KISWAHILI KINA WENYEWE

Siyagawi Kama Njugu

Mapenzi kitu azizi, katujalia Manani
Mapenzi yatoka enzi,si ya leo duniani
Mapenzi ni ya Mwenyezi, kashusha kwa insani
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

Wakupenda nachagua, si kama kila mmoja
Napenda alotulia, nikiona ipo haja
Sipendi viruka njia, ninaogopa viroja
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia
Wasichana wapo wengi, wanaojipendekeza
Wengine ni mashangingi, nahofu kunipoteza
Nina mambo ya msingi, kwanza ninayachunguza
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

 
Simapembe pendo langu, kila mmoja apate
Nibasmati ya tangu, hailiwi na watu wote
Huliwa na wenye fungu, sio wewe patasote
Siligawi kama njugu, pendo langu mawambia

 
Napenda wenye nidhamu, ‘lofunzwa akafunzika
Na walo wataalamu, kiwa ndani huna shaka
Kwani hao ni walimu, kwa mapenzi ni hakika
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

 
Hupenda wanaotunza, mambo yao ya nyumbani
Marufuku kutangaza, yafanyikayo chumbani
Sio kuihanikiza, kwa shoga na majirani
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

 
Yule atakayefika, kuwa mimi nimpende
Basi amebahatika, bahatiye ya mtende
Jangwani wanawirika, miti mingine isende
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

 
Kipenda napenda kweli, wala sifanyi utani
Pendo langu ni asali, tamu isiyo kifani
Lakini ni mbakhili, siligawii njiani
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

 
Wale wananyemelea, walipate langu penzi
Samahani nawambia, kwa sasa nina mpenzi
Huyo ndo anonilea, anienzi namuenzi
Siligawi kama njugu, pendo langu nawambia

Mzee Haji (Sir Haji)
24 Novemba 2011

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Twitter picture

You are commenting using your Twitter account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.