondoka na nchi hii. Jamhuri hii itabakia na itaendelea baada ya yeye.

Kwa hivyo, anatakiwa sio tu kuiwacha salama kisiasa kama alivyoikuta, bali pia ana wajibu wa kuongezea thamani kwenye misingi hiyo ya kitaifa na kikatiba aliyoikuta na sio kuiangamiza kama anavyoonekana sasa akifanya.

Ndio maana, kwa hilo la umagukrasia, mimi simuungi mkono kabisa kabisa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa mara ya kwanza na gazeti la Mwelekeo la tarehe 4 Julai 2017.