UCHAMBUZI

La uwanachama wa CAF, Zanzibar na udhaifu wa ndani

Makala hii inazungumzia kadhia ya Zanzibar kuondolewa kwenye uwanachama wake iliokaa nao siku 128 katika Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) kwa kugusia mule makala iliyotangulia ilimopitia, yaani “Siasa za Muungano kuelekea Zanzibar”, lakini kwa hoja kuwa siasa hizo za Muungano zinafanikishwa na uadui mkubwa uliomo ndani ya Zanzibar yenyewe.

Nitapiga mfano wa namna ambavyo siasa hizi zinaposhindwa kufanya kazi muda wowote ambao uadui huo ndani ya Zanzibar umedhibitiwa, na Zanzibar ikasimama kama moja kwenye mambo fulani makhsusi.

Kwa sababu ya suala lenyewe la michezo na kwa sababu ya historia yangu kwenye sekta ya utalii na vile vile kwamba kwa muda mrefu, Zanzibar imekuwa ikiunganisha mambo haya pamoja – yaani utalii, utamaduni na michezo, mfano wangu utaanguukia hapo.

Baina ya mwaka 2001 na 2010, nilikuwa mwajiriwa wa kampuni moja ya utalii visiwani Zanzibar, nilikoanzia kama mtembezaji wageni na kupanda ngazi hadi mwakilishi wa kampuni hiyo kwenye hoteli za mashariki mwa kisiwa cha Unguja.

Mwezi Machi 2008 ulikuwa muda mwengine wa kufanyika maonesho ya kimataifa ya utalii ya Berlin, Ujerumani, maarufu kama ITB. Kampuni za utalii visiwani Zanzibar kupitia chama chao (ZATO) na kwa kushirikiana kikamilifu na kamisheni ya utalii chini ya usimamizi wa wizara yenye dhamana ya utalii, wakaamuwa kushiriki kwa mara ya kwanza wakiiwakilisha Zanzibar kama Zanzibar.

Na Mohammed Ghassani

Sababu moja kubwa kabisa ya makampuni hayo kutaka kwenda yenyewe kuitangaza nchi, ilikuwa ni ukweli kuwa kamwe Zanzibar haikuwahi kuuzwa kama Zanzibar na mamlaka ya utalii ya Tanzania Bara, ambayo hadi sasa inataka kujiaminisha kuwa ni mamlaka ya utalii ya Tanzania nzima.

Matokeo yake, Zanzibar ilikuwa inauzwa kwenye vifurushi vya safari za watalii barani Ulaya na Amerika kama sehemu tu ya mapumziko kwa wageni waliokwishatembelea mbuga za Tanzania Bara, na sio kama kituo kikuu cha utalii.

Kwa hakika, hata mamlaka za utalii za Kenya zilikuwa zikiiuza Zanzibar kwa mahadhi hayo hayo, kwa kuiunganisha na Mombasa. Hili lilimaanisha kuwa Zanzibar haikuwa ikipata fedha za kutosha, licha ya kuwa wageni walimiminika kwa wingi kwenye hoteli na fukwe zake.

Kwa kuyazingatia hayo, ndipo chini ya Amani Karume kama Rais wa Zanzibar na Samia Suluhu Hassan kama waziri wa utalii, biashara na uwekezaji, Zanzibar ikaamuwa kushiriki maonesho.

Kilichotokea kwenye maonesho yenyewe mwaka huo kilikuwa kituko cha mwaka, lakini ambacho inaonekana kilishatarajiwa na Wazanzibari. Maafisa usalama wa ubalozi wa Tanzania nchini Ujerumani ‘waliwavamia’ wasimamizi wa banda la maonesho la Zanzibar na kuwataka walivunje.

Hoja yao kubwa ni kwamba Zanzibar ni sehemu ya Tanzania na hivyo haikupaswa kujitangaza yenyewe kwenye maonesho hayo kama nchi. Kwamba kufanya hivyo kulikuwa ni kinyume na itifaki za kimataifa na hatari kwa Muungano wa Tanzania.

Kwa mujibu wa mmoja wa waliokuwepo kwenye banda hilo, maafisa hao wa usalama walifika mahala pa kukiita kitendo hicho cha Zanzibar kufunguwa banda lake kuwa ni sawa na ‘uhaini’.

