Hii si mara ya kwanza kuzungumzia kundi hili la majina. Naamini ni kundi lenye mitego ni ghiliba nyingi zaidi, hata kwa watumiaji wa siku nyingi wa lugha ya Kiswahili. Na hii – ninavyodhani – inatokana na maumbile yake. Kwamba yote wingi wake unaanza na herufi au sauti ‘m(a)-‘.
Angalia mifano hii:
- Jino – Meno
- SIkio – Masikio
- Ini – Maini
- Jiwe – Mawe
- Daftari – Madaftari
Mifano yote hiyo hapo juu inaufanya wingi wa majina yote hayo kuanza na herufi au sauti ‘m(a)’. Lakini huo ni wingi tu, ambao licha ya kueleza urahisi wa kundi la majina la LI-YA. Mtego huo uko kwenye umoja wa majina yaliyomo kwenye kundi hili, ambapo kimakosa mtumiaji wa lugha huweza kubadilisha kila wingi kuwa umoja, kama vile ambavyo anadhani kila umoja na wingi.
Huko nyuma niliwahi kupiga mfano wa matumizi yaliyo siyo ya maneno kama vile mahitaji au madhumuni, ambapo watumiaji hao ninaowazungumzia hapa, hulazimisha umoja wake, na basi wakasema ‘hitaji’ na ‘dhumuni’.
Leo nimekumbana na mtumiaji mwengine wa lugha wa siku nyingi anayesema umoja wa ‘matakwa’ ni ‘takwa’, kwa kuwa tu anaamini kila chenye wingi, basi kilikuwa na umoja. Kiswahili, kama zilivyo lugha nyengine, kina pia aina za maneno ambazo hazifuati taratibu za kawaida. Kwenye kundi hili la LI-YA, maneno kama matakwa, madhumuni, maji, na mashambulizi – nikitaja mifano michache – ni maneno yasiyo na umoja, ingawa kwenye matumizi huja na wingi.
Hatusemi “takwa lake limetimizwa” bali “matakwa yake yametimizwa” hata kama huyo tunayemzungumzia alikuwa amedai kufanyika kwa jambo moja tu, na siyo mawili au zaidi.
Ni hayo kwa leo.
Nimeipenda hii