Mama mimi ni mwanao, kwa hili hakuna shaka
Juu hako zaidio, ila Muumba Rabbuka
Yeye ndio mwenye cheo, kisha wewe kakuweka
Mbele yako nimefika, kuitii amriyo
Sema lako kusudio, amri nipate shika
‘Taitenda mbio mbio, uone kweli nataka
Japo ina zuilio, lisomuudhi Rabbuka
‘Tatenda huku nacheka, kwa hamu na kusudio
Sema nipate radhio, kesho nisijeteseka
Itapotoka rohoyo, na kwenda kupumzika
Nisijelia kilio, hashindwa kunyamazika
Nawe kuwa kushafika, huko kuso marejeo
Mama wewe kimbilio, la furaha na fanaka
Kwani wakati wa leo, hapati mtu hakika
Kuwa na mapendeleo, faida na kadhalika
Hata akihangaika, hapati ayatakayo.
Said O. Shoka,
16 Aprili 2015,
Zanzibar