Bahati mbaya kwa maafisa hao wa usalama kutoka ubalozini ni kwamba waliwakuta Wazanzibari wakiwa wamejitayarisha kwa lolote ambalo lingeliweza kutokezea, kwani banda halikuvunjwa hadi mwisho mwa maonesho yenyewe. Kikubwa ambacho wasimamizi wa banda hilo walikifanya, kilikuwa ni kuweka mabango ya Tanzania ndani ya banda lenyewe ili kufikia muafaka na maafisa usalama kuwa Zanzibar inabaki kuwa sehemu ya Tanzania, ingawa inaweza kujitangaza na kujiuza kama Zanzibar.

Lakini sinema hii haikuishia hapo. Mwaka 2010, wakati kampuni za utalii zinajitayarisha kwenda maonesho mengine ya ITB ya mwaka huu, mamlaka ya utalii ya Tanzania Bara ikatuma ujumbe wake visiwani Zanzibar kwenda kusaka suluhisho la hali iliyojitokeza hapo kabla.

Bado, ujumbe huo ulikuwa na kauli ile ile, kwamba Zanzibar haipaswi kujitangaza kama Zanzibar kwenye jukwaa hilo la kimataifa, kwamba kinachofanywa na Tanzania Bara kwenye maonesho kama hayo ni kwa ajili ya Tanzania nzima na kwamba, kwa hivyo, Zanzibar iwe sehemu tu inayowakilishwa na Tanzania Bara na siyo kujiwakilisha na kujitangaza yenyewe.

Nao pia, kama walivyokuwa wale maafisa wa usalama wa ubalozini mjini Berlin, walikuwa na kauli zinazofanana juu ya kampuni za utalii za Zanzibar “kuuhatarisha Muungano”. Baada ya kutoka kwenye Kamisheni ya Utalii, sasa ukawa wakati wa wajumbe hao kutoka Bara kukutana na wamiliki wa kampuni za utalii kwenye ukumbi wa hoteli ya Bwawani.

Inayumkinika kuwa, kutokana na tabia ya woga waliyonayo baadhi ya viongozi wa taasisi za serikali ya Zanzibar pale wanapokutana uso kwa uso na wenzao kutoka taasisi kama hizo kutokea Bara, huenda wakuu wa Kamisheni ya Utalii ya Zanzibar (siku hizo chini ya Katibu Mkuu Alhalil Mirza), hawakuwaambia wenzao wa Bara kwamba suala la Zanzibar kwenda ITB lilikuwa suala la serikali nzima ya Zanzibar na sio la ZATO tu.

Ndio maana, walipoanza maafisa kutoka Bara ilikuwa moja kwa moja kuwashambulia jamaa wa ZATO kwamba wanataka kuharibu nchi kwa kujipeleka kwao Ujerumani kama Zanzibar wakati Zanzibar ni sehemu ya Tanzania. Hili jamaa wa ZATO hawakuwacha lipite hivi hivi. Wakawaeleza kinagaubaga nini kilichopo na kipi kinapaswa kufanyika.

Kwamba, kwanza, utalii si jambo la Muungano, kwa hivyo Zanzibar haihitaji kuwakilishwa na Tanzania kwenye jambo ambalo si la Muungano; pili, hata kama lingelikuwa la Muungano, basi taasisi za Tanzania Bara sio taasisi za Jamhuri ya Muungano, kwa hivyo hazina haki ya kukiwakilisha cha Muungano, na tatu; hata banda ambalo Zanzibar hukodi kwenye ITB huwa linachangiwa kwa pamoja kati ya Kamisheni ya Utalii na ZATO, kwa hivyo hii ni hatua ya pande zote zinazohusika visiwani Zanzibar, na sio ya ZATO pekee.

Msimamo huu wa Bwawani 2010 ndio ambao umesalia hadi hivi leo, miaka minane baadaye. Zanzibar imeendelea kujiwakilisha kila mwaka kwenye maonesho hayo, na imekuwa ikijiuza yenyewe kwa njia zake.

Hadithi hii ya Zanzibar, ZATO na ITB ina mafunzo makubwa sana kwenye hii kadhia ya Zanzibar kuvuliwa uwanachama wa CAF. Inawezekana kuwa ni kweli kwamba, kwanza, CAF inatumia hoja ya kuwa nchi haiwezi kuwa mwanachama wake kama si mwanachama wa FIFA. Kwa hivyo, Zanzibar ilipaswa kwanza kuwa kwenye FIFA.

