Karima ni Mola wangu, uwezo kunijalia
Huu si uwezo wangu, kipaji kutunikiwa
Kutupa kalamu yangu, hekima kuwapatia
Ni lipi kosa langu, dharau kutunikiwa?
Hutafuta vilo vyangu, kusudi kusaidia
Kadiri ya uwezo wangu, muhanga kujitolea
Kuwaona ndugu zangu, baba mama wa pamoya
Ni lipi kosa langu, dharau kutunukiwa?
Nachoka enyi wenzangu, lakini navumilia
Tena naona uchungu, jamii ‘kiangamia
Najitahidi wenzangu, kusudi kukumbushia
Ni lipi kosa langu, dharau kutunukiwa?
Hawaasa ndugu zangu, futuko kunifanyia
Nimekasirisha mbingu, sijui wapi ‘tangia
Naona kizunguzungu, dunia ‘kinilemea
Ni lipi kosa langu, dharau kutunukiwa?
Kuwaonya wa wenzangu, iwe nd’o yangu fidia
Au sichangii changu, miongoni mwao pia
Waniona nungunungu, mtu nisiye sawia
Ni lipi kosa langu dharau, kutunukiwa?
Japo ya mdudu chungu, hapewa ningepokea
Najua nd’o langu fungu, Mola kanihifadhia
Kukosa ya walimwengu, atosha yeye Jalia
Lipi miye kosa langu, dharau kutunukiwa?
Amaan, Masoud Bakar
Zanzibar