KISWAHILI KINA WENYEWE

Si La Ushoga Pekee

Kauli ‘liwashangaza, wakashangaa
Kameruni kutangaza, atakataa
Misaada ‘noagiza, kutuletea
Tanzania ikiwemo!

Kauli ‘lipotongoa, ‘kaianika,
Dunia ikasikia, ikagutuka
Madola ya Jumuia, ‘taadhibika
‘Kiukataa ushoga!

Mara wakajiinua, huku wang’aka
Viongozi ‘katongoa, ‘mekasirika
Wote wataoingia, ‘kajumuika
Ushogani ‘taumia!

Kwa ujuba na jeuri, wakatamka
Misada wahiyari, ikakatika
Na tena tuko tayari, njaa tukifa
Ela hatwebu ushoga!

Lakini ajabu yetu, inayotisha
Hivino vitendo vyetu, vyaogopesha
Viovu visivyo utu, unyama kwisha
Ila haya tweyajua?!

Siipingi Serikali, gamba kuvua
Kwa mdomowe mkali, kupapatua
Walakini ni muhali, kukubalia
Kwetu tukawaamini!

Umalaya hivi sasa, ‘meimarika
Ulevi ndio kabisa, ‘mezoeleka
Ulawiti watikisa, umetushika
Kipi mtatudanganya!?

Madanguro yamo mote, ‘mesajiliwa
Nanyi mwayajua yote, mwayatumia
La Kameruni ni tete, mwatuambia
Unafiki ni wa nini!?

Kama kweli mwayakana, ‘liyoeleza
Ya kwamba ni ya fitina, kuileteza
Mwashindwani hizi lana, kutokomeza?
Mwaja mukitudanganya!

Huo utayari wenu, u wapi sasa?
Hiyo mijineno yenu, umbo tasa
Sababu vitendo vyenu, vinawasusa
Ta’ lini ‘tatudanganya?

Othman Ali Haji
02 Disemba 2011
Zanzibar

2 thoughts on “Si La Ushoga Pekee”

  1. Ewe Ochu sikiliza, nilinenalo
    kula linopatiliza, likanye hilo
    yule anotekeleza, msuse nalo
    Mbawa zinyonyowe

    Wahenga watueleza, bila utata
    kuchukia ni kuanza, kupiga vita
    msitu kuteketeza, chechea ndo stata
    hata maji machafu yazima moto!

    Uovu auonaye, auondoe
    Mikono aitumiye, athari isibake
    ulimi ashambuliye, au achukie
    Elfu huanza na moja

    Alofanya jitihada, ‘simdharau
    hakuna kiso faida, japo kichunguu
    piopio ndio ada, alovunjika mguu
    alothubutu si kama alogugumia

  2. Nesikiya unenayo, e kijana Ahmedi,
    Wanona nekoseyayo, kutoutamba weledi,
    Negeuka mpitayo, kela kitu nihasidi,
    Na sasa wataka jibu!

    Sikia nonena kwako, nakwamba uwe shahidi,
    Nti hii walo wako, na wezazi wa shadidi,
    Wevita wapiganako, mema kuzidi shadidi,
    Na leo twayona yayo!

    Maadili yaloyepo, na adili ilozidi,
    Ushuwari wa upepo, rehema Mola ‘lozidi,
    Yeharibiwa kwa upo, nao wetenda kusudi,
    Sasa leo twewa wapi?

    Si kama niliyakana, waloyao ya usudi,
    Neyasifu niyaona, ni mema yenye kusudi,
    Tena yafaa kuyona, kwetu yawe ni waridi,
    Ela wakweli kivitendo?

    Kama ni wakweli sasa, waanze kuyahusudi,
    Mabaa, zinaa sasa, wazondoe kwa kusudi,
    Ulawiti wanoasa, waadhibiwe khuludi,
    Tena iwe kwa vitendo!

    Maneno walotongoa, hayatafawa abadi,
    Kama hawatajandaa, kuyondoa asilidi,
    Tena wajona wafaa, vitendo wavihasidi,
    Tuseme wekusudiya?

    Othman Ali Haji.
    03/01/2012,
    Zanzibar.

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Twitter picture

You are commenting using your Twitter account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.