KISWAHILI KINA WENYEWE

Uchawini Kuna Mambo

Habari za uchawini ndotoni zilinijia
Kubwa zisizo kifani ndugu yangu nakwambia
Ndugu yangu wa imani nawe nakudokezea
Uchawini kuna mambo!

Wachawi mahayawani tena ni watu wabaya
Hawana chembe imani na wala hawana haya
Matendo ya kishetani ndiyo waliozowea
Uchawini kuna mambo!

Hawamuogopi Mungu wachawi nakuambia
Wanaua kwa marungu mapanga na majambia
Hata uone uchungu mwiko kukuhurumia
Uchawini kuna mambo!

Mtu huchinjwa shingoni kisu kikamuingia
Damu yaruka hewani wengine washangiria
Si hadithi za kubuni ni mambo yanatokea
Uchawini kuna mambo!

Wanacheza ngoma zao kama walivyozaliwa
Watoto na mama zao wakwe na shemegi pia
Zaimeruka nyuso zao haya zimewapotea
Uchawini kuna mambo!

Suleiman Hakum

16 Disemba 2012

Zanzibar

12 thoughts on “Uchawini Kuna Mambo”

  1. Ya mchawi huyaoni kama na wewe hujawa
    ndugu yetu selemani mbona unatushtuwa
    kama kweli ni ndotoni radhi zako tapewa
    Uchawini nawe umo?

  2. Lo! kake mie simo simo mie uchawini
    Siningize kwenye shimo la wenyeji wa motoni
    kama huamini simo naweza kula yamini
    uchawini mie simo.

  3. Nami nimepata shaka,maneno ulotwambia,
    Umeningia wahaka,sijui pakuanzia,
    Kwa jina sinamashaka,na njema yako tabia,
    lakini sijaridhika,vipi weyajuwa haya?

  4. Somo kwani nawe umo, He tuweke bayana
    Ungalimo kwenye shimo, Tueleze kwa mapana
    Uchawi kwani ni shimo, Lilo refu tena pana
    Tuwekaneni Bayana.

    1. Taireni taireni , mbona mwanielemea
      Hayo mambo ya ndotoni , si nilishawambia
      Mimi simo uchawini , ndugu zangu nawambia
      Uchawini mie simo

    2. Seleman hana kosa. Hili aliloongea
      Ni wangapi ‘mewakosa. Rafiki zeti wekuwa
      Wachawi wakajitosa. Nyama wakenda jilia

      Wangapi mechuliwa. Kisha kwetu kurejea
      Lengo lao kuwatowa. Vituko kuwafanyia
      Kisha tunahadithiwa. Ya huko yanotokea

      Jamani seleni yuko sawaaaaaaaaaaa

  5. Wa Hakumu nakwelewa, ndoto liyojiotea,
    Wachawi twavyoambiwa, ndotoni wanatujia,
    Warambisha, wakwangiwa, waburuzwa jionea,
    Kwavyo siyo yako hoja!

    Pamoja kutwaambia, ndotoni mejionea,
    Sisi twaona vioja, kamwe haiwezi kua,
    Uote bila ya haja, lazima wejiendea,
    Twambe kama ushingia!

    1. Wallahi sijaingia , naona mwanionea
      mbona mnanichangia , kutaka kuniumbua
      ndoto ilyonijia , nikosa kuwaambia
      Sina nia ya kungia

      1. Haya uliyoeleza. Seleman uko sawa
        Hawa wanaokubeza. Juwa hawjaelewa
        Mwanzo ulipolianza. Shairi kulitohowa

        Tukatae tukubali. Jamani uchawi upo
        Hili nasema ukweli.tena nakula kiapo
        Tena una mafahali.popote pale wendapo
        Alonena selemani. Hakika hajakosea
        Naomba muyaamini.’Singizini lomjia
        Habari za uchawini. Mitaani ‘meenea

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.