Kwa jinalo Rahmani, Mola wetu Msifika
Naomba uniauni, kwa hili ninalotaka
Naingia utungoni, mchango wangu kuweka
Unipe njema lisani, mazuri kuyatamka
Utamu wake shairi, si betize kupangika
Si vina na misitari, kama inavyodhanika
Wala si kwa umahiri, wa maneno kurapuka
Tamuye ni kudhukuri, maneno yenye mipaka
Si tu mtiririko wake, wa fani na maudhui
Vifanyavyo tusimkwe, tuwe hatujitambui
Na vicheko tuvicheke, tuloambwa hatujui
Hiyo siyo tamu yake, tungoni inovutiya!
Utamuwe si wa fumbo, kwa watu kuwafumbika
Wala utata wa tungo, usoweza eleweka
Ya kweli na ya uongo, tungoni ukayaweka
Si tamuye asilani, tungoni inovutia
Hasa ladhaye shairi, ni tungo za umakini
Si tungo za ki urari, wa vina wala mizani
Ni tungo zilo sheheni, mazuri yaliyo ndani
Na iwe mantikiye, kuadilisha jamia
Ladhaye siyo ya nyimbo, ya sauti kuighani
Kuitilia mapambo, na sherehe uwanjani
Lazima uwe na jambo, la kuweka hadhirani
Ili wajifunze kwalo, watakaolisikia
Ladhaye huzidi tamu, maneno yakipangika
Yenye kutoa elimu, watu wakaadilika
Ujumbewe ukadumu, muongozo ukatupa
Ndiyo tamu ya shairi, tungoni inovutiya
Sina mengi ya kunena, nisije nikakuchusha
Uwanda bado mpana, wapo watokujibisha
Kwa marefu na mapana, na maneno ya kutosha
Hoja utaianzisha, kama hukutoshezeka
Amour Seif Farsy (Mzanzibaria Halisi),
08 Juni 2011,
Dar es Salaam