KISWAHILI KINA WENYEWE

Hajuti Anosubiri

Si jipya nilinenalo, lilishanenwa dahari
Mote linanenwa lilo, na miye nalikariri
Jambo nikushaurilo, hupaswi kulighairi
Subiri akhi subiri
Kwamba kila lianzalo
Ndilo pia liishalo

Hakuna aliyejuta, kwa kuwa alisubiri
Hakuna aliyepata, kwa papatu na kikiri
Na kila anotafuta, hutafuta na saburi
Akhi na wewe subiri
Kushavyoanza nyonyota
Upandacho kitaota

Wala hupotezi kitu, akhi yangu ‘kisubiri
Wala hutakera mtu, moyowo ‘kiusitiri
Subira ni utu wetu, tumeumbwa kusubiri
Subiri akhi subiri
Kilokwenda jana yetu
Kitarudi kesho yetu

Nyuki asaliye tamu, ela yuna misumari
Na mkate wa ajemu, una joto la tanuri
Kupata haya lazimu, kuteswa uwe tayari
Tumai akhi subiri
Ndivyo kibinaadamu
Mwisho wa chungu ni tamu

Hu wa mwanzo kukupata, wala huwi wa akhiri
Yewapata walopita, na wajao yatajiri
Na wao hawakujuta, sababu walisubiri
Subira nawe subiri
Wasubirio hupata
Kama wanavyotafuta

‘Tasema nikirudia, sababu hii si siri
Hikuona ‘takwambia, na hata ukisafiri
Salamu ‘takutumia, na daima ‘tadhukuri
Wasia wangu subiri
Subiria kwa lolote
Uone mwisho wa yote

Mohammed K. Ghassani
Septemba 2000
Zanzibar

 

1 thought on “Hajuti Anosubiri”

  1. Nashukuru kaka Kwa kazi nzuri. Kila la heri katika mwaka wa 2016

    Mosol Kandagor Chuo Kikuu cha moi Kenya

    Sent from my iPhone

    >

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Twitter picture

You are commenting using your Twitter account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.