KISWAHILI KINA WENYEWE

Kituko cha Mwaka Mpya

Nealikwa watuningwa, kwenda kusherehekea
Sherehe ya mwaka mpya, huu ulioingia
Hafikwa ni ya kufikwa, hapa tawasimulia

Kwewa na kila namna, ya vyakula na kunywiwa
Vya Kizungu na Kichina, vya kuchotwa na kubwiwa
Nikala bila khiyana, nikashiba havimbiwa

Kituko kikaja tuka, pale tulipoambiwa
Ifikapo saa sita, kinywaji tutapatiwa
Kinywaji kisicho shaka, si kilevi haambiwa

Ingawa newa na shaka, kuamini haamuwa
Kwa kuwa alonalika, ni mtu namuelewa
Kiovu hawezi nipa, hathubutupo najua

Moyo ukaja nirapa, shampeni kugunduwa
Nikajawa ni wahaka, ela siweze kimbia
Saa sita ikafika, chupa tukasogezewa

Huku nje kwaalika, fashfashi zin’jaa
Kinywaji chamiminika, gilasini kwa madaha
Chan’gara chameremeta, bilauri haitwaa

Kwa shaka na kuogopa, ndogo ndogo hachubuwa
Kinywaji kikanipata, hajiona nanogewa
Nikanywa bila kusita, gilasi haikubwia

Bada kitambo kupita, domo likaanza pwaya
Mipweso napwesa pwesa, macho siwezi fumbuwa
Mara macho yarembusha, kwa juu yalewalewa

Mwenyeji namtafuta, aje nipate mwambiya
Haya yaliyonikuta, apate nisaidiya
Niaminivyo naota, au jamaa nshalewa?

Hamad Hamad
1 Januari 2013
Copenhagen

2 thoughts on “Kituko cha Mwaka Mpya”

  1. Kake weye kunlewa kushalewa muungwana
    usije ukanogewa ukaja kulewa tena
    Ila utasamehewa ukimuomba rabana.

    Weonaje kake yangu mvinyo ulipopiga
    Hivi ladhaye ni chungu au ni kama ya togwa
    wepatikana mwezangu wazungu walikutega

    kake usionje tena tutenda kunywa peponi
    ladha za kila namna na Mahur l Eini
    kake ukionja tena hwendikunywa wa peponi
    Nakwambia kabisaaaa!

  2. Ndugu yangu kunlewa, pole kwa kujisifia.
    Wenzako washakuoa, ndivyo walivyozoea.
    Jua washakubirua, bilisi achekelea.
    Na nguo washakuvua, wenyewe kujilipia.

    Walikutaka zamani, kukwambia ni vigumu.
    Uliona ihsani, kukupa vilo vitamu.
    Watu hawana imani, kote wameshakuchumu.
    Washakutia chumbani, na kuja zamu kwa zamu.

    Ulifataje ya watu, ewe mpemba mwenzangu.
    Umesahau ya kwetu, ya Wete na ya Madugu.
    Mwaka mpya si wa kwetu, tuwaachie wazungu.
    Sisi tunao wa kwetu, alotupangia Mungu.

    Uliona shampeni, kwa nini ulijinywea?
    Ukajifanya muhuni, ushamba kuukimibia.
    Sasa mavi yako chini, na yai ushabanjiwa.
    Lawama zende kwa nani? mwenyewe wejitakia.

    Wajidanganya ni ndoto, kujifanya hufahamu.
    Na kutufanya watoto, tuna akili timamu.
    Wewe sasa ni mtoto, kwa ulowapa utamu.
    Na huna hata majuto, wahadithi bila gamu.

    Weacha ya kuhadithi, wasimulia ya pombe.
    Hayo ndo tuloyarithi?, kwa wavyele na vikongwe?
    Usijitie nuhusi, maisha usiyazonge
    Sisi kwetu ni matusi, kuvishiriki vigenge.

    Kwanini sishereheke, kwa mwaka wa hijiria?
    Naamini siku yake, pengine hukuijua.
    Hujui maana yake, hata ilivyoanzia.
    Hala hala ewe kake, pole kwa kutojijua.

    Tambua sipo ulipo, wafanya usoyajua
    Usifuate upepo, ukazidi kupotea
    Tubia hapo ulipo, Allah anakungojea.
    Akulipe yake pepo, jirani na manabia.

    By: Al’Rumhy.

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Twitter picture

You are commenting using your Twitter account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.