KISWAHILI KINA WENYEWE

Watu Wane

Kuna yule ajuae, na ajua yuajua
Tatizo mpelekee, lolote atatatua
Yuajijua mwenyewe, kwamba yeye yuajua
Kuwa karibu na yeye, elimuye kuchukua

Mwengine ni ajuae, na hajui yuajua
Elimu i tele naye, hana asichokijua
Ela aonavyo yeye, yu juha wa kurembewa
Huyu na ashituliwe, hadhi yake kuijua

Na kuna asiyejua, na ajijua hajui
Mambongwa huyakimbia, watuni yeye hakai
Adhara aichelea, kuja tolewa nishai
Huyu si wa kuzomewa, ni wa kufunzwa kwa rai

Wa nne ni asojua, na hajijui hajui
’kiitwa kuhutubia, himahima hakatai
Maringo kujisifia, yukajifanya nabii
Huyu ni kushushuliwa, yukaambiwa hajui

Wa kwanza ni ajue, akajua yuajua
Wa pili ni ajuae, na asijue ajua
Wa tatu ni asojua, akajijua hajui
Wa nne ni asojua, yusijijue hajui

Hamad Hamad
25 Disemba 2012
Copenhagen

1 thought on “Watu Wane”

  1. Wako wengi wanojua, wenyewe hujifahamu.
    Hao mengi huyajua, yeyote humuheshimu.
    Popote hujitambua, huongozwa na elimu.

    Mwengine nae hujua, bila ya kujifahamu.
    Yale anayoyajua, yote ni mambo muhimu.
    Aje wa kumzindua, watu wachote elimu.

    Wa tatu ni asojua, mwenyewe hujifahamu.
    Hupenda nae kujua, tena kwa zote nidhamu.
    Yafaa kumpokea, kumpa yenu elimu.

    Wa mwisho ni asojua, na kujiona Mwalimu.
    Hana analolijua hata, kushika kalamu.
    Huyu huungua jua, sawa na mwendawazimu.

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.