KISWAHILI KINA WENYEWE

Upweke

Upweke waadhabisha, pekeyo unapokuwa
Maisha huwa yachosha, la raha karaha lawa
‘Kiona watu wacheka, utasema wazomewa
Upweke nao maradhi

Upweke watunyofowa, ndani kwa ndani watula
Wakondefu tushakuwa, kukosa zetu aila
Tuyafanyayo hayawa, twadhalilika madhila
Upweke nao ni nduli

Upweke wasononesha, myoyoni joto watia
Furaha waiondosha, arijojo ‘kapotea
Hata kijilazimisha, ‘taishia kupumbaa
Upweke si jambo zuri

Upweke ‘kikufumbata, maisha ‘tayachukiya
Sononeko sononeka, nani atakusikia?
Utatamani kucheka, ukose la kuchekea
Upweke ni pigo baya

Upweke ‘kikugubika, saa huwa zasimama
Dakika zikazunguka, zikenda kinyuma nyuma
Utachoka hangaika, usiweze tenda jema
Upweke nao watisha

Upweke sifaye chafu, wapiga nyoyo na macho
Utawa na kila kitu, usione kifaacho
Kuruba na wako watu, ndicho peke utakacho
Upweke haushindika

Nsikize nyimbo ipi, ya kunitoa upweke?
Ntende matendo yapi, upweke unikopoke?
Dawa ya upweke ipi, nibwie na nijipake?
Upweke gonjwa thakili

© Hamad Hamad
March 12, 2011
Copenhagen

1 thought on “Upweke”

  1. SWADAKTA BA HAMAD
    Ba Hamadi wanikuna, maneno uyanenayo
    Unavyovipanga vina, waugusa wangu moyo
    Upweke hauna mana, ukizowea wenzio
    Upweke ni ukatili

    Hata uwe na dinari, mafedha na mayakuti
    Au uwe jemedari, upigiwae saluti
    Upweke una hatari, utapata kibuhuti
    Upweke ! nh!

Leave a Reply

Fill in your details below or click an icon to log in:

WordPress.com Logo

You are commenting using your WordPress.com account. Log Out /  Change )

Facebook photo

You are commenting using your Facebook account. Log Out /  Change )

Connecting to %s

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.