Pili, CAF na FIFA – kwa pamoja – zilimeelezwa  kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi moja tu na ambayo chombo chake cha uwakilishi kwenye soka ni Shirikisho la Soka la Tanzania Bara (TFF), na kwa kuwa mashirikisho hayo ya kimataifa humtambua mwakilishi mmoja kwa kila nchi, basi TFF aliyejipeleka kama mwakilishi wa Tanzania nzima, ndiyo keshajaza nafasi hiyo.

Kwenye utalii, hoja za waliokuwa hawakutaka Zanzibar ijiwakilishe na kujiuza yenyewe kimataifa zilikuwa zinafanana na hizi. Lakini tafauti ni kuwa uongozi wa juu wa serikali ya Zanzibar na kampuni za utalii, kwa pamoja, ulisimama imara kujenga hoja ya kipi ni kipi, na hivyo ndivyo ikawa.

Kwenye hili la soka pia, hoja ni zile zile ambazo zinaweza kutumiwa na Zanzibar, kwanza kwa mamlaka za ndani ya Zanzibar na Tanzania, kisha kwa mashirikisho hayo ya soka ya kimataifa, ukiacha mbali hoja nyengine zinazohusiana na undumilakuwili wa FIFA na CAF yenyewe kwenye suala hili la uwanachama wa Zanzibar.

Ni kweli kuwa siasa za Muungano zinataka kuiona Zanzibar ikiwa dhaifu ili kuweka mizani ya umadhubuti wa Muungano huo, lakini ni siasa dhaifu za ndani ya Zanzibar zenyewe ndizo hasa zinazoziruhusu siasa hizo za Muungano kufanikiwa.

TANBIHI: Makala hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza na gazeti la MwanaHalisi la tarehe 7 Agosti 2017.

UCHAMBUZI

La Zanzibar kufukuzwa CAF, tuangalie tulipojikwaa

Ijumaa ya tarehe 21 Julai 2017 itachukuwa muda mrefu kwangu kusahaulika. Kwenye ukurasa wa Facebook, mtumiaji mmoja alikuwa ametuma taarifa iliyoandikwa na dawati la michezo la mtandao wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) kuhusu nchi yangu, Zanzibar, kuvuliwa uwanachama wake iliokuwa imeupata siku 128 hapo kabla kwenye Shirikisho la Soka la Afrika (CAF).

Kwanza niliipita habari hiyo ghafla kama siijui, lakini kisha nikarudi kuisoma kwa kina neno kwa neno. Ilikuwa taarifa fupi na nzito. Licha ya kuwa kwangu mhariri na mtangazaji wa shirika la habari la kimataifa kwa takribani miaka saba sasa na kwamba BBC yenyewe ni shirika la habari la kimataifa, nilijikuta siiamini habari hiyo.

Nikaenda kwenye mtandao wa CAF, kisha kwenye akaunti binafsi ya Twitter ya mkuu wake, Ahmad Ahmad wa Madagascar, na mote humo sikukuta taarifa hizo. Hadi muda huo, bado kwenye mtandao wa CAF kulikuwa na bendera na jina la Zanzibar kwenye orodha ya wanachama, tena chini ya bendera na jina la Tanzania.

Hata hivyo, nikaituma tena ripoti hiyo ya BBC kwenye ukurasa wangu wa Facebook, nikiambatanisha na wasiwasi na matarajio yangu. Niliomba na kupenda ile iwe ni habari ya uzushi tu, ambayo punde ingelitamkwa kuwa si kweli.

Na Mohammed Ghassani

Siku hiyo pia, nikiwa mhariri wa zamu, nilikuwa nimefikiwa mezani pangu na habari ya wafanyakazi wa kigeni wa kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia nchini Tanzania kutakiwa kuondoka mara moja. Muda mchache baadaye, mkurugenzi wa Acacia jijini London akakanusha ripoti hiyo ya shirika la habari la Reuters, akisema kilichotokea ni kuhojiwa kwa wafanyakazi wake wawili tu, na sio kufukuzwa nchini Tanzania.

Kwa hivyo, nikawa naomba kimoyokimoyo na hii ya Zanzibar kuvuliwa uwanachama wa CAF itamkwe kuwa haikuwa ya kweli. Lakini hadi siku ya pili yake mchana, habari ilikuwa imebakia hivyo hivyo, huku wahusika wa Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) wakitajwa kutokuwa na habari ya jambo hilo. Ikimaanisha kuwa aidha hawakuwa wamearifiwa kwa taratibu rasmi au walikuwa wanadanganya. Na bado, moyoni mwangu nikawa nataka kuamini kuwa kutokuwa kwao na taarifa kunamaanisha kuwa jambo lenyewe halipo.

