KISWAHILI KINA WENYEWE

Fukara Thamani Hana

Fukara hathaminiki, wahenga walishasema
Na wala hatambuliki, itapokuja neema
Kutwa yupo kwenye dhiki, hajui yake khatima
Tatizo yeye fukara

Watapendana kwa dhati, moyoni watashibana
Watapanga mikakati, na ahadi kupeana
Wazazi hawalitaki, ugomvi watashindana
Fukara hathaminiki

Atajawa na busara, hekima tele kichwani
Kulitoa lilo jema, kueleza hadharani
Hata hawatolipima, ni kwa faida ya nani
Fukara hana sauti

Hata kama ni sheria, fukara ndo kosa lake
Watakaa kuamua, kumnyima haki yake
Hana pa kukimbilia, abaki ahangaike
Fukara hatambuliki

Na hata akiokota, fukara huwa kaiba
Ni wapi atapopata, njia zake ukiziba?
Kakosa pa kukamata, ufukara ni msiba
Fukara yupo tabuni

Hata akifanya nini, fukara yupo tabuni
Hajui leo ni lini, kutwa kucha mashakani
Hujui yu furahani, ama yupo msibani
Fukara hatambuliki

Suleiman Mkubwa (Tajiri wa Ushauri)
27 Disemba 2011
Zanzibar

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.