Mwapenda mafanikio, kazi kwenu ni laana
Mwaweka matumanio, ndoto zenu za mchana
Utajiri kujiotea:
“Kesho ‘tawa milionea”
Mwajidanganya!
Mwatakangia Peponi, ela kifo mwakikana!
Mwachekesha!!
Mnapenda ubwanyenye, na kiburi kufatana
Alo chini mumkanye, mtumikiwe ne wana
“Ni mimi mwanafulani
Shepu ya kazi siyoni”
Mwaajabisha!
Mwautaka utukufu, kwa kuliangaza jua?
Mwachekesha!!
Mwavipenda vibaraza, vidole kuoneshana
Majungu mwajiapiza, husuda kuoneana
“Bora mimi ni fulani
Yeye ana hadhi gani!?”
Mwasikitisha!
Mnathamini maneno, njaa inawasakama!
Mwachekesha!!
Maendeleo yaliyopo, japo kwa duni maana
Mwayaharibu kwa upo, na mawe kuongozana
“Chama chake ni fulani
Na changu hatuwiyani”
Mwastaajabisha!
Mwaukana Muungano, siasa yakutengeni!
Mwachekesha!!
Dhamana mkwewazo, muishi thaminiana
Ubinafsi mjayazo, tamaa kuungamana
“Wacha nichukue changu
Nawaumie wenzangu!”
Mwahuzunisha!
Mwatamani endelea, kwa ndoto ziotelea!
Mwachekesha!!
Othman Ali Haji,
25/11/2011
Zanzibar