Sijui kama unazielewa hisia hizi, lakini mchangiaji mmoja wa ukurasa wangu wa Facebook aliniandikia faraghani akizifananisha na za mzazi aliyepotelewa na mwanawe katika mazingira ya kutatanisha. Mzazi huyu huwa haamini kuwa mwanawe hatapatikana tena. Hata kama miaka mingi itapita, bado huwa anadhani kuwa kuna siku mwanawe atarejea akiwa mzima, salama usalimini.

Ndizo hisia zangu ambazo hadi naandika makala hii, masaa 24 baada ya kupokea taarifa ya kupotea Zanzibar kutoka ramani ya CAF. Kuna kitu kinanifanya nisitake kuamini ukweli kuwa tumeshatolewa. Hisia tu.

Naam, ni hisia tu. Hisia si lazima ziwe uhalisia. Ingawa baadhi ya wakati, sadfa huzigeuza hisia zetu kuwa ukweli. Hayo ndiyo yale yaitwayo makarama. Bahati mbaya kwangu ni kuwa miye si mja wa makarama, na hivyo mara kadhaa hisia zangu hazikumbwi na rehema ya sadfa zikawa ukweli. Zanzibar yangu imeondoshwa kwenye CAF.

Huo ndio uhalisia uliopo mbele yangu na ndio ambao nitaujadili hapa, baada ya kuipata barua rasmi Rais wa Chama cha Soka cha Zanzibar, Ravia Idarus Faina, na Kaibu Katibu Mkuu wa CAF, Essam Ahmed, siku hiyo hiyo ya tarehe 21 Julai. Nitaachana kabisa na hisia zangu binafsi za mzazi aliyepotelewa na mwanawe.

Uhalisia namba moja ni kauli ya Ahmad Ahmad inayosema hivi: “Zanzibar imeondolewa kwenye uwanachama wa CAF kwa kuwa ni wanachama wa FIFA tu ndio ambao wanaweza kuwa pia wanachama wa CAF.”

Uhalisia namba mbili ni sababu ya ziada iliyomo kwenye Kifungu Na. 4(4) cha Katiba ya CAF ambacho kinalilazimisha shirikisho hilo “kukitambua chama kimoja tu cha kitaifa kwa nchi.”

Na uhalisia huo namba mbili ndio unaopigilia msumari kwenye wa namba tatu, unaosema kuwa “uwakilishi wa kitaifa uliopo sasa unaotambuliwa na FIFA na CAF ni ule wa Shirikisho la Soka la Tanzania.” Hapo anakusudia Shirikisho la Soka la Tanzania Bara (TFF).

Huo ndio uhalisia uliopo kwenye uamuzi wa CAF iliyokutana Rabat, Morocco, na kuiondolea Zanzibar uwanachama wake ilioupata tarehe 16 Machi 2017 mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Sasa tuje kwenye uchambuzi wa uhalisia huu, kuangalia ambapo sisi Wazanzibari tulijikwaa na sio tulipoangukia.

Ukweli ni kwamba vyombo vya kimataifa vinaitambua Tanganyika (ninaiita Tanganyika kwa makusudi, maana ushahidi unathibitisha kuwa ndiyo inayojiwakilisha kama Jamhuri ya Muungano wa Tanzania). Ukweli huu ndilo jinamizi kubwa kwenye nafasi, maslahi na taswira ya Zanzibar ndani na nje ya mipaka yetu, maana siasa ya Tanganyika nje ya mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuelekea Zanzibar ni muakisiko tu wa siasa yake ya ndani.

Nimeandika mara kadhaa – na daima nitaandika hivi hivi madhali hakuna kilichobadilika – kwamba Tanganyika inaamini kwa dhati kwamba ukitaka kuwa na Muungano imara (soma Tanganyika imara), basi lazima uwe na Zanzibar dhaifu. Kinyume chake ni kuwa unapokuwa na Zanzibar imara, basi ujikubalishe kuwa na Tanganyika (Muungano) dhaifu. Huu ni ukweli mchungu, lakini ndio uhalisia ulivyo.

