KISWAHILI KINA WENYEWE

Sekufa Niliuliwa!

Chini ya mkondo huu, nipo bado nateseka
Wao wameshasahau, huku walikoniweka
Kwa uzembe na dharau, ndipo haya yakatuka
Takwenda mwambia Mungu, sekufa niliuliwa

Ndivyo nitakavyosema, sekufa niliuliwa
Walijuwa lenda zama, kwani hawelizuwia?
Kama wejua si zima, kwani likaruhusiwa?
Sekufa niliuliwa, ndivyo Mungu tamwambia

Hii si mara ya kwanza, kwa Mungu tenda shitaki
Hii ni kuendeleza, walianza kwa bunduki
Ela hawenimaliza, wakaona haitoshi
Mungu takwenda mwambia, sekufa waliniuwa

Tasema yote hiwahi, kwa Mola wetu muweza
Tayasema ya Fatihi, walivyoniangamiza
Mbele ya zao nyajihi, nikafa wakinichunza
Sijafapo tenda sema, daima nehiuliwa

Sekufa waliniuwa, kwa kutaka na kusudi
Kisha wakatangazia, ‘kasema ndio ahadi
Hakuna alofidiwa, si ubani si kwa udi
Mungu takwenda mwambia, sekufa wanniua

Kifo changu kilijiri, kuwa kwao ni dhihaka
Wakaonesha viburi, hawetaka wajibika
Wakafichiana siri, hakuna aliyen’goka
Mungu yote wayajua, lakini taja yasema

Walipokwisha niua, changi wakazidiriki
Ati kuwasaidia, wale waliowabaki
Kwani hawewapatia, meli ilo madhubuti?
Ela hilo halitawa, waketaka nighariki

Ati waliunda timu, ya ajali kuchunguza
Wale wote mahkumu, ndio wakaiongoza
Vipi wangejihukumu, adala kuifanyiza?
Mola mie neuliwa, sekufa wanniua

Nipo chini ya bahari, nasubiri malaika
Wao watanisitiri, kama nyie hamwetaka
Ni sitara ya Qahari, sitara iso chafuka
Tubuni nawashauri, kabla siku kufika

Siku ya kwenda ungama, nenda simama hifika
Hawataje kwa majina, nyote muliohusika
Mulonacha hasakama, huku kusiko kalika
Rabi mjao sekufa, madhulumu neuliwa.

 
Hamad Hamad
September 25, 2011
Copenhagen

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Twitter picture

You are commenting using your Twitter account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.