KISWAHILI KINA WENYEWE

Donda Bichi Nsumari Mmoto

Nilitoka ni mzima, nenda na safari zangu
Hadi njiani hakwama, kwa kudra zake mungu
Jimwiba lilinichoma, ukagwaya mwili wangu

Nerudishwa kwa vitanga, wenibeba walimwengu
Tumboni nafungwa kanga, nimudu pumzi zangu
Uso wangu umefinga, yamenijaa matungu

Watu wakakusanyika,wa tele nyumbani mwangu
Wakaanza hangaika, kunitibu donda langu
Wote wanahuzunika, nilikavyo mlimwengu

Wakakutana wavyele, wambali na majirani
Zikamiminika pole, lukuki wa milioni
Maumivu pale pale, utasema hayaoni

Donda limenichanganya, kutwa ninahangaika
Kila mara nalibinya, ati napunguza taka
Nalo bado lanyekenya, mimaji latiririka

Lipatiwe dawa gani donda lipate tibika!
Wa dua, wa qur-ani, wa makombe kuandika
Wa vidonge, wa majani, dawa zote metumika

Donda limekuwa sugu, sili, siogi, silali
Donda lafanya vurugu, lanitwika idhilali
Na vinzi na vinyigu, vyaidadisi ajali

Kiumizacho zaidi, donda lisitake pona
Vinzi vimeshitadi, kutwa kucha walin’gon’ga
Vinaniumiza hadi, ila sina la kufanya

Waganga na waganguzi, hawatambui kulala
Magwiji na wanagenzi, wanaiona thaqala
Yakapangwa maamuzi, ije tiba mbadala
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto!!

Wa mbadala kungia, donda wakalichunguza
Haraka wakachupia, chuma kwenda kuunguza
Tiba waliyoamua, vidudu kuangamiza
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

“Tuviunguze vidudu, donda vinolitafuna
Mana vyaleta vurugu, na donda halitapona
Vikipata vuguvugu, uhai hivi havina”
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

Donda lilivyoshamiri, maumivu mesharabu
Libichi lichirichiri, lanyekenya, lajilabu
Hatiwa moto sumari, ati tiba mjarrabu
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

Sumari moshi lafuka, kwenye donda likatiwa
Donda lilivyochemka, wamba kwapwazwa maziwa
Na huku wao wacheka, “sasa donda litapoa”
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

Vidudu vyaangamizwa, donda visiliadhibu
Kumbe huku naumizwa, maumivu ya ajabu
Kwa kweli ningesikizwa, ‘ngegomea matibabu
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

Sumari linalowaka, nimeshachomwa dondani
Na maumivu hakika, bado yapo si utani
Mbele ya watu nacheka, wanone ni afwani
Ni tiba ya donda bichi kutiwa sumari moto

Donda hili kutibika, si rahisi asilani
Kila saa na dakika, natonesheka kwa ndani
Nje hukaa hacheka, halia nikiwa ndani

Donda tatizole kuu, ni mwiba uliongia
Mwiba wa nyenga mkuu, alopea na kupea
Na sitapata nafuu, kwa namna ulivyongia

Ulichoma ukapinda, ukakaa kama lamu
Kijipande kikaganda, kwenye mshipa wa damu
Ndiyo mana hili donda, kupona haswa ni ngumu

Na kwa tiba ya sumari, nazidi kuteketea
Sumari l-ahmari, kwa moto ‘livyokolea
Nachokorwa kwirikwiri, naona naangamia

Dawa ni kumshukuru, mola wa hii dunia
Kuleta stighfaru, nisije nikapotea
Hii ni yake qadaru, aliyonichagulia

Alhamdulillah, Alhamdulillah, Alhamdulillah

Astaghfirullah, Astaghfirullah, Astaghfirullah

Allahumma ajirnii fii muswiibaty, wakhluf lii khayran minhaa…

Salma Hamad

21 Machi 2013

Zanzibar

1 thought on “Donda Bichi Nsumari Mmoto”

  1. Huruma nakuonea. Ila la kufanya sina
    Juhudi meziendea. Donda kutaka lipona
    Dawa zote metumia. Hadi dua kwa rabbana

    Ila lililobakia. Usiache kutafuta
    Tiba kuziulizia. Huenda ukaja pata
    Ingawa yako kadhia.tiba zote umepita

    Usijekata tamaa. Kimya ukajikalia
    Hakuna mbaya kadhi. Kwa mola ikakomaa
    Maradhi tuliletewa. Meambatanishwa na dawa

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.