Na wala hili jambo halijaanza leo kwenye la uwanachama wa CAF tu. Limekuwa hivyo ndani ya hii inayoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na limekuwa hivyo pia nje yake. Chimbuko lake lilianzia hata mwezi mmoja haujatimia tangu kuwekwa saini kwa Makubaliano ya Muungano, pale Mwalimu Julius Nyerere alipoanza kuipopotowa Zanzibar nguvu zake kwa kutunga sheria ya kuzibatiza jina la Muungano shughuli zote za Tanganyika ambazo hazikuwa katika yale Mambo 11 ya Muungano, tunayoambiwa walikubaliana na Mzee Abeid Karume.

Kati ya sheria hizi ni ile iliyoitwa The Transitional Provision Decree (N0. 1) ya mwaka 1964, ambayo iliwapa uhamisho wafanyakazi wote wa serikali ya Tangayika na kuwa wa serikali ya Muungano. Kwa sheria hii, iliyochapishwa kwenye Gazeti Rasmi la Serikali la tarehe 1 Mei 1964, ndipo taasisi kama vile Mahkama Kuu ya Tanganyika zilipogeuka kuwa Mahkama Kuu ya Tanzania.

Kisha wiki mbili tu baada ya hapo, yaani tarehe 15 Mei 1964, akachapisha sheria nyengine iliyoitwa The Transitional Provision Decree (No. 2) iliyoelekeza kuwa “kila pale penye neno au kumbukumbu inayosomeka Tanganyika sasa pasomeke Serikali ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.”

Kwa hivyo, hata lile agizo lililokuwemo katika Katiba ya Muda kwamba “Tanganyika and Zanzibar are one United Sovereign State” baadaye likaja kubadilika na sasa ikawa “Tanzania is one State and is a Sovereign United Republic”, ambayo ndiyo iliyomo hadi sasa, na ndiyo inayotumika kuifanya Zanzibar isiwe na chake mbele ya jumuiya za kimataifa, hata kama ushirikiano wa kimataifa si jambo la Muungano.

Kwa kutumia mwanya huu, kila kitu cha Zanzibar kinakuwa kimsingi na kiutekezaji ni cha Tanganyika kwa jina la Muungano, hata kama kijuujuu kitasemwa na kuoneshwa kinyume chake. Vyote na chochote cha Zanzibar si chake.

Ndio maana ukaona, kwa mfano, Rais wa Jamhuri ya Muungano anaunda wizara zake, kisha anachanganya mambo yasiyokuwa ya Muungano na ya Muungano kwenye wizara moja, kama hilo la Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kimataifa na Masuala ya Afrika Mashariki, ambamo ndani yake ni Mambo ya Nje tu lililo la Muungano. Ndivyo pia ilivyo pia kwa Wizara ya Mambo ya Muungano na Mazingira, Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia, na kadhaa wa kadha.

Anaweza pia kuunda wizara isiyohusiana kabisa na Mambo ya Muungano na ambayo, kwa hivyo kimsingi inakuwa ya Tanzania Bara tu, lakini akamteuwa Mzanzibari kuwa waziri, kama vile Dk. Hussein Mwinyi alivyowahi kuwa waziri wa afya na sasa Profesa Makame Mbarawa alivyo waziri wa ujenzi.

Kizungumkuti hiki hakifanywi kwa bahati mbaya. Kipo kwa makusudi, maana kwa jicho la ndani la Dodoma ni kwamba kuna nchi moja tu, kuna serikali moja tu na kuna chama kimoja tu. Hii ndiyo falsafa ya mwasisi wa huo unaoitwa Muungano wenyewe, Mwalimu Nyerere, na ambayo inatekelezwa kivitendo na wafuasi wake, miongoni mwa Watanganyika na miongoni mwa Wazanzibari pia.

Kwa hivyo, kwenye hili la CAF, tulipojikwaa sisi Wazanzibari tunaotaka kuiona nchi yetu ikisimama kwa miguu yake yenyewe kwenye mambo yake yote yasiyokuwa ya Muungano, sio kwenye kiherehere chetu cha kujipeleka CAF kabla ya kutoka FIFA, kama inavyojieleza barua ya kufukuzwa kwetu, bali ni kwenye kutokulimaliza kwanza lililosababisha kila chetu kikawa si chetu wenyewe – kutolimaliza la siasa za Muungano kuelekea nchi yetu.

Kama kweli tunataka kuiona Zanzibar ikiwa mwanachama wa jumuiya yoyote ya kimataifa, kama kweli tunataka kuiona Zanzibar ikisimama kwenye mambo yake yote yasiyo ya Muungano, tunapaswa kwanza kukimaliza kizungumkuti kilichomo kwenye Muungano wenyewe. Je, tuko tayari?